Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 53 2016-11-04

Name

Devotha Methew Minja

Sex

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. DEVOTHA M. MINJA aliuliza:-
Je, Serikali haioni kuwa kuna haja ya kupunguza gharama za upimaji viwanja ambazo ni kubwa sana ili kumwezesha kila Mtanzania kupata huduma hiyo na kuondoa migogoro ya ardhi?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Devotha Mathew Minja, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, nitoe kwanza maelezo ya awali kwa sababu swali hili juzi limejibiwa, liliulizwa pia na Mbunge wa Mbozi. Kwa hiyo, majibu nitakayoyatoa pengine yanaweza yakafanana na yale yale kwa sababu swali linafanana.
Mheshimiwa Mwenyekiti, upimaji wa ardhi hapa nchini unafanywa na wapima ardhi wa Serikali walioajiriwa na Serikali na wapima binafsi waliosajiliwa na Bodi ya Wapima Ardhi na kupewa leseni za biashara ya upimaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Serikali, gharama za upimaji rasmi kwa sasa ni Sh. 300,000/= kwa hekta moja ya shamba na pia kwa kiwanja kimoja. Gharama hizi zilipunguzwa na kuridhiwa na Bunge lako Tukufu mwaka 2015/2016 ambapo kabla ya hapo zilikuwa Sh. 800,000/= kwa hekta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kubwa za upimaji zinatokana na sababu zifuatazo:-
(i) Halmashauri nyingi nchini hazijajengewa uwezo wa wataalam na vifaa. Jukumu la kuajiri wataalam na kununua vifaa ni la Halmashauri zenyewe ila upungufu wa vifaa na wataalam ni mkubwa kwa nchi nzima.
(ii) Gharama za vifaa vya upimaji ni kubwa. Ili kupata seti moja ya kawaida ya upimaji kwa kutumia total station ni shilingi milioni 18 na seti moja ya GPS ni shilingi milioni 48. Ukubwa huu wa gharama za vifaa husababisha wapimaji wengi kutokuwa na uwezo wa kununua vifaa na hivyo kutegemea kukodi kwa gharama kubwa na hivyo kufanya pia upimaji kuwa ghali ili kuwezesha kurejesha gharama za vifaa.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na ongezeko la gharama za upimaji nchini, Serikali ina mpango wa kusogeza huduma zote zinazotolewa Wizarani kwenda kwenye kanda. Hatua hii itawezesha kanda hizo kujenga uwezo na hivyo kuchangia kupunguza gharama. Katika kuzijengea uwezo, Serikali inategemea kununua vifaa vya upimaji kupitia mradi wa Benki ya Dunia na kuvigawa vifaa hivyo kwenye kanda ambavyo vitasaidia Halmashauri katika kanda husika na hivyo kuwafikia Watanzania walio wengi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hili, nitoe rai kwa Halmashauri zote nchini kutenga bajeti kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya upimaji pamoja na kuajiri wataalam wa kutosha katika kada hii ya upimaji na wengine wa sekta ya ardhi ili kuondokana na gharama kubwa za kukodisha vifaa hivyo toka kwenye taasisi binafsi.