Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 41 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2022-06-09

Name

Priscus Jacob Tarimo

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Moshi Mjini

Primary Question

MHE. PRISCUS J. TARIMO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa nafasi hii ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu sera ya Serikali ya kuwa na shule ya sekondari kila kata imefanyika vizuri na imekuwa na mafanikio, na nia yake ni kuhakikisha watoto wote ambao wanastahili kwenda sekondari wanakwenda, lakini kupunguza umbali ambao Watoto/wanafunzi walikuwa wanatembea na wakawa wanapata tabu kidogo, lakini zaidi kupunguza pia gharama ya nauli kwa wazazi ambao walikuwa na watoto wale wa sekondari. Sasa mafanikio hayo yamepelekea kwamba watoto wale wanaofaulu form four sasa wanapangiwa shule mbalimbali.

Mheshimiwa Spika, sasa kumekuwa na wimbi kubwa la kupangiwa shule za mbali mtoto anatoka Mtwara kwa mfano anapangiwa Kagera, anatoka Kilimanjaro anapangiwa Kigoma, sasa ile gharama ya nauli ile imekuwa kidogo inakuwa nzito kwa wazazi, lakini pia usalama wa wale watoto. Najua zamani kulikuwa kuna utaratibu wa kuwasafirisha kwa treni kabla ya kipindi ambacho nimesoma mimi.

Sasa Mheshimiwa Waziri Mkuu, swali langu ni nini mkakati wa Serikali, aidha kwa kuwapangia shule za karibu au kutafuta namna nzuri zaidi ya kuwasafirisha wanafunzi hawa? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tarimo, Mbunge wa Manispaa ya Moshi, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, Serikali ilianza mkakati wa ujenzi wa shule za sekondari kila kata nchini kuanzia mwaka 2006 kwa lengo la kuwezesha watoto wanaotoka kwenye kata hiyo wasome eneo lililo karibu ili kupunguza gharama pia usumbufu. Zoezi hili limeendelea vizuri na leo hii angalau kila Wilaya au Halmashauri tumefikia ujenzi wa zaidi ya asilimia 95 wa shule za kata kwenye maeneo yake na kazi hiyo inaendelea kwa malengo yale yale ya kupunguza gharama za wazazi kuwasomesha Watoto, lakini hao watoto wenyewe kuwapunguzia usumbufu wa kutembea umbali mrefu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge anataka kujua Serikali ina mkakati gani wa mpango wetu wa kuwasomesha watoto shule za mbali.

Sasa kwenye sekondari huku tuna kidato cha kwanza mpaka cha nne, lakini kuna kidato cha tano mpaka cha sita. Wanaosoma mbali ambao tunaweza kuwatoa Dodoma kuwapeleka Kagera, Lindi na maeneo mengine ni wa kidato cha tano na sita. Sisi tuliona Serikali kwamba ni muhimu pia Watanzania hawa wakatambua pia jiografia ya nchi yao, lakini pia tukaimarisha uzalendo, pia waweze kujua jiografia ya maeneo mengine na waweze kuingiliana na makabila mengine. Kwa sababu Tanzania ya leo hatuna suala la udini, ukabila wala rangi kwa sababu Watanzania tunaingiliana tulitaka tulidumishe hilo, na kwenye elimu ya sekondari tunalifanya sana kwenye kidato cha tano na sita. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, sasa suala la usumbufu kwa kuwa Serikali imesema kuanzia kidato cha kwanza mpaka cha nne wanasoma bure, tunaamini mzazi tunampa nafasi ya kujiandaa kwa mtoto wake kwenda kidato cha tano popote atakapopangiwa nchini ili kumuimarisha vizuri kitaaluma na aweze kuendelea vizuri kwa kufahamu jiografia ya nchi yake na namna nyingine yoyote ambayo tunaweza kujifunza kwa utaratibu huo. Na huko atakakokwenda tunajitahidi pia kupunguza gharama zake, shule yoyote ya kidato cha tano na cha sita ni zile shule ambazo zinagharamiwa kwa kiasi kikubwa na Serikali halafu kiasi kidogo wananchi wanachangia. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tumeendelea kumpungia mzigo wa kuchangia elimu kwa mtoto wa kidato cha tano na cha sita. Kwenye sekondari kidato cha tano wanalipa shilingi 70,000 lakini gharama zake ni kubwa na Serikali inapeleka chakula na huduma nyingine. Kwa hiyo, haya yote yanalenga kukuza ule utamaduni ambao tuliujenga kutoka Serikali ya Awamu ya Kwanza ambayo ilikuwa imeimarisha sana watanzania kuondoa watu kukaa eneo moja na kujigawa kuwa ndio wako sehemu moja ili kila mmoja aweze kufahamu maeneo mengine. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunapokea ushauri, lakini tunaendelea kuangalia namna bora ya kuwapunguzia mzigo wazazi kwenye upatikanaji wa elimu na tutakuwa tunafanya maboresho kadri tunavyoendelea, kama ambavyo Wizara ya Elimu sasa inaendesha mjadala wa mtaala haya yote yatakuwa yanaingia kwenye mtaala na kuona namna bora ya kuendesha elimu na namna nzuri ya kuwapunguzia gharama wazazi, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister