Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 13 Sitting 3 Education, Science,Technology and Vocational Training, Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2023-11-02

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwanza nikupongeze sana kwa wasilisho zuri ambalo kwa kweli limekuja wakati muafaka katika kusimamia tasnia nzima ya Sekta ya Elimu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri Mkuu ametaja wadau muhimu katika ushirika huu, lakini hadi hivi ninavyozungumza hakuna chombo maalum kinachoisimamia Sekta Binafsi ya Elimu, hivyo kuwa na sauti ya pamoja pale inapotimiza majukumu yake ya kutoa elimu. Tutakumbuka kwamba shule za Serikali zipo chini ya TAMISEMI na zinapokea miongozo yote kutoka TAMISEMI, lakini Shule za Sekta Binafsi na Vyuo vya Sekta Binafsi na vya Kidini hawa hawana chombo ambacho kinawaunganisha kwa pamoja. Sasa nataka tu kufahamu kwamba ni upi mkakati wa Serikali kuhakikisha kwamba sekta hii nayo inakuwa na chombo ambacho inaweza ikakisimamia? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shangazi, Mbunge wa Mlalo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Sera yetu ya Elimu imetoa nafasi kutekelezwa kupitia Sekta ya Umma ambayo ni ya Serikali, lakini pia Sekta Binafsi na ndio kwa sababu leo Taasisi za Kidini zimeanzisha shule za msingi, sekondari hata vyuo, mtu mmoja mmoja ameweza kuanzisha shule ya msingi, sekondari na vyuo na wote hawa wako kwenye utekelezaji wa Sera ya Elimu kwa pamoja.

Mheshimiwa Spika, sasa suala la chombo kwa Sera ya Elimu inavyotekeleza, Wizara ya Elimu ndio msimamizi wa sera na yeye ndio anayeshughulikia na udhibiti ubora wa elimu hapa nchini wakati usimamizi wa shughuli za kila siku kwa shule za msingi na sekondari inafanywa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Kwa hiyo matatizo yote na shughuli zote za Elimu ya msingi na sekondari zinasimamiwa na Mamlaka ya Serikali za Mitaa. Wanapofanya hivi pamoja na Sekta ya Elimu ambayo inatambua Sekta Binafsi ambayo inafanya kazi ya kutoa elimu nchini inaingia kwenye utaratibu huo huo. Watatekeleza sera ya nchi, lakini pia watakaguliwa kwa mifumo iliyopo nchini, lakini utendaji wa kila siku utaendelea kufuatiliwa na Mamlaka za Serikali za Mitaa kwa sababu shule zote za msingi na sekondari za sekta binafsi ziko kwenye Halmashauri husika na msimamizi ni Mkurugenzi wa Halmashauri.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Mkurugenzi na Idara yake ya Elimu wataendelea kufuatilia mwenendo wa utoaji elimu nchini kupitia Idara ya Elimu watakwenda kwenye shule za sekta ya umma za Serikali watakwenda na kwenye shule za sekta binafsi ili kuona kuwa mwenendo wa utoaji wa elimu unakuwa mmoja na ndio kwa sababu wanafuata ratiba ya Serikali hata Sekta Binafsi, wanafanya mitihani ya Serikali chini ya Baraza la Mitihani pia ni pamoja na Sekta Binafsi.

Mheshimiwa Spika, hii sasa inaweza wakajua sasa sekta binafsi kwamba wanawajibika kwa Mkurugenzi wa Halmashauri husika. Suala la kuwa na chombo maalum cha sekta binafsi kwa kuwa tumesema shule za msingi, sekondari zote zinawajibika kwa Mamlaka ya Serikali za Mitaa hicho ndio Chombo chao ambacho inatakiwa kuripoti matatizo yao, mafanikio yao na kama kuna changamoto nyingine zozote zile wataripoti kwa Wakurugenzi wa Halmashauri. Shule hizo za Binafsi zinakaguliwa na Mkurugenzi wa Halmashauri kupitia chombo cha Wizara ya Elimu cha Udhibiti Ubora tulichokipeleka kwenye Halmashauri zetu.

Mheshimiwa Spika, hii inafanya uendeshaji wa elimu kwa ujumla wake kuwa hauna matatizo na tumewaruhusu pia Sekta Binafsi kuanzisha umoja wao, watajadili mafanikio yao, watajadili mapungufu yao na watapeleka kwenye ngazi husika za Serikali pale ambapo wanaona kuna umuhimu wa kushirikiana na Serikali. Kwenye maboresho ya Sera hii ambayo leo tunaisoma hapa na kwamba tumeshakamilisha, tunasubiri kuzindua. Sekta Binafsi wameshirikishwa kikamilifu na waliitwa wote hapa Dodoma wamezungumza kwa pamoja, wamekubaliana, wamerudi wakiwa wameridhika na naamini wako Waheshimiwa Wabunge hapa nao wamejikita kwenye utoaji wa elimu na wao pia wanajua kwamba walishirikishwa na Serikali.

Mheshimiwa Spika, nataka niwahakikishie wadau wote wa utoaji elimu kwa Umma kwamba Sera yetu inalenga kufanya maboresho makubwa. Dhamira ya Rais wetu katika kuanzisha mchakato huu, lakini michango ya Waheshimiwa Wabunge imepelekea kukamilika kwa Sera hii na Wadau wa Sekta Binafsi ambao wamechangia, yote inapelekea kwenda kuimarisha Sera hii na iweze kutekelezeka. Kwa hiyo wajibu wetu sasa ni kuipokea na kuanza maandalizi ya kutekeleza Sera hii. Hayo ndio majibu ya msingi. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister