Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 39 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 333 2016-06-09

Name

Ignas Aloyce Malocha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kwela

Primary Question

MHE. IGNAS A. MALOCHA aliuliza:-
Mbuga ya Akiba ya Uwanda katika Wilaya ya Sumbawanga Vijijini ilitengwa miaka ya nyuma wakati idadi ya watu ikiwa ndogo sana ikilinganishwa na sasa.
(a) Je, Serikali ina mpango gani wa kulipunguza pori hilo ili kunusuru shida inayowapata wananchi wanaozunguka eneo hilo ya kukosa maeneo ya kilimo na ufugaji?
(b) Je, kwa nini wananchi wa maeneo hayo wanapigwa na Askari wa Wanyamapori na kunyang’anywa mali zao, wakati hakuna alama yoyote inayoonyesha mpaka katika mbuga hiyo?
(c) Je, wananchi wa vijiji vinavyozunguka pori hilo wamenufaika na nini zaidi ya vipigo wanavyovipata?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ignas Aloyce Malocha, Mbunge wa Kwela, lenye sehemu (a), (b) na (c) kwa pamoja kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Akiba Uwanda lenye ukubwa wa kilometa za mraba 5,000 lilianzishwa mwaka 1959 na kutangazwa upya kwa Sheria ya Uhifadhi Wanyamapori Namba 12 ya mwaka 1974, kwa tangazo la Serikali namba 275 la tarehe 8 Novemba, 1974. Kati ya mwaka 1974 na 2013 pori hilo lilikuwa chini ya usimamizi ya Halmashauri ya Wilaya ya Sumbawanga ambapo lilikabidhiwa rasmi kwa Wizara ya Maliasili na Utalii tarehe 20 Januari, 2014.
Mheshimiwa Naibu Spika, pori hili linazungukwa na jumla ya vijiji tisa ambapo asilimia kubwa ya wakazi wake wanajihusisha na shughuli za kilimo, uvuvi na ufugaji. Umuhimu wa pori hili umejikita katika uhifadhi wa rasilimali wanyamapori, mimea na mazalia ya samaki katika Ziwa Rukwa ambayo ni mojawapo ya vyanzo vikuu vya kiuchumi kwa wananchi wa eneo hilo. Pamoja na umuhimu huo, Pori la Akiba Uwanda kama yalivyo maeneo mengine ya hifadhi, linakabiliwa na changamoto ya ongezeko la shughuli za kibinadamu.
Mheshimiwa Naibu Spika, aidha, eneo kubwa la pori hili ni sehemu ya Ziwa Rukwa, na sehemu iliyobaki yenye eneo la kilometa za mraba 400 ni nchi kavu. Kutokana na umuhimu huo Wizara yangu inaona ni mapema kupunguza ukubwa wa pori hilo kwa sababu uamuzi huo utaathiri sababu na malengo ya kuanzishwa kwake. Hata hivyo, Serikali kwa upana wake itajumuisha eneo hili la Pori la Akiba la Uwanda, kuwa miongoni mwa maeneo yanayotarajiwa kushughulikiwa kimkakati zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu haikubaliani na vitendo vya baadhi ya watumishi wake, wakiwemo Askari Wanyamapori kujichukulia sheria mkononi kwa kuwapiga, kuwanyang’anya mali, kuwatoza faini kinyume cha utaratibu, kuwachomea moto nyumba zao, na kuwanyanyasa kwa namna yoyote ile, kwa kisingizio cha kutekeleza matakwa ya sheria. Wizara yangu inasisiza msimamo wa Serikali wa kuendelea kusimamia utawala wa sheria, na hivyo kujipanga zaidi, ili kuchukua hatua kali dhidi ya watumishi watakaodhibitika kukiuka, kwa mujibu wa sheria, kanuni, na taratibu.
Mheshimiwa Naibu Spika, wananchi wanaombwa, kutoa ushirikiano katika kuwabaini watumishi wa aina hii, na pia wachukue hatua stahiki kabla, wakati na baada ya matukio ya aina hiyo ili kuirahisishia Serikali kuchukua hatua sahihi kwa wakati sahihi. Hata hivyo Wizara yangu inasisitiza kuwa wananchi wanaoishi katika maeneo yanayopakana na hifadhi, wazingatie na kutii sheria bila shuruti. Ili hifadhi hizo ziendelee kuleta manufaa kwa taifa wakiwemo wananchi hao kwa tija zaidi.
Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na kwamba ni kipindi kifupi tu, takribani miaka miwili na nusu tangu usimamizi wa Pori la Akiba Uwanda, ukabidhiwe kwa Wizara yangu. Tayari tumeanza mkakati wa kuwekeza kwa kuboresha miundombinu na vivutio ili kuhakikisha kwamba pori hilo linarudi kwenye hadhi yake ya awali. Kabla ya kufanyika kwa shughuli za utalii zitakazoiwezesha Serikali kushughulikia ipasavyo changamoto za maendeleo ya wananchi. Azma hii inaendana na mipango ya Serikali ya muda mrefu ya kuboresha shughuli za utalii Ukanda wa Kusini.