Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 36 Health and Social Welfare Ofisi ya Rais TAMISEMI. 294 2016-06-03

Name

Raphael Michael Japhary

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. EMANUEL A. MWAKASAKA (K.n.y MHE. RAPHAEL J. MICHAEL) aliuliza:-
Hospitali ya Mawenzi ambayo ni ya Rufaa ya Mkoa wa Kilimanjaro inakabiliwa na changamoto mbalimbali kama vile uchakavu wa miundombinu yake, samani, mlundikano mkubwa wa wagonjwa kwa sababu Manispaa ya Moshi haina Hospitali ya Wilaya, upungufu wa Madaktari, wauguzi na wahudumu wengine wa afya:-
(a) Je, ni lini hospitali hiyo itafanyiwa ukarabati ili iweze kufanya kazi zake kwa ufanisi na kuiongezea watumishi niliowataja?
(b) Je, ni lini Serikali itakubali ombi la Halmashauri ya Manispaa ya Moshi la kujenga Hospitali ya Wilaya?
(c) Je, Serikali itasaidiaje Hospitali ya Mawenzi iweze kupata mkopo kutoka Benki ya Rasilimali Tanzania (TIB) ili iweze kuboresha miundombinu yake?

Name

Dr. Selemani Said Jafo

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kisarawe

Answer

NAIBU WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, TAWALA ZA MIKOA NA SERIKALI ZA MITAA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Nchi, Ofisi ya Rais, TAMISEMI, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Raphael Japhary Michael, Mbunge wa Moshi Mjini, lenye sehemu (a), (b) na (c), kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, mkoa umejiwekea utaratibu wa kufanya ukarabati wa Hospitali ya Mkoa kupitia fedha za uchangiaji wa gharama za matibabu. Hadi sasa zimeshatumika Sh. 14,700,000/= kwa ajili ya ukarabati wa mfumo wa maji, jengo la wagonjwa wa nje pamoja na jengo la Madaktari waliopo mafunzoni (intern doctors). Mkakati uliowekwa ni kuimarisha makusanyo ya mapato ili kujenga uwezo wa kuihudumia hospitali hiyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu suala la watumishi, hospitali hiyo imepata kibali cha kuajiri watumishi wapya 79, katika mwaka wa fedha 2015/2016 na watumishi 65 wamepangwa kuajiriwa katika mwaka ujao wa 2016/2017 ili kukabiliana na upungufu huo.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, kwa sasa Wilaya ya Moshi imeingia ubia wa utoaji huduma na Hospitali ya Mtakatifu Joseph (DDH) ambayo itatumika kama Hospitali ya Wilaya. Ili kuendelea kuboresha huduma za afya, Halmashauri imeamua kukiboresha Kituo cha Afya cha Msaranga ili kukiongezea uwezo wa kutoa huduma zenye hadhi ya hospitali.
(c) Mheshimiwa Naibu Spika, ili kuhakikisha ukarabati wa miundombinu ya Hospitali ya Mawenzi unafanyika, Serikali imetenga shilingi bilioni 1.35 katika Bajeti ya mwaka wa fedha 2016/2017. Aidha, kuhusu suala la mkopo kutoka TIB, Mkoa unashauriwa kukamilisha mazungumzo yanayoendelea na yatakapowasilishwa Ofisi ya Rais, TAMISEMI tutatoa ushirikiano baada ya kuridhishwa kama mkopo huo umekidhi vigezo vinavyozingatiwa katika tathmini ya mikopo ya aina hii.