Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 4 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 50 2016-09-09

Name

Frank George Mwakajoka

Sex

Male

Party

CHADEMA

Constituent

Tunduma

Primary Question

MHE. FRANK G. MWAKAJOKA aliuliza:-
Je, ni lini Serikali itatumia wataalam wake katika kupanga Miji na kuondokana na ujenzi holela unaoendelea nchi nzima?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Frank George Mwakajoka, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu imeshaanza kushughulikia jambo hili kwa kuhakikisha kuwa katika kila Kanda tulizoanzisha tunapeleka wataalam wa kutosha wa fani zote. Hii yote ni kuhakikisha kuwa usimamizi wa uendelezaji miji nchini unakuwa katika viwango vinavyokubalika. Aidha, pamoja na jitihada hizo bado tuna changamoto kubwa ya uhaba wa maeneo yaliyopangwa na kupimwa nchini ambayo pia ni chimbuko la ujenzi holela katika nchi yetu.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kukabiliana na changamoto hii, Wizara yangu imekuwa ikichukua hatua mbalimbali ikiwa ni pamoja na:-
(i) Kuandaa program ya miaka mitatu ya kuandaa mipango kabambe ya Miji, Manispaa na Halmashauri za Miji yote Tanzania. Utayarishaji wa mipango kambambe ya Miji ya Mwanza, Musoma, Singida, Kibaha, Tabora, Iringa na Mtwara upo katika hatua za kutangazwa katika gazeti la Serikali ndani ya siku 90 ili watu waweze kutoa maoni yao.
Katika Jiji la Dar es Salaam zoezi hili bado halijakamilika lakini pia katika Jiji la Arusha zoezi hili halijakamilika kwa sababu zile Halmashauri hazikuelewana kwa hiyo, inabidi wakae waridhie. Aidha, katika mwaka wa fedha 2015, Wizara yangu pia ilitoa wataalam wa Mipango Miji kusaidia utayarishaji wa mipango kabambe katika Miji ya Iringa, Mtwara na Shinyanga. (Makofi)
(ii) Vilevile, Wizara imeendelea kuhakikisha kuwa kila kipande cha ardhi kinapimwa nchi nzima na Serikali imeshaanza kufanya upimaji katika Wilaya ya Kilombero, Ulanga na Malinyi kupitia mpango wa Land Tenure Support Progamme.
(iii) Kuruhusu makampuni binafsi ya Mipango Miji kushiriki katika kutayarisha mipango kabambe na mipango ya kina katika miji yote nchini.
(iv) Wizara pia ilitoa wataalam katika zoezi la urasimishaji makazi katika Manispaa ya Kinondoni katika Kata za Kimara na Saranga na katika Halmashauri ya Wilaya ya Makete katika Kata ya Tandala. Katika mwaka huu wa fedha Wizara yangu inatarajia kupeleka wataalam katika Halmashauri za Manispaa ya Sumbawanga, Lindi, Kigoma Ujiji, Singida, Musoma na Tabora kwa ajili ya kuwezesha zoezi kama hilo.
(v) Vilevile kuzijengea uwezo Halmashauri nyingine ili ziweze kurasimisha maeneo yao kwa kutumia wataalam wake. Hii ni utekelezaji wa program ya miaka mitano ya urasimishaji wa maeneo ambayo hayajapangwa, ambapo Wizara yangu imeandaa mwongozo wa namna ya kufanya urasimishaji, mwongozo utakapokamilika utasambazwa katika Halmashauri zote.
Mheshimiwa Naibu Spika, nitoe rai kwa Halmashauri zote kuandaa mipango kabambe ya maeneo ambayo yamefikia hadhi ya kuanzishwa kuwa miji ili upimaji ufanyike mapema kwa lengo la kuepusha ujenzi holela. Aidha, kwa maeneo ambayo yamejengwa kiholela Wizara yangu kwa kushirikiana na Halmashauri na wananchi wa maeneo husika tutaendelea kuboresha kwa kuyarasimisha kwa kadri ya mahitaji. (Makofi)