Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Primary Question

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 3 Sitting 44 Lands, Housing and Human Settlement Development Wizara ya Ardhi Nyumba na Maendeleo ya Makazi 375 2016-06-16

Name

Hassan Selemani Kaunje

Sex

Male

Party

CCM

Constituent

Lindi Mjini

Primary Question

MHE. HAMIDA M. ABDALLAH (K.n.y. MHE. HASSAN S. KAUNJE) aliuliza:-
Kuna migogoro ya ardhi iliyosababishwa na upimaji na ugawaji wa ardhi kwa ajili ya makazi na ujenzi wa taasisi katika Kata ya Rasbura eneo la Mitwero.
Aidha, watumishi wa Idara ya Ardhi walijigawia ardhi kinyume na taratibu na kuiuza kwa manufaa yao. Pia wananchi wanalalamikia fidia na utwaaji wa maeneo makubwa tofauti na michoro iliyomo kwenye nyaraka zilizothibitishwa na Wizara kwa matumizi ya taasisi za umma au binafsi:-
Je, Serikali ipo tayari kufanya uchunguzi au uhakiki wa zoezi zima la upimaji na ugawaji wa viwanja katika eneo hilo?

Name

Dr. Angeline Sylvester Lubala Mabula

Sex

Female

Party

CCM

Constituent

Ilemela

Answer

NAIBU WAZIRI WA ARDHI, NYUMBA NA MAENDELEO YA MAKAZI alijibu:-
Mheshimiwa Naibu Spika, kwa niaba ya Waziri wa Ardhi, Nyumba na Maendeleo ya Makazi, naomba kujibu swali Na.375 la Mheshimiwa Hassan Seleman Kaunje, Mbunge wa Lindi Mjini, kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Naibu Spika, eneo la Mitwero lililoko katika Kata ya Rasbura ni moja ya maeneo ambayo upimaji wa viwanja kwa ajili ya matumizi mbalimbali katika Manispaa ya Lindi umefanyika. Kwa kawaida, upimaji wa viwanja popote hufanyika kwa kuzingatia Sheria ya Ardhi pamoja na Sheria ya Mipango Miji na kanuni zake ambazo huelekeza upimaji na fidia stahiki kwa eneo husika kabla ya kutwaliwa.
Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba pamoja na kuwepo kwa utaratibu huu wa kisheria wa upimaji na ugawaji viwanja, yapo malalamiko mbalimbali yaliyojitokeza wakati Halmashauri ya Manispaa ya Lindi ikiwa inatekeleza mradi wa upimaji viwanja katika eneo la Mitwero. Miongoni mwa malalamiko hayo ni wananchi kulipwa fidia ndogo, ucheleweshaji wa malipo ya fidia na utaratibu usioridhisha wa ugawaji wa viwanja.
Mheshimiwa Naibu Spika, katika kushughulikia malalamiko ya wananchi wa Mitwero, nilitoa maagizo kwa Mkurugenzi wa Manispaa ya Lindi kwamba washirikiane na Kamishna wa Ardhi Msaidizi Kanda ya Kusini katika kuyashughulikia malalamiko hayo ikiwemo kurejea uthamini wa maeneo na maendelezo ambayo hayakuthaminiwa wakati Halmashauri ikitekeleza mradi huo ili walalamikaji walipwe stahiki zao.
Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu watumishi wa Halmashauri ya Manispaa ya Lindi watakaobainika kukiuka maadili ya Utumishi wa Umma pamoja na ukiukwaji wa miiko ya taaluma zao, kwa kushirikiana na Ofisi ya Rais, (TAMISEMI) tutachukua hatua zinazostahili.
Mheshimiwa Naibu Spika, mwisho, napenda kumhakikishia Mheshimiwa Mbunge kuwa Wizara yangu kwa kushirikiana na Manispaa ya Lindi imeshafanya uhakiki na wote waliokuwa na madai yameanza kushughulikiwa kwa kulipwa fidia zao stahiki.