Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 41 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2022-06-09

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa fursa hii ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu kumekuwa na ongezeko la wanyama wakali hasa tembo ambao wamekuwa wakivamia maeneo ambayo yako mbezoni mwa Hifadhi za Taifa, lakini pia na mapori tengefu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu wanyama hawa kwa nyakati tofauti wamekuwa wakiathiri shughuli za kijamii, kiuchumi lakini pia wakati mwingine kusababisha hata vifo.

Mheshimiwa Waziri Mkuu suala la ulinzi wa mali na usalama wa raia ni jukumu la Serikali. Je, ni kwa kiasi gani Serikali itawahakikishia wananchi hawa walioko pembezoni mwa hifadhi hizi usalama wao ili wasiendelee kupata athari zinazosababishwa na wanyama hao? Ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, nimeona nilijibu hili swali la Mheshimiwa Shangazi, Mbunge kutoka Lushoto kwa sababu pia nimefanya ziara maeneo mengi na nimekuwa nikilalamikiwa na Watanzania wanaoishi kwenye maeneo yaliyo kando kando na maeneo ya hifadhi kwa maslahi ya Taifa.

Nikubaliane naye kwamba Serikali inao wajibu wa kulinda mali lakini pia usalama wa raia ndani ya nchi. Pia nikiri kwamba tuna ongezeko kubwa la wanyamapori hasa baada ya kuwa tumeimarisha ulinzi kwa maana ya uvamizi, uwindaji haramu, kwa hiyo wanyama wengi wameongezeka na tembo nao pia wameongezeka sana.

Mheshimiwa Spika, huu mjadala huu nimeusikia sana pia hapa Waheshimiwa Wabunge wakichangia wakati wa bajeti ya Maliasili na Mheshimiwa Waziri amejitahidi kueleza namna Serikali inavyojitahidi kudhibiti wanyamapori wanaoingia kwenye maeneo ya makazi ya watu, lakini mashamba na kusababisha pia upotevu, uharibifu wa mali pia hata vifo kwa baadhi ya Watanzania ambao wako karibu sana na maeneo haya ya hifadhi.

Mheshimiwa Spika, ziko jitihada za Serikali zinafanyika sasa za kuhakikisha kwamba tunapunguza au kuondoa kabisa madhara haya kwa yale maeneo yaliyo pembezoni ikiwemo kwenye Jimbo la Mlalo anakotoka Mheshimiwa Shangazi ambalo linakaribiana sana na Mbuga ya Mkomazi.

Mheshimiwa Spika, na ziko Wilaya kadhaa, nimeenda Liwale, Mkoani Lindi, nimefanya ziara Wilayani Kilwa, Mkoani Lindi na hata Lindi Vijijini pia. Nimefanya ziara Mkoani Ruvuma maeneo ya Tunduru Jimboni kwa Mheshimwia Mpakate. Nimefanya ziara pia Meatu, Bariadi maeneo ambayo yamekaribiana sana na Mbuga wa Serengeti pia hata Wilaya ya Serengeti kote huko nimepita na moja kati ya vilio vya Watanzania ni ongezeko la Tembo ambao pia wanakuja hapa. Na kwenye mjadala hapa nilimsikia hata Mheshimiwa Mulugo akirejea misahafu na biblia juu ya jambo hili. (Makofi)

Sasa jitihada ambazo tumezifanya ni kwanza tumeongeza idadi ya askari wa wanyamapori na askari hawa tunawapeleka kwenye maeneo yote yaliyo karibu na makazi ya watu kwenye mbuga hizi ambazo ziko karibu na watu.

Mheshimiwa Spika, lakini pia tumeimarisha na tunaendelea kujenga amary ya hivyo vituo ambavyo vinatunza silaha ambazo zitasaidia pia angalau kuwaondoa hawa tembo warudi kwenye maeneo yao. Na sasa hivi Wizara inaendelea kuratibu ujenzi wa vituo vile 32 kando kando ya maeneo yote haya. Hata nilipokuwa Mkoani Lindi, eneo la Rondo zamani ilikuwa ni Kituo cha Maliasili ambao walikuwa wanasaidia sana kupunguza idadi ya wanyama hatari wanaoingia kwenye makazi ya watu kwa Wilaya za Lindi Vijijini, lakini pia Kilwa maeneo ya Kilanjelanje na maeneo mengine. Kwa hiyo tunarudisha vile vituo uhai wake ili tupeleke hawa askari ambao tunawapeleka kwenye maeneo haya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, wanyama tembo pamoja na ongezeko lake Serikali haikusudii kuvuna, lakini kusudio hasa na ndio kazi kubwa tuliyonayo ni kuzuia wanyamapori kuingia kwenye makazi. Tembo yuko kwenye kundi la top five ya wanyama ambao wenyewe kazi yetu ni kuhifadhi kama sehemu ya nyara za Taifa. Tembo wenyewe, tuna simba, tuna twiga, chui na faru hawa wako kwenye top five ambao Serikali kwa namna yoyote ile itaendelea kuwahifadhi waendelee kuwa ni tunu ya Taifa letu. (Makofi)

Kwa hiyo, niwahakikishie wananchi wote wanaoishi kwenye maeneo ya pembezoni mwa mbuga ambao wameendelea kupata tatizo la tembo kwamba mkakati wa Serikali wa kuongeza askari wengi watakaokaa kwenye maeneo hayo na wakafanya kazi hiyo na tumewakabidhi TAWA wasimamie kwa kina wahakikishe kwamba madhara haya hayajitokezi tena.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo tutaendelea kufanya tathmini kadri tunavyoendelea ili kupunguza athari hiyo na Mheshimiwa Shangazi eneo lile mimi nimefanya ziara Wilayani Same kwa Mheshimiwa Kilango, lakini pia nilikuja mpaka mpakani mwa vijiji vyako nimeona hiyo na nimepata malalamiko hayo. Kwa hiyo, tutaendelea kudhibiti maeneo yale ya vijiji vyako vile ambavyo tembo wanaingia kwako kutoka Mkomanzi ili wananchi waweze kuishi kwa amani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niliona nilijibu hili nifafanue niwahakikishie Watanzania kwamba Serikali inaimarisha mifumo ya kuzuia madhara haya kwa kuhakikisha tunaongeza askari wanaoweza kusaidia kuwazuia tembo wasiingie kwenye makazi ya watu. Tathmini itatuonesha zaidi nini tufanye baada ya zoezi la awali tunalotekeleza sasa, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister