Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 6 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 66 2016-02-02

Name

Marwa Ryoba Chacha

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Serengeti

Primary Question

MHE. MARWA R. CHACHA aliuliza:-
Wananchi wa Serengeti wamekuwa wakiathirika sana na wanyamapori hususan tembo ambao huharibu na kula mazao ya wananchi katika mashamba yao na kuikosesha Halmashauri mapato:-
(a) Je, Serikali itarejesha chanzo cha mapato yaani bed fee na sehemu ya gate fee kwa Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti?
(b) Makampuni mengi ndani ya hifadhi yanagoma kulipa ushuru wa huduma (service levy) kwa Halmashauri. Je, Serikali inaisaidiaje Halmashauri ya Wilaya ya Serengeti kupata ushuru huu wa huduma?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Marwa Ryoba Chacha, Mbunge wa Serengeti, lenye sehemu (a) na (b) kama ifuatavyo:-
(a) Mheshimiwa Naibu Spika, Sheria ya Utalii Na. 29 ya mwaka 2008 ilifuta Sheria ya Hoteli Sura ya 105 ya mwaka 2006 iliyokuwa inaruhusu tozo za bed fee ambapo Tozo ya Maendeleo ya Utalii ilianzishwa. Tozo ya Kitanda Siku (Bed Night Levy) ambayo ni sehemu ya Tozo ya Maendeleo ya Utalii hukusanywa na Mamlaka ya Mapato Tanzania kwa niaba ya Wizara ya Maliasili na Utalii. Tozo ya Maendeleo ya Utalii hugharimia shughuli za kuendeleza utalii nchini ikiwa ni pamoja na kutangaza vivutio vya utalii, kupanga hoteli kwenye daraja na kugharamia masuala ya kitaaluma yanayohusiana na utalii.
Mheshimiwa Naibu Spika, Shirika la Hifadhi za Taifa linayo mamlaka kisheria kusimamia kulinda na kuendeleza Hifadhi za Taifa. Aidha, makusanyo ya Gate Fee hufanywa na TANAPA ambapo kupitia vitengo vyake vya ujirani mwema vilivyoko kwenye kila hifadhi, huchangia moja kwa moja kwenye miradi ya maendeleo na huduma za kijamii pamoja na kutoa elimu ya mazingira kwa vijiji vinavyozunguka hifadhi hizo.
Kwa upande Wilaya ya Serengeti, kati ya mwaka wa fedha 2004/2005 mpaka 2014/2015, TANAPA iligharimia miradi 37 ya maendeleo na huduma za kijamii yenye thamani ya jumla ya shilingi 1,521,362,239.71.
(b) Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu inayo taarifa kwamba kumekuwapo na mabishano ya kisheria baina ya Makampuni yanayotoa huduma kwa watalii na Halmashauri kuhusu uhalali wa makampuni hayo kulipa ushuru wa huduma, yaani Service Levy. Suala hili lipo Mahakama ya Rufaa ya Tanzania, Civil Appeal No. 135 ya mwaka 2015 na kwa sababu hiyo, ni vema likasubiri maamuzi ya Mahakama. (Makofi)