Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 13 Sitting 3 Natural Resources and Tourism Wizara ya Maliasili na Utalii 44 2023-11-02

Name

Oliver Daniel Semuguruka

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. OLIVER D. SEMUGURUKA aliuliza:-

Je, ni lini Serikali itaona umuhimu wa kukitangaza vya kutosha Kivutio cha Maporomoko ya Maji Rusumo ili kuchangia pato la Taifa?

Name

Dunstan Luka Kitandula

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Mkinga

Answer

NAIBU WAZIRI WA MALIASILI NA UTALII alijibu:-

Mheshimiwa Spika, kwa niaba ya Waziri wa Maliasili na Utalii, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Oliver Daniel Semuguruka, Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Wizara inaendelea kushirikiana na Halmashauri za Wilaya kubaini vivutio mbalimbali vya utalii nchini kwa lengo la kuongeza wigo wa mazao ya utalii, katika kutekeleza hilo mwaka 2021 wataalam wa Wizara kwa kushirikiana na Halmashauri ya Wilaya ya Ngara walibaini vivutio vya utalii na fursa mbalimbali za uwekezaji na shughuli za utalii katika Mkoa wa Kagera.

Mheshimishiwa Spika, miongoni mwa vivutio vilivyobainishwa ni Maporomoko ya Maji ya Mto Rusumo ambayo yanatoa fursa ya uendelezaji wa shughuli za utalii. Hata hivyo, tathmini ya awali iliyofanywa na watalaam wa Wizara imebaini kwamba kiasi kikubwa cha maji ya maporomoko hayo kimechepushwa kwa ajili ya uzalishaji wa umeme na hivyo kupunguza mvuto wa utalii wa maporomoko pekee.

Mheshimishiwa Spika, kwa mujibu wa ushauri wa watalaam, mara baada ya kukamilika kwa mradi wa uzalishaji wa umeme na kukabidhiwa Serikalini, tathmini mpya itafanyika ili kuunganisha utalii wa maporomoko ya maji na utalii wa uzalishaji wa umeme. Endapo tathmini hiyo itaonesha uwezekano wa eneo hilo kutumika kama kivutio cha utalii wa maporomoko ya maji na utalii wa uzalishaji umeme, Serikali itajielekeza kwenye kufanya maboresho ya miundombinu katika maporomoko hayo na kuyatangaza ndani na nje ya nchi kwa lengo la kuvutia watalii kutembelea katika kivutio hicho.

Mheshimiwa Spika, kupitia Bunge lako tukufu niendelee kuwahamasisha Watanzania wenzangu kuwa na utamaduni wa kutembelea vivutio mbalimbali vya utalii. Aidha, nitoe wito kwa Mheshimiwa Mbunge, uongozi wa Mkoa na wadau wengine kwa ujumla kuhamasisha uwekezaji wa huduma ikiwemo huduma za malazi na miundombinu mbalimbali katika vivutio vya utalii vilivyopo katika Mkoa wa Kagera.