Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 7 Sitting 22 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2017-05-11

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Primary Question

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kumuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nchi yetu imekuwa na sera nyingi sana, sera ambazo mara nyingi utekelezaji wake ama ni pungufu au hazitekelezwi kabisa. Sera hizi mara zote kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi zimekuwa zikirudiwa rudiwa mara nyingi sana.

Mheshimiwa Naibu Spika, leo swali langu litaenda kwenye Sera ya Maji ya mwaka 1991 ambayo lengo kubwa ilikuwa wananchi wetu waweze kupata maji kwa umbali wa mita 400, utekelezaji wa sera hii mpaka ifikapo mwaka 2002, siyo hivyo tu, Julai 2002 hiyo baada ya ile sera kuwa haijafikiwa, ikafanyiwa mapitio tena, ikatambua kwamba maji ni uhai, maji ni siasa, maji ni uchumi, vilevile ikaingizwa rasimu ya kwamba maji na mazingira.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, mpaka leo hii wananchi wetu wamekuwa na janga kubwa la maji. Ni nini kauli ya Serikali juu ya utekelezaji wa sera hii?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kuchauka, Mbunge wa Liwale kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nikiri kwamba sera hiyo tunayo na huo ndiyo msisitizo wetu na hata bajeti ambazo Waheshimiwa Wabunge huwa mnazipitia kila mwaka zinalenga kufikia hatua hiyo. Nataka niwahakikishie kwamba pamoja na mipango ya Serikali ya usambazaji wa maji, pamoja na kutenga bajeti ambazo tunazo huku ndani, bado tunapata tatizo kubwa nchini la kupatikana kwa vyanzo vya kutosha vya maji vinavyoweza kutosheleza kusambaza maji kwa kiwango ambacho tumejiwekea.

Mheshimiwa Naibu Spika, sera ni malengo na malengo yetu tunataka tuyafikie, tunapata changamoto kwenye utekelezaji kama ambavyo nimeeleza. Sasa hivi nchi imekumbwa na uharibifu mkubwa sana wa mazingira na nimelieleza mara kadhaa. Maeneo haya yamesababisha kukosekana upatikanaji wa maji na miradi mingi ambayo inatakiwa itekelezwe ni ya gharama kubwa kwa sababu inatakiwa tufuate maji kwenye umbali mkubwa ambapo gharama zake ni kubwa, hiyo sasa inakuja kugongana na mahitaji pia ya bajeti. Waheshimiwa Wabunge sasa hivi tuko kwenye Bajeti ya Maji ambayo mnaendelea kujadili na kushauri Serikali na Serikali kwa usikivu tulionao tutaendelea kuwasikiliza na kuyachukua yale yote muhimu.

Mheshimiwa Mwenyekiti, ningependa kutumia nafasi hii kuwasihi Waheshimiwa Wabunge tushirikiane sana katika kuhakikisha mazingira yetu nchini yanalindwa ili tuwe na vyanzo vya kutosha, Serikali imudu kuchimba visima hata vya urefu wa kati au urefu mfupi ili kuweza kumudu kusambaza maji kwa kiwango kikubwa.

Mheshimiwa Naibu Spika, tatizo kubwa ambalo tunalipata sasa ni hilo la kukosekana kwa vyanzo sahihi vya maji. Lakini pia nitumie nafasi hii kuwasihi Watanzania, tuendelee kuvitunza vyanzo vyetu vya maji ili Serikali isitumie gharama kubwa kutafuta mradi ambao maji yake hayatoshi na kama unayapata ni ya muda mfupi kwa sababu huku juu kote kuko kweupe na jua linavyopiga maji yote hukauka.

Kwa hiyo, nataka nikuhakikishie kwamba Ilani yetu inayosema katika kipindi cha miaka mitano tunataka tufikie hatua fulani, tutaitekeleza. Serikali ya Awamu ya Tano sasa tuna mwaka mmoja na tunaomba ridhaa yenu mwaka wa pili wa utekelezaji, mpaka kufikia mwaka 2020 kama miaka mitano ya ahadi zetu, tunatarajia sehemu kubwa ya nchi kwenye vijiji, kata na miji mikubwa tuwe tunapata maji kwa kiwango ambacho tumejiwekea commitment kwenye sera ya kufikia mita 400 kila mmoja aweze kupata maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumemuona Makamu wetu wa Rais, Mama Samia Suluhu akipita kuzindua miradi mingi sana, naomba sasa mtupitishie bajeti yetu ambayo tunaijadili hapa ili tuendelee kutoa huduma za maji. Tunajua tuna changamoto, inaweza kuwa fedha kidogo lakini tutaendelea kuwa na miradi mingi sana ambayo tutaifungua. Juzi tumefungua mradi mkubwa sana Tabora, unaotoa maji Shinyanga, Ziwa Victoria, tunasambaza Tabora na Wilaya zake zote.

Mheshimiwa Naibu Spika, tutaendelea na miradi mikubwa kama hiyo, tutaendelea kuzungumza na marafiki zetu ambao pia tunapata miradi ili tuweze kusambaza miradi hii kwenye vijiji na kwenye umbali ambao tumeuweka kwenye sera yetu. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Zuberi Mohamedi Kuchauka

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Liwale

Question 1

MHE. ZUBERI M. KUCHAUKA: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, ahsante kwa majibu yanayotia matumaini, lakini umeainisha kwamba tatizo kubwa tulilonalo ni tatizo la vyanzo vya maji. Je, Serikali haioni sasa imefikia wakati wa kuvuna maji ambayo maji mengi kwa mfano, wakati wa masika kama sasa hivi, maji mengi yanapotea hakuna namna yoyote ya kuvuna hayo maji ili iwe ni chanzo mbadala cha maji?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, moja kati ya mipango ambayo tunayo ni ya uchimbaji wa mabwawa kwenye maeneo ambayo tunadhani tunaona kwamba kuna utiririshaji wa maji hasa msimu wa mvua.

Pili, tumeendelea kutoa elimu kwa Watanzania kuzitumia mvua na maji ambayo yanatiririka, kuweza kuyaweka pamoja ili yawe akiba yetu ya kuweza kupata maji na kusambaza kwenye vijiji. Mpango huo upo pia hata kwenye bajeti umeona mipango wa uchimbaji mabwawa maeneo mbalimbali.

Mheshimiwa Kuchauka, wewe unatoka Liwale ni jirani yangu na ninapafahamu Liwale, iko miradi mingi sana tu ya kuchimba mabwawa, lakini jambo la kusikitisha ni kwamba juzi nilikuwa nazungumza na Mkurugenzi wako akiripoti kwamba kuna mvua nyingi, mabwawa mengi yameharibiwa, kwa hiyo tuahitaji tena kutenga fedha za kutengeneza mabwawa yako pale, jambo hili nalo tunalifanya karibu maeneo yote ya nchi.

Mheshimiwa Naibu Spika nasihi na ninatoa wito kwa Halmashauri zote za Wilaya nchini kuhakikisha kuwa tunatumia vizuri mifereji iliyopo na mvua ambazo sasa zinaisha mwishoni, pia hata msimu ujao wa mvua kuweza kujenga mazingira ya kukusanya maji yanayotiririka, wenye nyumba za bati na nyumba zote watumie mvua hizi kupata maji na kuyaweka mahali ili tuweze kuyatumia kipindi cha ukame, kwa kufanya hilo tutakuwa tumepunguza ugumu wa upatikanaji wa maji.

Mheshimiwa Naibu Spika, nataka niwaahidi Waheshimiwa Wabunge na Watanzia wote Serikali itaendelea na mipango yake ya kuhakikisha kwamba tunamtua ndoo Mama ili aweze kufuata maji kwa umbali mfupi na hasa ule umbali ambao tumejiwekea kwenye sera wa usiozidi mita 400. Ahsante