Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 5 Foreign Affairs and International Cooperation Wizara ya Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki 70 2016-09-13

Name

Angelina Adam Malembeka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ANGELINA ADAM MALEMBEKA aliuliza:-
Ofisi nyingi za Balozi zetu katika nchi mbalimbali zimekodishwa. Aidha, ofisi nyingine ujenzi haujakamilika au hazijafanyiwa ukarabati kwa muda mrefu sasa na ofisi nyingine zina madeni makubwa.
(a) Je, ni lini ujenzi wa baadhi ya ofisi za Ubalozi zitakamilika ikiwemo ya Msumbiji?
(b) Je, Serikali ina mkakati gani wa kukarabati ofisi chache za Ubalozi zilizopo pamoja na kununua samani mpya?
(c) Je, kwa nini Serikali isilipe madeni ya Balozi zetu kwa wakati ili kuepusha aibu kwa Taifa?

Name

Dr. Augustine Philip Mahiga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI KILIMO, MIFUGO NA UVUVI (K.n.y. WAZIRI WA MAMBO YA NJE NA USHIRIKIANO WA AFRIKA MASHARIKI) alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Nje na Ushirikiano wa Afrika Mashariki, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Angelina Adam Malembeka, Mbunge, lenye sehemu (a), (b) na (c) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, ujenzi wa ofisi na makazi ya Balozi zetu umekuwa ukitekelezwa kwa awamu kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha za bajeti ya maendeleo. Mwaka wa fedha 2016/2017, Wizara ilipanga kutekeleza miradi ya ujenzi katika Balozi zake ikiwemo Maputo, Nairobi na Stockholm na uboreshaji wa mifumo ya mawasiliano kati ya Balozi na Makao Makuu wa Wizara. Mradi wa Maputo umepangiwa shilingi 1,316,435,000. Tunategemea utekelezaji wa mradi huu ufanyike pale Wizara itakapopokea fedha kutoka Hazina.
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kutambua kuwa fedha za bajeti ya maendeleo hazikidhi mahitaji, Wizara inaendelea kushirikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii kama vile Mfuko wa Taifa wa Hifadhi ya Jamii (NSSF) na Taasisi ya Miradi ya Maendeleo ya Miundombinu katika ujenzi wa majengo ya ofisi na vitega uchumi katika Balozi zetu. Wizara inaamini uamuzi wa kuishirikisha mifuko hiyo itaongeza kasi ya ujenzi wa majengo ya ofisi katika Balozi zetu.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, mkakati wa Wizara uliopo hizi sasa katika kukarabati majengo ya ofisi yaliyopo kwenye Balozi zetu ni kuendelea kuiomba Serikali kutenga fedha za bajeti ya maendeleo; pili, kuelekeza Balozi zetu kutumia utaratibu wa karadha (mortgage finance) ili kuwezesha Balozi kupata fedha za ukarabati, kununua na kujenga majengo ya ofisi na vitega uchumi; na tatu, kuishirikisha Mifuko ya Hifadhi ya Jamii iliyopo nchini kutekeleza miradi ya Wizara Balozini kwa Wizara kuingia makubaliano na vyombo hivyo. Aidha, Wizara itaendelea na utaratibu wa kununua kwa awamu samani mpya za ofisi kwa kuzingatia upatikanaji wa fedha.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, Serikali katika nyakati tofauti imekuwa ikitoa fedha kwa ajili ya kulipa madeni ya Balozi zake nje. Serikali ilitoa kiasi cha shilingi 7,315,720,301.84 kulipa madeni ya Wizara yaliyohakikiwa na Wakaguzi wa Hesabu. Hadi kufikia tarehe 30 Juni, 2016 deni lililobaki ni shilingi 15,540,603,526. Madeni haya yameanza kukaguliwa na Hazina, hivyo ni matarajio yetu kuwa baada ya kukamilika kwa ukaguzi huo, Hazina itatoa fedha za kulipa madeni hayo.
Mheshimiwa Naibu Spika, hata hivyo, katika mwaka wa fedha 2016/2017 Hazina imetoa mwongozo unaoelekeza kuandaa mpango wa bajeti ambao unaelekeza madeni yote ya Wizara, Wakala na Taasisi za Serikali kulipwa moja kwa moja na Hazina.