Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 2 sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2016-01-28

Name

Pauline Philipo Gekul

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Babati Mjini

Primary Question

MHE. PAULINE P. GEKUL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nimuulize swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, hivi karibuni Serikali imetoa Waraka katika Halmashauri zetu kuhusu elimu bure na Waraka wenyewe ni wa tarehe 6 Januari, 2016.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, Waraka huu umezua sintofahamu katika sehemu ya chakula cha wanafunzi katika shule zetu. Mfano, Waraka huu unasema kwamba wanafunzi wanaosoma day wazazi walipe chakula, lakini wanafunzi wanaosoma shule za bweni ambao wazazi wao wana uwezo hata wameweza kuwafikisha katika shule hizo, hawatakiwi kulipa hata chakula, Serikali itapeleka chakula.
Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali inasemaje katika hali hii ambayo imezua mtafaruku kwa wazazi kuona kwamba wamebaguliwa wale ambao hawana uwezo na Serikali imewaongezea uwezo wale ambao kidogo wana uwezo?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Pauline Philip Gekul, Mbunge wa Jimbo la Babati Mjini kama ifuatavyo:-
Ni kweli kwamba ipo mikanganyiko imejitokeza sana hasa baada ya kuwa tumeanza kutekeleza mfumo wa elimu bure. Hata hivyo, nataka niwajulishe Watanzania wote maeneo ambayo Serikali imejikita, kuwa ni ya bure.
Moja, kwa upande wa sekondari, tulikuwa na ada ya shilingi 20,000/= kwa mwaka kwa shule za kutwa, eneo hilo sasa hawatalipa. Eneo la sekondari za bweni, wazazi walikuwa wanalipa shilingi 70,000/= kwa mwaka eneo hilo halilipiwi, ni bure. Eneo la tatu, kwa shule za msingi na sekondari mitihani yote ya darasa la nne na kidato cha pili, iliyokuwa inafanywa kwa wanafunzi kuchangia, eneo hilo sasa wanafunzi hawatachangia. Serikali itatenga fedha kwa ajili ya mitihani hiyo ya kidato cha pili na darasa la nne, watafanya bure.
Mheshimiwa Spika, eneo la lingine kwa shule za sekondari za bweni ambazo wanakula chakula tunaendelea na utaratibu wa kuwalipia, kuwagharamia. Sasa mkanganyiko unaojitokeza kwa uelewa wangu, Mheshimiwa Mbunge na Watanzania wote, ni pale ambako zipo shule za kutwa, ambazo kisera shule za kutwa, ni za mtoto anatoka nyumbani anaenda shuleni, anasoma anarudi kula nyumbani. Hizi sasa ndiyo ambazo zimeleta mkanganyiko hasa kwa wazazi ambao walikuwa wamejiwekea mpango wao, wao wenyewe ili kuweza kuwafanya vijana wetu waweze kupata lishe shuleni.
Mheshimiwa Spika, katika eneo hili nikiri kwamba pamoja na mkanganyiko ikiwemo na hili, Wizara sasa inaandaa utaratibu mzuri wa maelezo mazuri ya namna tutakavyotekeleza kwenye eneo hili halafu tutatoa taarifa, kwa sababu ndiyo tumeanza kutekeleza mwezi Januari, hizi changamoto zimeanza kujitokeza, yako maeneo mengine wanaendelea kuchangisha. Kwa hiyo, tunataka tutoe Waraka ambao sasa utaweka wazi kila kitu na Waheshimiwa Wabunge, tutawaletea nakala ili mtusaidie katika kuratibu jambo hili. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister