Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 8 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 90 2016-11-09

Name

Josephine Johnson Genzabuke

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JOSEPHINE J. GENZABUKE aliuliza:-
Kwa muda mrefu sasa kumekuwa na malalamiko baina ya wakulima na Mamlaka ya Mapori ya Hifadhi ya Misitu, kwa sababu ya kuongezeka kwa watu lakini ardhi haiongezeki, hivyo kufanya ongezeko hili la watu wakose ardhi kwa shughuli zao za kilimo na mambo mengine yahusuyo ardhi:-
Je, ni lini Serikali italeta Bungeni Muswada wa Sheria husika ili kufanya marekebisho katika mipaka ya Hifadhi hizo ili kupata eneo la kilimo kwa wananchi walioongezeka ambao hawana maeneo ya kilimo.

Name

Prof. Jumanne Abdallah Maghembe

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Answer

WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Josephine Genzabuke, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kuwa idadi ya Watanzania inaongezeka siku hadi siku, ambapo 75% ya watu hao wanaishi vijijini na kwamba wananchi wengi wa vijijini wanategemea rasilimali za misitu na ardhi kwa ajili ya maisha yao. Pia, inaeleweka wazi kuwa kasi ya ongezeko la idadi ya watu linachangia katika kuongezeka kwa mahitaji ya mazao ya misitu na ardhi kwa ajili ya kilimo, ufugaji pamoja na makazi. Kukosekana kwa mipango ya matumizi bora ya ardhi ya vijiji, inachochea kuongezeka kwa kasi ya uharibifu wa misitu na ukosefu wa ardhi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na mahitaji makubwa na umuhimu wa ardhi katika kukidhi mahitaji ya wananchi na maendeleo ya kiuchumi, Serikali inatambua misitu ni muhimu kwa maisha ya viumbe hai, katika kupunguza hewa ukaa, kulinda hewa safi, kupunguza joto la ardhi, kutunza vyanzo vya maji, upatikanaji wa nishati na shughuli mbalimbali za kibinadamu. Hivyo, kwa kutambua umuhimu wa ustawi wa maisha ya wananchi na uhifadhi wa misitu, Serikali inaendelea kuchukua hatua zinazozingatia uwiano kati ya mahitaji ya maendeleo ya wananchi na uhifadhi wa misitu.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua changamoto zinazotokana na upungufu wa ardhi, Wizara inawashauri wananchi wote na Serikali za Vijiji vyote vinavyozunguka misitu ya hifadhi kushirikiana na sekta husika katika kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi itakayolenga kutenga maeneo kwa matumizi mbalimbali kufuatana na mahitaji katika maeneo yao.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu itaendelea kutoa ushirikiano katika kuandaa mipango ya matumizi bora ya ardhi ikiwa ni pamoja na hifadhi ya misitu. Vilevile, tunawaomba Waheshimiwa Wabunge kuwahamasisha wananchi kutumia mbinu za kilimo bora chenye tija na kuibua shughuli nyingine za kiuchumi ambazo hazihitaji matumizi makubwa ya ardhi kama vile ufugaji wa samaki, ufugaji wa nyuki, uanzishaji wa viwanda vidogovidogo na shughuli nyingine ambazo ni rafiki wa mazingira.