Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 41 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2022-06-09

Name

Esther Nicholus Matiko

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ESTHER N. MATIKO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru. Tunatambua kwamba vijana ambao wanakuwa wamemaliza kidato cha sita na wengine wanawajibika kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa ili kuweza kujifunza uzalendo, umoja wa kitaifa, stadi za kazi, stadi za maisha lakini cha zaidi utayari wa kulitumikia Taifa.

Mheshimiwa Spika, tarehe 31 Juni kuna wito umetolewa na JKT kuwaita vijana waliomaliza kidato cha sita kujiunga na JKT, lakini umeambatana na orodha ya mahitaji mengi sana ambayo wanatakiwa waende nayo. Tunatambua kwamba ni muhimu sana vijana hawa kujiunga na JKT na hapo zamani ilikuwa ikitolewa na vijana wanaenda kuripoti kambini vifaa vyote vinatolewa kule kambini.

Sasa nilitaka tu kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu, ni kwa nini sasa Serikali isione kwamba ni muhimu kuwajengea uwezo hawa vijana ili tuweze kuwaacha wale vijana ambao wanatoka kwenye kaya maskini iweze kutoa vifaa hivi kama ilivyokuwa ikitoa hapo zamani? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Esther Matiko, Mbunge kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali imeendelea kutoa wito kwa vijana wetu kujiunga na Jeshi la Kujenga Taifa kwa malengo ambayo Mbunge ameeleza kujenga uzalendo, kumjengea uwezo wa kujiamini ili pia kushiriki katika ulinzi wa Taifa lake na tunapofanya hili tunawapeleka kwenye makambi yetu.

Mheshimiwa Spika, Mbunge akitaka kujua kwa nini sasa tunapowaita tunaambatisha na orodha ndefu ya vifaa vinavyotakiwa jeshini. Serikali tumejipanga na tumeandaa utaratibu wa kuwahudumia hawa na vifaa vilivyo muhimu vya shughuli ile ya kijeshi kama bukta, viatu pamoja na sare yenyewe zile ambazo zinatumika kwenye shughuli yenyewe ya mazoezi na uimara na ukakamavu.

Mheshimiwa Spika, pia Serikali tumetoa nafasi ya watu kuja na vifaa ambavyo tunaweza kuvitumia viko vifaa ambavyo tumewaambia kwamba ukija kwenye eneo hili unatakiwa kuja na moja, mbili, tatu, nne ili uweze kuishi kwenye maeneo haya. Lakini vile vifaa muhimu vyote vinapatikana kwenye eneo lile la ulinzi.

Kwa hiyo, tofauti ya vifaa vile vinavyoagizwa na vile ambavyo vipo ni kwamba vilivyopo ni muhimu kwa mazoezi lakini kuna vile ambavyo vina-support wakati wote kijana huyu akiwa jeshini navyo pia anaweza kujitafutia ndio tunaorodheshea kwamba wanapokuja Makutupora uje na hiki na hiki kulingana na mazingira hayo.

Mheshimiwa Spika, hata sisi tulipokuwa jeshi wakati ule tuliagizwa na tulienda navyo na tulipata vifaa vingine jeshini. Kwa hiyo, ni utaratibu wa kawaida kuagiza vifaa muhimu vya jeshi ambavyo vinapatikana pale pale jeshini, lakini vile ambavyo ni muhimu kwa kuishi kwenye eneo lile basi tunakuagiza uweze kuja navyo ili uweze kuvitumia.

Mheshimiwa Spika, nashukuru kwa kutoa majibu hayo. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister