Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 4 Sitting 3 Other Sectors Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2016-09-08

Name

Stephen Hillary Ngonyani

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Primary Question

MHE. STEPHEN H. NGONYANI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kuniona.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumeendelea kuwa na mauaji ya mara kwa mara katika nchi yetu hasa askari pamoja na wananchi wa kawaida, hasa katika mikoa ya Mwanza, Tanga, Vikindu, je, Serikali inatoa kauli gani kuhusiana na vitendo hivi vinavyosababisha mauaji makubwa kwa wananchi wasiokuwa na makosa yoyote?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Stephen Ngonyani, Mbunge wa Korogwe kama ifuatavyo:-
Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba hapa karibuni tumepata matukio mengi ya mauaji ya raia, lakini pia hata askari wetu nao wameuawa katika mfululizo wa matukio hayo hayo kwenye maeneo ya Tanga, Mwanza na hivi karibuni pale Vikindu.
Mheshimiwa Spika, natumia nafasi hii kwanza kutoa pole kwa wananchi wote ambao ndugu zao wamepoteza maisha kupitia mauaji hayo yaliyotokea kwenye maeneo haya yote. Lakini pili, ningependa niwahakikishie Watanzania kwamba Serikali imesikitishwa sana na jambo hili ambalo linaonekana kuna Watanzania wachache wasingependa maisha ya wenzao yaendelee na kuamua kukatiza kwa njia ya mauaji ambayo Serikali haijaridhishwa, na Watanzania wengi wamepata uoga katika hili kwamba linaweza kuwa endelevu.
Mheshimiwa Spika, nataka niwatoe wasiwasi huo Watanzania kwamba Serikali iko macho, na imeendelea kuwasaka wale wote waliohusika kwenye mauaji haya, na tutahakikisha tutawakamata wote popote walipo ili tuwatie mikononi na hatimaye mkondo wa kisheria uweze kuchukua nafasi yake.
Mheshimiwa Spika, lakini jambo hili kwa masikitiko ambayo nimeyaeleza napenda tuwahakikishie Watanzania kwamba vyombo vya dola viko macho, na tutaimarisha ulinzi maeneo yote, kutoka ngazi ya vitongoji na maeneo yote ambayo wananchi wanavyokuwa wanaishi na wanahitaji amani ya kutosha. (Makofi)
Mheshimiwa Spika, katika hili niombe wananchi wote washirikiane sana na vyombo vya dola katika kuhakikisha kwamba kwenye maeneo yetu kama kuna jambo ambalo tunalitia mashaka, kama kuna mtu ambaye tunamtilia mashaka tushirikiane na vyombo vya dola kuvipa taarifa ili vyombo vya dola viweze kuchukua tahadhari kabla ya mauaji hayo hajawahi kujitokeza.
Kwa hiyo, kauli ya Serikali katika hili ni kuhakikisha Watanzania kwamba usalama wa nchi hii utaendela kwa kuhakikisha kwamba tunathibiti matukio matukio yote ya hovyo yanayopelekea wananchi kusitisha maisha yao kama ambavyo imetokea kwa askari, lakini pia kwa wananchi wetu ambao wametangulia mbele za haki kwa matukio haya.
Mheshimiwa Spika, kwa hiyo bado nirudie kwamba Serikali itaongeza ulinzi katika nchi yetu kwenye maeneo yote, na ndio hiyo ambayo tulikuwa tunaijadili hapa juzi kuona kwamba tumeimarisha ulinzi zaidi; polisi wako wengi wanaangalia usalama katika nchi hii unaendelea. Kwa hiyo, naomba niwahakikishie kwamba nchi itaendelea kuwa salama na wale wote waliohusika katika matukio haya tutaendelea kuwasaka ili kuhakikisha tunawapata na kuwachukulia hatua. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister