Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 6 Investment and Empowerment Ofisi ya Rais TAMISEMI. 72 2016-09-14

Name

Esther Lukago Midimu

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER L. MIDIMU aliuliza:-
Wanawake katika Mkoa wa Simiyu wamehamasika sana kujiunga kwenye vikundi ili kukusanya nguvu za kiuchumi kwa lengo la kujiendeleza kiuchumi zaidi.
Je, Serikali ina mpango gani wa kuwapatia wanawake hawa mafunzo ya kimtaji ili waweze kufanya shughuli zao za kiuchumi kwa ufanisi zaidi?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Lukago Midimu, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali imekuwa ikiwawezesha kiuchumi wanawake kupitia Mfuko wa Maendeleo ya Wanawake ambao kila Halmashauri inatakiwa kutenga asilimia tano ya mapato yake ya ndani. Katika mwaka wa fedha 2015/2016, Mkoa wa Simiyu ulitoa mikopo kwa wanawake na vijana yenye thamani ya shilingi milioni 116.5 ambapo kati ya hizo wanawake walikopeshwa shilingi milioni 75.7 kwa vikundi vipatavyo 74. Kwa mwaka wa fedha 2016/2017 Mkoa wa Simiyu umetenga shilingi milioni 978.08 kwa ajili ya vijana na wanawake.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Halmashauri zote zimeelekezwa kulipa madeni ya fedha ambazo hazikupelekwa kwenye Mifuko ya Vijana na Wanawake kwa mwaka wa fedha 2015/2016. Aidha, kwa mwaka wa fedha 2016/2017 Ofisi ya Rais, TAMISEMI kwa kushirikiana na Hazina iliweka kigezo kwa kila Halmashauri kuonesha fedha zilizotengwa kwa ajili ya vijana na wanawake kabla ya kupitisha bajeti yake na Halmashauri zote zimetenga fedha hizo jumla ya shilingi bilioni 56.8.
Mheshimiwa Mwenyekiti, kuhusu mafunzo, Halmashauri kupitia Idara ya Maendeleo ya Jamii zimeendelea kutoa elimu ya masuala ya biashara na ujasiriamali kwa vikundi vya wanawake na vijana kabla na baada ya kupata mikopo ili kuhakikisha kwamba mikopo inayotolewa inatumika na kusimamiwa ipasavyo. Katika utekelezaji wa jukumu hili, Serikali inashirikiana na sekta binafsi zikiwemo asasi za kiraia.