Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 12 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2023-09-07

Name

Joseph Anania Tadayo

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mwanga

Primary Question

MHE. JOSEPH A. TADAYO: Mheshimiwa Spika, nashukuru kupata nafasi hii ya kuuliza swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nchi yetu kupitia Bunge hili ilitunga sheria nyingi nzuri za kulinda uhifadhi hapa nchini na hasa kuzuia uwindaji haramu kwa ajili ya kukuza utalii, kulinda ikolojia na pia kuongeza Pato la Taifa kupitia mapato yanayotokana na utalii. Hivi karibuni Mheshimiwa Waziri Mkuu, wanyamapori hawa ambao tumewahifadhi kwa mujibu wa sheria zetu na pia kwa kuheshimu mikataba ya Kimataifa katika eneo hili wamegeuka kuwa janga kwa kuharibu mali za watu, kuvuruga miundombinu na hata kusababisha watu wengi kupoteza maisha.

Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba tunapitia upya sheria hizi ambazo tuliziweka kwa ajili ya kulinda uhifadhi ili pia ziwalinde wananchi wetu na hata ikibidi kujitoa kwenye baadhi ya mikataba ya Kimataifa ambayo inatushurutisha kuweka sheria za namna hii ambazo zinawadhuru wananchi wetu na mali zao? Ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tadayo, Mbunge wa Mwanga kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kupitia vikao vyetu vya Bunge hapa na baadhi ya Waheshimiwa Wabunge wamekuwa wakieleza usumbufu ambao wananchi kwenye maeneo yetu wanaupata kwa wanyama waliohifadhiwa kwenye maeneo mbalimbali kwenye misitu yetu kuhamia kwenye makazi ya watu na kusababisha uharibifu wa mali, lakini pia hata maisha ya watu, na tumepata taarifa hizi mara nyingi kwenye miji iliyoko kando kando na hifadhi zetu.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba tunazo sheria zinazosimamia utekelezaji huu wa kuhakikisha kwamba wanyama wanabaki porini na wananchi wanaendesha maisha yao kwenye maeneo yao rasmi. Pia kumekuwa na wimbi kubwa la ongezeko kubwa la wanyama kwenye misitu yetu na hii ilitokana na jitihada tulizozifanya kupitia sheria zetu hizo hizo za kulinda uwindaji haramu, hili ndiyo limepelekea kuwa na idadi kubwa ya Wanyama.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo, Wizara ya Maliasili imekuwa ikifanya taratibu kadhaa kukutana na vikao na Wizara ambata zinazohusika kwenye uhifadhi wa mazingira yetu, wa misitu yetu, wanyama wetu na kuona kuwa wanyama wanabaki huko, jitihada kadhaa ambazo zimechukuliwa ni pamoja na kuongeza idadi ya Maaskari ambao pia wameweka vituo kando kando ya maeneo haya ili kuzuia wanyama kuingia, lakini pia tumeona jitihada za kutumia hata ndege kufukuza wanyama kuingiza porini.

Mheshimiwa Spika, tunajua ziko sheria zinalinda haya na Mheshimiwa Mbunge ametaka tubadilishe sheria, lakini muhimu sasa ni Wizara kuhakikisha kuwa maeneo yote yaliyohifadhiwa kwa ajili ya kuweka wanyama yanaendelea kusimamiwa na sheria zake, lakini na taratibu hizo ambazo wamezipanga kwa ajili ya kudhibiti wanyama hawa kuingia kwenye makazi. Hii ni pamoja na kulinda ile buffer ambayo tuliitenga kilometa tano kutoka makazi kuingia kwenye msitu na baadaye tukaruhusu wananchi wafanye shughuli zao za uzalishaji mali, shughuli za maendeleo kwenye hifadhi ile ya kilometa tano, lakini sasa inaonekana pia wanyama wanavuka hifadhi hiyo na kuingia kwenye makazi ya watu.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa ziko jitihada zimechukuliwa na Wizara ya Maliasili na Utalii na wameunda timu ya kufanya ukaguzi wa maeneo haya na kubaini tatizo exactly ni nini hasa kinapelekea wanyama kutoka kule kuingia huku, baada ya kamati ile kukamilisha kazi yao tutapata majibu. Kwa hiyo, niwaahidi kwamba hili ilimradi Wizara imeshaanza kuunda timu ya kwenda kukagua na kugundua tatizo ni nini, baada ya kubaini tatizo, kama tatizo hilo pia litagusa kwenye sheria basi Wizara itatuongoza katika kuleta sheria hapa tufanye mabadiliko ili tuweze kuhifadhi, lakini pia tuhakikishe kwamba wananchi wanaendesha shughuli zao na maisha yao yanaendelea kuimarishwa na kulindwa kama ambavyo tuliweka sheria hizi awali na hatukuwa na tatizo hili hapo mwanzo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo nilitaka nikuhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba kwa ushauri wake kwa Serikali sisi tunauchukua, lakini kwa kuwa timu ilishaanza kazi, tuipe muda timu yetu ikamilishe kazi, halafu ije na mkakati ambao imeuweka na tutaona mkakati huo na jinsi ambavyo utaweza kulinda maisha ya watu, utaweza kulinda pia na hawa wanyamapori wakiwa kwenye maeneo yao. Hii ndiyo njia sahihi ambayo itatusaidia katika kuzuia madhara yaliyojitokeza kwenye makazi ya watu hasa yale makazi yaliyopo karibu na sehemu za hifadhi. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister