Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 40 Investment and Empowerment Ofisi ya Rais TAMISEMI. 337 2016-06-10

Name

Halima Ali Mohammed

Sex

Female

Party

CUF

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MWANNE I. MCHEMBA (K.n.y. MHE. HALIMA ALI MOHAMMED) aliuliza:-
Serikali imejipanga kupiga vita suala la ajira kwa watoto na imekuwa ikiunga mkono matamko ya Umoja wa Mataifa kuhusiana na ajira za watoto.
Je, kupitia Mradi wa TASAF III Serikali ina mikakati gani ya makusudi kuwasaidia watoto na tatizo la ajira za utotoni kwa upande wa Zanzibar?

Name

Angellah Jasmine Mbelwa Kairuki

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

WAZIRI WA NCHI, OFISI YA RAIS, MENEJIMENTI YA UTUMISHI WA UMMA NA UTAWALA BORA alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Halima Ali Mohamed, Mbunge wa Viti Maalum, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Mpango wa Kunusuru Kaya Maskini au TASAF III ulianza utekelezaji wake mwezi Agosti mwaka 2012. Hadi kufikia mwezi Machi, 2016, mpango umeandikisha jumla ya kaya milioni 1.1 Tanzania Bara na Zanzibar. Kati ya hizo, kaya 33,532 zimeandikishwa na zinapata ruzuku ya malipo kwa upande wa Tanzania Zanzibar.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika utekelezaji, mpango unatilia mkazo uhawilishaji wa fedha kwa kaya maskini zilizoandikishwa. Uhawilishaji wa fedha umeziwezesha kaya hizi maskini kuwa na uhakika wa chakula, kupata huduma za afya na kuwawezesha watoto walio na umri wa kwenda shule kuanza shule na kwa walio katika shule za msingi na sekondari kupata mahitaji muhimu ya shule. Aidha, kaya hizi zinapata kipato cha ziada kupitia ajira za muda kwa wanakaya wenye uwezo wa kufanya kazi kwa kufanya kazi kwenye miradi midogo-midogo inayotekelezwa na TASAF.
Mheshimiwa Naibu Spika, uhawilishaji wa fedha kwa kaya maskini umewezesha watoto waliokuwa katika ajira za utotoni katika maeneo mbalimbali kwa ajili ya kuongeza kipato cha kaya kutoka katika ajira hizo na kuweza kuhudhuria shule kwa kiwango cha 80% au zaidi. Kwa wale ambao hawajafikia umri wa kwenda shule waliweza kupata huduma za afya kwa kufuata taratibu za sekta husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, utaratibu uliowekwa unashirikisha viongozi wa maeneo ya utekelezaji katika ngazi zote kufuatilia mahudhurio ya watoto shuleni ili waweze kufikia viwango vilivyowekwa. Kwa kaya ambazo watoto wao hawafikishi idadi ya siku zilizopangwa za kwenda shule hupunguziwa ruzuku kama njia ya kuwahimiza kutimiza masharti ya kuhakikisha kwamba watoto wao wanahudhuria shuleni ipasavyo.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni mategemeo ya Serikali kwamba Waheshimiwa Wabunge watashirikiana na viongozi wa Serikali katika ngazi zote ili kufanikisha mpango huu kwa kuhakikisha kwamba watoto walio na umri wa kwenda shule wanaotoka katika kaya maskini wanaandikishwa na kutimiza masharti ya Mpango kwa kuhudhuria shule kama inavyotakiwa.