Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 14 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2024-02-01

Name

Timotheo Paul Mnzava

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Korogwe Vijijini

Primary Question


MHE. TIMOTHEO P. MNZAVA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru; moja kati ya jambo litakalosaidia sana utekelezaji wa Sera hii ya Elimu na kuendeleza maendeleo ya elimu yetu, ni maelekezo na uamuzi wa Serikali wa Elimu Msingi Bila Malipo. Hivi karibuni tumeshuhudia baadhi ya shule kuwa na utitiri mkubwa wa michango kiasi cha kupelekea kuondoa ile dhana ya Elimu Msingi Bila Malipo. Ni nini kauli ya Serikali juu ya jambo hili?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mnzava, Mbunge wa Korogwe, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, msimamo wa Serikali umebaki vilevile kwamba michango holela hairuhusiwi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, ninaposema michango holela, tunajua tuna michango inayokubalika kwenye jamii. Hizi shule zetu za msingi na sekondari ni shule za jamii, ziko kwenye meneo hayo. Tumeunda Kamati ya Shule kwa Shule za Msingi lakini tuna Bodi ya Shule kwa Sekondari. Wajumbe wa Bodi hizi ni wale walioko kwenye maeneo yale kwa lengo la kuwa wanapaswa kusimamia maendeleo ya shule, kushauri mwenendo wa shule na pia kupata changamoto zinazotokana na mwenendo wa kila siku, nao washiriki katika usimamizi wa uendeshaji au uendelezaji wa shule hiyo na taaluma yake kwa ujumla. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa maana hiyo, Kamati ya Shule inajua inawajibika kwenye ile shule kufuatilia maendeleo yake na pia mahitaji yake. Inaweza kutokea kwa mfano, choo cha shilingi milioni mbili kimebomoka. Siyo lazima kusubiri Serikali ije kujenga choo. Jamii inaweza ikaweka mpango mkakati wa kujenga choo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, michango holela na michango inayokubalika, hapa iko ya aina mbili. Michango inayokubalika ni hiyo ya maendeleo; ya choo kimebomoka, Kamati ya Shule inakutana, wanasema kuna choo kimebomoka tunataka kijengwe kwa haraka watoto wetu waanze kukitumia kesho. Badala ya kusubiri kuandika barua, bajeti ipangwe mpaka TAMISEMI, wanaweza kukubaliana kwamba bwana, tuchangie hapa shilingi mia tano, mia tano, mchango ambao unaenda kwenye choo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, michango hii pamoja na maamuzi hayo tumeidhibiti kidogo. Pamoja na maamuzi yenu ninyi Kamati ya Shule na Kijiji kwa ajili ya jambo la maendeleo, bado mwenye idhini ya kuanza kuchangisha ni Mkuu wa Wilaya. Tumeiweka hiyo kuondoa pia watu kukaa pamoja kutengeneza michango ambayo pia haikubaliki. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, msimamo wa Serikali umebaki pale pale kwamba hatuhitaji michango holela. Michango holela ni ile ambayo wakati wote ninapokuwa ziara huwa natoa mifano. Mtu mmoja tu anakurupuka anasema, kesho kila mmoja awe na shilingi mia mbili mia mbili, hazina maelekezo, hazina maelezo. Michango kama hii ndiyo ile holela ambayo haikubaliki.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumeagiza pia kwamba Mamlaka ya Serikali za Mitaa, kusimamia kutokuwepo kwa michango holela inayokwaza wazazi katika kuendesha shughuli au usimamizi wa mtoto kupata taaluma. Hiyo ndiyo maana ya michango holela na michango rasmi ambayo pia nayo tumeidhibiti na msimamo wetu umebaki pale pale kwamba michango holela haikubaliki. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister