Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 42 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 357 2016-06-14

Name

Njalu Daudi Silanga

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Itilima

Primary Question

MHE. KISWAGA B. DESTERY (K.n.y. MHE. NJALU D. SILANGA) aliuliza:-
Mheshimiwa Rais kwenye kampeni za uchaguzi aliahidi kupanua mpaka wa Game Reserve iliyoko Maswa:-
Je, ni lini ahadi hiyo itatekelezwa?

Name

Eng. Ramo Matala Makani

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Tunduru Kaskazini

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Njalu Daudi Silanga, Mbunge wa Itilima, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Akiba Maswa lilianzishwa kisheria kwa Tangazo la Serikali Namba 270 la mwaka 1962. Pori hilo ni sehemu muhimu ya uhifadhi wa baioanuai katika mfumo wa ikolojia ya Serengeti ambayo inatoa mchango muhimu kwa viumbe mbalimbali wanaopatikana katika maeneo hayo ikiwemo kutunza vyanzo vya maji kwa mahitaji ya binadamu na shughuli za kiuchumi hususan utalii. Kwa muda mrefu tokea kuanzishwa kwa pori hili, wananchi wa vijiji husika wamekuwa wakinufaika na pori hili kwa shughuli mbalimbali za kiuchumi, upatikanaji wa ajira na mgao wa fedha ambapo asilimia 25 ya mapato yatokanayo na shughuli za uwindaji wa kitalii hutolewa kwa Halmashauri ya Wilaya husika.
Mheshimiwa Naibu Spika, Pori la Akiba la Maswa limefanyiwa marekebisho ya mpaka mara tano katika jitihada za kutatua changamoto ya mahitaji ya ardhi kwa wananchi wanaoishi jirani na pori hili. Hata hivyo, uamuzi wa kumega ardhi ya pori hili kwa kurekebisha mipaka mara kwa mara haujaweza kukidhi haja ya kumaliza tatizo hili kwa namna endelevu.
Mheshimiwa Naibu Spika, chanzo kikuu cha changamoto hii ni ukosefu wa mpango wa matumizi bora ya ardhi ambapo wananchi huendelea na utamaduni wa kumiliki idadi kubwa ya mifugo inayozidi uwezo wa maeneo ya malisho na kilimo cha kuhamahama. Uzoefu umeonyesha kuwa umegaji wa ardhi kwa namna ulivyofanyika siku za nyuma si suluhu endelevu ya tatizo la migogoro kati ya hifadhi na wananchi.
Mheshimiwa Naibu Spika, kama nilivyojibu katika swali namba 332 la tarehe 8 Juni, 2016 linalohusu marekebisho ya mipaka ya Hifadhi ya Moyowasi na wananchi, Wizara yangu itaorodhesha maombi haya katika orodha ya maeneo yanayopakana na hifadhi yatakayoshughulikiwa kimkakati na Serikali kwa kushirikisha wadau wote muhimu ikiwa ni pamoja na wananchi, Wizara ya Maliasili na Utalii, Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, TAMISEMI, Maji, Nishati na Madini na Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira kwa nchi nzima.
Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara yangu inaendelea kusisitiza kwamba utekelezaji wa azma ya Serikali ya kujibu kero za wananchi kuhusu changamoto za mahitaji ya ardhi utazingatia uwepo wa sheria, kanuni na taratibu na pia kuweka mbele maslahi ya Taifa.