Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 5 Sitting 1 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 06 2016-11-01

Name

Ignas Aloyce Malocha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Kituo cha afya kilichopo Laela kinategemewa na Kata za Lusaka, Kasanzama, Laela, Mnokola, Miangalua na Kaoze; kutokana na kupanuka kwa kasi kwa mji huo na ongezeko la watu wanaohudumiwa katika kituo hicho, kimesababisha upungufu wa dawa, wataalamu na vifaa tiba.
(a) Je, ni lini Serikali itakipa kituo hicho hadhi ya Hospitali ya Wilaya?
(b) Je, ni lini kituo hicho kitapatiwa gari la wagonjwa?
(c) Je, ni lini Serikali itapeleka wataalam wa kutosha, vifaa tiba na dawa za kutosha katika kituo hicho?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa sasa Kituo cha Afya Laela hakina miundombinu inayokidhi sifa za kuwa hospitali, kazi inayofanyika kwa sasa ni upanuzi wa miundombinu ya kituo hicho ambapo tayari jengo la upasuaji wa dharura kwa mama wajawazito limekamilika pamoja na wodi ya mama wajawazito na wodi ya wagonjwa waliofanyiwa upasuaji. Aidha, mpango wa muda mrefu katika eneo hilo ni kujenga Hospitali ya Wilaya kukidhi mahitaji ya matibabu kwa wagonjwa wanaotembea umbali mrefu kufuata huduma hiyo.
(b) Mheshimiwa Mwenyekiti, huduma za rufaa kwa wagonjwa wanaohudumiwa katika kituo hicho kwa sasa zinatolewa kupitia magari ya kawaida ya Halmashauri kutokana na ukosefu wa gari la kubebea wagonjwa. Ni matarajio ya Wizara kwamba Halmashauri itaweka kipaumbele katika kutenga bajeti katika mwaka wa fedha 2017/2018 kwa ajili ya ununuzi wa gari la wagonjwa.
(c) Mheshimiwa Mwenyekiti, upungufu wa watumishi katika Kituo cha Afya Laela ni tisa kati ya 45 wanaohitajika. Katika mwaka wa fedha 2016/2017, Halmashauri imepewa kibali cha kuajiri watumishi wapya wapatao 42 ambapo baadhi yao watapelekwa kituoni hapo. Kuhusu dawa na vifaa tiba, kituo kimetengewa bajeti ya shilingi bilioni 9.3 katika bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017 kwa ajili ya ununuzi wa dawa na vifaa tiba.