Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 7 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 89 2016-02-03

Name

Atupele Fredy Mwakibete

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Busokelo

Primary Question

MHE. ATUPELE F. MWAKIBETE aliuliza:-
Wananchi wa Bonde la Mwakaleli, Kata za Kandete, Isange na Luteba wanaoishi kando ya Hifadhi ya TANAPA wamekuwa wakinyanyaswa sana na watumishi wa TANAPA kwa kisingizio kwamba wamevamia Hifadhi wakati TANAPA ndio waliovamia makazi ya wananchi kwa kuweka mipaka mipya tofauti na ile ya zamani hali inayofanya baadhi ya shule na taasisi zingine kuonekana kuwa ndani ya Hifadhi ya TANAPA kwa sasa:-
Je, ni lini Serikali itarudisha mipaka ya zamani ili wananchi wasiendelee kuishi kwa wasiwasi, lakini pia waendelee na shughuli za kilimo kama ilivyokuwa zamani?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Atupele Fredy Mwakibete, Mbunge wa Busokelo, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Msitu wa Livingstone ulikuwa Msitu wa Hifadhi yaani Forest Reserve ulioanzishwa kwa Tangazo la Serikali Na. 48 la mwaka 1940, kwa lengo la kutunza vyanzo vya maji vya Ziwa Nyasa na baianuwai nyingine muhimu. Wananchi wa Kata za Kandete, Isange na Luteba katika Jimbo la Rungwe Mashariki mnamo mwaka 1945 walianza taratibu kuingia katika msitu huo na kufanya shughuli za kibinadamu ikiwa ni pamoja na makazi, kilimo na ufugaji, kinyume na Tangazo la Serikali.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ili kunusuru vyanzo muhimu vya maji vya Ziwa Nyasa na baianuwai muhimu ndani ya msitu, Serikali iliamua kubadilisha hadhi ya Msitu wa Livingstone kutoka Forest Reserve kuwa Hifadhi ya Taifa Kitulo, iliyotangazwa rasmi katika Gazeti la Serikali Na. 279 la mwaka 2005, baada ya hatua zote muhimu za Kiserikali kukamilika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, baada ya Tangazo hilo la Serikali la mwaka 2005, mnamo mwaka 2007 lilifanyika zoezi la uhakiki na uwekaji wa mawe ya mipaka ya hifadhi zoezi ambalo lilishirikisha wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi na wadau wengine muhimu ikiwa ni pamoja na Halmashauri ya Wilaya ya Rungwe, Menejimenti ya Hifadhi ya Taifa Kitulo na viongozi wa vijiji husika.
Mheshimiwa Mwenyekiti, zoezi la uhakiki na uwekaji mipaka kwa eneo lote la hifadhi lilikamilika mwaka 2010. Aidha, katika zoezi hilo ilibainika kuwa baadhi ya mashamba, makazi na miundombinu ya taasisi kama vile shule na kanisa, vimo ndani ya mipaka ya hifadhi na hivyo kusababisha migogoro kati ya hifadhi na wananchi, mgogoro ambao unahitaji kupatiwa ufumbuzi wa pamoja baina ya Serikali na wananchi.
Mheshimiwa Mwenyekiti, ufumbuzi wa kudumu wa suala hili unafanyiwa kazi na Shirika la Hifadhi za Taifa, kwa niaba ya Wizara yangu kwa kushirikiana na wataalam wa Wizara ya Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi pamoja na uongozi wa Mkoa wa Mbeya na unatarajiwa kukamilika katika kipindi cha mwaka mmoja. Wakati suala hili likisubiri kupatiwa ufumbuzi, wananchi wawe wavumilivu kwa kutofanya shughuli za uharibifu wa mazingira katika maeneo husika.