Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 7 Sitting 21 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2022-05-12

Name

Mwantumu Mzamili Zodo

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. MWANTUM M. ZODO: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa ya kuuliza swali kwa Waziri Mkuu. Mheshimiwa Waziri Mkuu kumekuwa na matukio ya unyanyasaji wa kijinsia, ukatili na hata wakati mwingine mauaji ya wanawake na watoto yanayoendelea nchini. Je, ni upi mkakati wa Serikali wa kuhakikisha wanakabiliana na changamoto hii? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zodo Mbunge wa Mkoa wa Tanga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, yako matukio yameripotiwa kwenye vituo vyetu vya usalama ya unyanyasaji na ukatili wa Watoto na wanawake. Siwezi kusema kwamba yanaendelea lakini tunajitahidi kudhibiti na njia ya kuendelea kudhibiti matatizo haya Serikali imeimarisha utoaji elimu wa wale wote wanaofikwa na madhira haya kwa vyombo vya sheria. Hata hivyo, tumewakaribishia huduma hiyo kwa kufungua vituo vya kwenda kupeleka malalamiko kila palipo kituo cha polisi ili iwe rahisi kwa wananchi kwenda kuripoti kwenye maeneo hayo. Kwa lugha nyingine tunasema tumefungua madawati.

Mheshimiwa Spika, pia tumeanzisha madawati hayo kwenye taasisi za elimu, shule za msingi, shule za sekondari vyuo vya kati na vyuo vikuu na tunao waalimu maalum wanashughulikia malalamiko haya ya unyanyasaji wa kijinsia na ukatili kwa Watoto na wanawake pindi yanapotokea. Kwa hiyo, eneo hilo pia nalo tunapata msaada huo ili kukabiliana na tatizo hili, huku tukiwa tunaendelea na elimu kwa jamii yetu pale ambapo jambo hili linajitokeza basi jamii ituambie ni nani huyo anasababisha jambo hili na hatua kali zinaendelea kuchukuliwa.

Mheshimiwa Spika, nataka nitumie nafasi hii kupitia swali hili la Mheshimiwa Zodo kutoa wito kwa jamii yetu pale ambako tatizo hili la ukatili wa watoto na wanawake linapojitokeza. Hatua kali zichukuliwe kwa kuwapeleka kwenye vyombo vya sheria ili kuweza kudhibiti hali hii. Hata hivyo kwa kuwa nimeeleza kwamba tunaendelea kutoa elimu kwa jamii basi ni muhimu sana pia jamii zetu zikaona umuhimu wa kukaa na watoto na wakawake ambao ndio binadamu wenzetu kuwa tunawatendea haki katika kila jambo ambalo tunatenda nao ili na wao waweze kuweka mipango yao ya maendeleo binafsi na jamii zao. Hili linaweza likasaidia sana kuifanya jamii yetu ya watanzania kuishi kama ndugu, kuishi wamoja lakini kwa Watoto kuwalea na hatimaye waje kuchukua fursa ya kuleta maendeleo kwenye nchi yetu.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali inaendelea na utaratibu huo wa kufatilia madawati haya kuona matukio yanayojitokeza ili tuweze kupunguza kwa kiasi kikubwa ikiwezekana tukomeshe kabisa, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister