Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 10 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2023-02-09

Name

Nusrat Shaaban Hanje

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi niweze kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, malengo ya kuanzishwa kwa Mfuko wa Maendeleo ya Vijana mwaka 1993 ilikuwa ni kuhakikisha inawapatia mtaji vijana kwa mikopo ya masharti nafuu ili waweze kujikwamua kiuchumi, lakini kwa muda sasa mfuko huu umekuwa ukitengewa fedha, lakini vijana wanakosa hizo fedha kwa kiasi kwa sababu ya kukosa vigezo, lakini pia tunafahamu zipo halmashauri ambazo zinakosa asilimia 10 zile ambazo ni four, four, two; nne za vijana, nne za wanawake na mbili za walemavu, kwa sababu hazina mapato ya kutosha.

Ni kwa nini sasa Serikali isitumie Mfuko wa Maeneleo ya Vijana kama equalization fund kuziwezesha zile halmashauri amabzo zina mapato machache, mapato kidogo ili na zenyewe ziweze kutoa zile asilimia nne za halmashauri ili vijana waweze kupata mitaji kama ambavyo yalikuwa malengo ya kuanzishwa Mfuko wa Maendeleo Vijana? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hanje, Mbunge wa Singida kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kama nilivyotoa majibu ya swali la awali linalohusu vijana kwamba Ofisi ya Waziri Mkuu inaendelea kuwawezesha vijana nchini kwa kuwatengea fedha kupitia mfuko, lakini pia kwa kutengeneza vigezo ambavyo vinaweza vikakidhi kwa ajili ya vijana hawa waweze kunufaika na mfuko wao.

Mheshimiwa Spika, eneo hili la kutunisha mfuko nimeeleza kwamba Serikali inajitahidi kila mwaka kutenga fedha kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu. Tulitenga bilioni moja, tukaongeza milioni 800 na bado tutaenedelea kutenga, lakini bado hazitoshi na nimeeleza awali. Kwa kutotosha fedha hizi bado tunaendelea kuhusisha na Wizara nyingine zenye programu za vijana ikiwemo na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo imetenga mfuko na fedha kupitia mapato ya ndani asilimia 10; asilimia nne ni za vijana, lengo ni kutunisha ule mfuko.

Mheshimiwa Spika, sasa na tumefungua milango kwa taasisi binafsi ambazo na zenyewe zinashughulikia vijana na Serikali yetu tuna marafiki wengi ambao pia wanaona jitihada zetu za kuwawezesha vijana, nazo pia zinachangia na ndio kwa sababu tulianzisha mfuko ili kurahisisha pia michango yao kuingia pale, jukumu letu Serkali ni kuusimamia mfuko uweze kuleta manufaa.

Mhehimiwa Spika, lakini la pili hivyo vigezo ambao vijana wengi wanakosa vigezo, tunaposema kukosa vigezo ni pale ambako kijana anakuwa hana anwani maalum, kijana huyu ni mzaliwa wa pale Singida, lakini anakutwa yupo Dar es salaam; kule Dar es Salaam anahitaji pia kuwezeshwa ni lazima tujue huyu hapa Dar es salaam anakaa wapi? Mtaa gani anafahamika na viongozi wa mtaa huo?

Sasa sehemu kubwa ya vijana wetu wanashindwa kukidhi kigezo hicho kwa sababu na wenyewe wako mobile, wanatembea huku, wanaenda huku katika kutafuta manufaa hayo, katika kujiwezesha kiuchumi. Lakini nini tunakifanya sasa, tunaendelea kuwahamasisha vijana kwenye halmashauri zetu na tunawatambua vijana hawa kupitia Idara yetu ya Maendeleo ya Jamii kwenye halmashauri, tunawatambua vijana kwenye vijiji, idadi yao, mahitaji yao ya shughuli za kiuchumi, huku Ofisi ya Waziri Mkuu kama nilivyosema tumeandaa mpango wa mafunzo ya vijana hawa ili kuwawezesha kuwa mafundi, kuwa na uwezo wa kufanya kazi mbalimbali na mafunzo haya yanachukua miezi sita, yanagharamiwa na Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu, wanaenda vyuoni wakisoma miezi sita, wanarudi wanakuwa tayari wanakuwa na vigezo vya kupata mikopo kwa sababu tayari tunafahamu anakokaa, ana ujuzi, unajua akichukua fedha anaenda kuitumia kwa ajili ya moja, mbili, tatu. Jitihada hizi zinaendela kupanuliwa wigo ili sasa tuweze kuwafikia vijana wote.

Mheshimiwa Spika, na mwisho niliishia na ushauri kwa vijana wetu, pindi wanapomaliza mafunzo haya, wanapokuwa pamoja kwa maana ya kuunda vikundi wanakuwa vizuri zaidi, huo ni ushauri na wanapofikiwa ni rahisi wao wakiwa kikundi kukopesheka kuliko wakiwa mtu mmoja mmoja.

Kwa hiyo, tunaendelea kufanya maboresho kwenye maeneo yote haya; kwanza kuwa na vigezo, lakini mbili kuweza kuwafikia na kutunisha mfuko ili waweze kunufaika. Jitihada hizi zinaendelea na tunaendelea sasa kukusanya Wizara zote ambazo zinahusika na vijana ikuwemo na Wizara ya Utamaduni, Sanaa na Michezo, Ofisi ya Rais, TAMISEMI na Ofisi ya Waziri Mkuu yenyewe na wadau ambao tunao na jumuiya mbalimbali za dini na vijana zote hizi zinatumika katika kuhakikisha tunakusanya nguvu ya pamoja kuwawezesha vijana ili kuweza kuwawezesha kiuchumi.

Mheshimiwa Spika, huo ndio utaratibu tunautumia kwa sasa, lakini nikiri kwamba maswali yote mawili yanaweka msisitizo kwa vijana, kwa hiyo Serikali tutapanua wigo wa kutoa huduma kwa vijana zaidi ili malengo ya vijana yaweze kufikiwa, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister