Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 Sitting 7 Home Affairs Wizara ya Mambo ya Ndani ya Nchi 82 2016-02-03

Name

Khatib Said Haji

Sex

Male

Party

CUF

Constituent

Konde

Primary Question

MHE. KHATIB SAID HAJI aliuliza:-
Matukio ya wananchi kujichukulia sheria mkononi yamezidi kuongezeka siku hadi siku na kusababisha madhara na vifo kwa watu wasio na hatia:-
Je, Serikali inafanya juhudi gani ili kupunguza au kuondoa kabisa ukatili huu?

Name

Eng. Hamad Yussuf Masauni

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Kikwajuni

Answer

NAIBU WAZIRI WA MAMBO YA NDANI alijibu:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, kwa niaba ya Mheshimiwa Waziri wa Mambo ya Ndani ya Nchi, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Khatib Said Haji, Mbunge wa Konde, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Mwenyekiti, vitendo vya mtu ama watu kujichukulia sheria mikononi ni uhalifu ambao umeanza kushamiri katika jamii yetu ikiwemo Visiwa vya Zanzibar katika kipindi cha mwaka 2013/2014. Jumla ya matukio 2,041 yaliripotiwa katika vituo mbalimbali vya polisi nchini.
Mheshimiwa Mwenyekiti, mwaka 2013 kulikuwa na matukio 1,112 ambapo Zanzibar yaliripotiwa matukio 14. Mwaka 2014 yalipungua na kufikia matukio 929, kati ya hayo Zanzibar yalikuwa ni matukio matano. Aidha, matukio yote yalichukuliwa hatua stahiki ikiwemo wahusika kukamatwa na kufikishwa Mahakamani.
Mheshimiwa Mwenyekiti, Serikali kupitia Jeshi la Polisi, limekuwa likichukua hatua mbalimbali za kupambana na wimbi la uhalifu huo, miongoni mwa juhudi hizo ni pamoja na kutoa elimu kwa umma juu ya umuhimu wa kufuata sheria. Aidha, Jeshi la Polisi huwakamata na kuwafikisha Mahakamani watu wanaojichukulia sheria mkononi, kutenda makosa mbalimbali ya jinai.
Mheshimiwa Mwenyekiti, naomba kutumia fursa hii kupitia Bunge lako Tukufu, kutoa rai kwa wananchi wote kujiepusha na vitendo vya kujichukulia sheria mkononi, naomba Waheshimiwa Wabunge wote kushirikiana na Serikali kuwaelimisha wananchi kuepuka vitendo hivyo.