Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 21 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2022-05-12

Name

George Ranwell Mwenisongole

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mbozi

Primary Question

MHE. GEORGE R. MWENISONGOLE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kumuuliza swali Waziri Mkuu. Maji ni nyenzo muhimu sana katika Maisha ya binadamu na hata katika mahitaji makuu matatu ya binadamu maji ni sehemu mojawapo. Na katika Ilani yetu ya Chama cha Mapinduzi inasema kwamba kufika mwaka 2025 lazima maji yawe yamefika kwa asilimia 95 mijini na asilimia 85 vijijini.

Mheshimiwa Spika, kwa sasa hatukaribii kufikia hayo ingawa Serikali imepeleka fedha nyingi sana vijijini lakini ukiangalia maji yanafika kwenye vituo kuna umbali mkubwa sana kati ya kituo kimoja na kituo kingine. Sasa Serikali kwa nini isishushe bei za kuunganisha maji vijijini kwa wananchi wote nchi nzima iwe kama umeme wa REA ili wananchi maskini wale wafaidike na huduma hii ya maji ambayo wanatembea umbali mrefu nchi nzima kuangalia hivyo? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kuujibu swali la Mheshimiwa Mwenisongole Mbunge wa Mbozi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, sera yetu ya maji nchini iko wazi kwamba matumizi ya maji yatakuwa yanafika mpaka vijijini tena kwa wingi na gharama nafuu. Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua gharama za kuvuta maji kwenye maeneo yetu. Sera yetu inaeleza kwamba wananchi watachangia kwakulipia miundombinu ya kuvuta maji kwenda mahali alipo ikiwa na umbali usiozidi mita 60 ni umbali mfupi ambao gharama yake si kubwa. Lakini pale ambapo umbali ni zaidi ya mita 60 gharama hizo zitaingiwa na Serikali. Na ndio kwa sababu Serikali sasa inatoa fedha nyingi kutoka mahali maji yanatoka kwenda kwenye eneo la makazi ya wananchi. Pale ambako mwananchi anahitaji kupeleka maji kwenye nyumba yake basi zile gharama za kutoka kwenye nyumba yake mpaka pale kwenye chanzo kama iko chini ya mita 60 ataendelea kugharamia yeye mwenyewe.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo Waheshimiwa Wabunge na Watanzania mnajua kwamba Mheshimiwa Rais Mama Samia Suluhu Hassan alipokuwa Makamu wa Rais Serikali ya Awamu ya Tano moja kati ya majukumu ambayo viongozi wetu wakuu, Rais na Makamu wa Rais waligawana, Mheshimiwa Makamu wa Rais ndio alipewa jukumu la kusimamia usambazaji wa maji nchini. Na akauanzishia kampeni ya kumtua ndoo mama kichwani na aliweza kusimamia kupunguza gharama za maji katika upatikanaji wa gharama za maji kwa wananchi na ndio kazi ambayo sasa inafanyika kwamba kiwango unacholipia kwenye maji ni kuchangia tu gharama ambazo kamati ya maji iliyoundwa na wananchi kwenye kijiji husika ndizo zinazotumika pindi miundombinu iliyowekwa inapoharibika ili wananchi wenyewe waweze kukarabati miundombinu hiyo muweze kupata huduma ya maji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tumetumia utaratibu huo ambao ni rahisi kwa kuchangia maji kwa kiwango kidogo pia kuvuta maji kupeleka nyumbani kwako kwa umbali usiozidi mita 60 utaugharamia mwenyewe lakini ikiwa zaidi ya mita 60 Serikali inawajibika kuleta maji mpaka mahali ulipo. Kwa utaratibu huu sasa tunaanza kuona huduma za maji zinasambaa maeneo yote na malengo yetu kila Kijiji kipate huduma za maji kama sio kwa mtandao wa bomba unaofata makazi ya watu basi tutajenga vilura kwenye maeneo ambayo wananchi waweze kupafikia kwa ukaribu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, tunaendelea kuhakiki bei zetu na kwa kuwa Wizara ya Maji inaanza leo kuwasilisha bajeti yake tutapata maelezo mazuri zaidi kwenye eneo hili na Waheshimiwa wabunge mtapata fursa ya kuchangia na Serikali tunaendelea kupokea maoni yenu, ushauri wenu namna mtakavyoboresha utoaji wa huduma za maji nchini, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister