Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 1 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 12 2016-11-01

Name

Mwita Mwikwabe Waitara

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tarime Vijijini

Primary Question

MHE. MWITA M. WAITARA aliuliza:-
Suala la Mpango Miji ni jema na mtu aliyepimiwa ardhi na kupata hati ya eneo lake huweza kutumia hati hiyo kukopa kirahisi lakini gharama za kupima ardhi ni kubwa sana kiasi kwamba wananchi walio wengi wanashindwa kupima maeneo yao.
Je, Serikali ina mpango gani wa dharura wa kupunguza gharama za upimaji ardhi ili wananchi wengi zaidi waweze kupima maeneo yao na kuyaongezea thamani?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali namba 12 la Mheshimiwa Mwita Mwikabe Waitara, Mbunge wa Ukonga kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, upimaji wa ardhi hapa nchini unafanywa na Wapima wa Ardhi wa Serikali walioajiriwa na Serikali na Wapima Binafsi walioajiriwa na Bodi ya Wapima Ardhi na kupewa leseni za biashara ya upimaji.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa upande wa Serikali, gharama za upimaji rasmi kwa sasa ni shilingi 300,000 kwa hekta ya shamba moja na kiwanja kimoja. Gharama hizi zilipunguzwa na kuridhiwa na Bunge lako Tukufu kwa mwaka wa fedha 2015/2016 ambapo kabla ya hapo zilikuwa shilingi 800,000 kwa hekta.
Mheshimiwa Mwenyekiti, gharama kubwa za upimaji zinatokana na sababu zifuatazo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, jambo la kwanza, Halmashauri nyingi hazijajengewa uwezo wa wataalam na vifaa na jukumu la kuajiri wataalam na kununua vifaa ni la Halmashauri yenyewe hivyo upungufu wa vifaa pamoja na wataalam ni mkubwa kwa nchi nzima.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sababu ya pili ni kwamba gharama za vifaa vya upimaji ni kubwa sana na upatikanaji wa seti moja ya kawaida ya upimaji kwa kutumia darubini ni shilingi milioni 18 kwa seti moja na GPS ni shilingi milioni 48. Ukubwa huu wa gharama na vifaa husababisha wapima wengi kutokuwa na uwezo wa kununua vifaa na hivyo kutegemea kukodi kwa gharama kubwa hivyo kufanya pia upimaji kuwa ghali ili kuweza kurejesha gharama za vifaa kwa sababu ni vya kukodi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, katika kukabiliana na ongezeko la gharama za upimaji nchini, Serikali ina mpango wa kusogeza huduma zote zinazotolewa Wizarani kwenda kwenye kanda. Hatua hii itawezesha kanda hizo kujengewa uwezo na hivyo kuchangia kupunguza gharama. Katika kuzijengea uwezo, Serikali inategemea kununua vifaa vya upimaji katika mradi wa World Bank na kuvigawa katika kanda zake ambavyo vitasaidia Halmashauri katika kanda husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, sambamba na hilo, nitoe rai kwa Halmashauri zote nchini kutenga bajeti kwa ajili ya ununuzi wa vifaa vya upimaji pamoja na kuajiri wataalam wa kutosha katika kada hii ya upimaji na wengine wa sekta ya ardhi ili kuondokana na gharama kubwa za kukodisha vifaa hivyo kutoka katika taasisi binafsi.