Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 10 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2023-02-09

Name

Kilumbe Shabani Ng'enda

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kigoma Mjini

Primary Question

MHE. KILUMBE S. NG'ENDA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kunipa nafasi ya kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu wa Jamhuri ya Muungano wa Tanzania.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali imekuwa na utaratibu wa kuchukua maeneo ya wananchi kwa ajili ya miradi ya maendeleo pale ambapo Serikali haina eneo la kufanya miradi hiyo hasa hasa miradi kama ya shule, hospitali au kupanua maeneo ya jeshi au uwekezaji, na baada ya kuchukua maeneo hayo hufanyiwa tathmini ili watu waweze kulipwa fidia. Hata hivyo kumekuwa na tatizo la ucheleweshaji wa kulipa fidia na sehemu nyingine kuingia hata mambo yasiyokuwa ya uaminifu katika utekelezaji wa ulipaji wa fidia.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini msimamo wa Serikali katika jambo hili?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Ng’enda, Mbunge wa Manispaa ya Kigoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, upo utaratibu wa Serikali wa kuchukua maeneo mbalimbali ya ardhi yetu, kwa ajili ya miradi ya maendeleo pale ambapo tunaona tunahitaji kutekeleza mradi maalum kwa maslahi ya Watanzania na kwa hili naomba nianze kueleza umma wa Watanzania kuwa ardhi yetu hii ni ya umma na Mheshimiwa Rais, ndio mdhamini wa ardhi hii. Mheshimiwa Rais anaweza kuchukua ardhi popote kwa maslahi ya umma, kwa lengo la kutekeleza mradi ambao unaweza kusaidia jamii ya eneo hilo kuutumia vizuri. Lakini tunapochukua ardhi hiyo huwa tunafanya tathmini ili kulipa fidia ya mali iliyoko kwenye ardhi, inaweza kuwa labda nyumba au mazao, lazima yafanyiwe tathmini.

Mheshimiwa Spika, ni kweli mara kadhaa Serikali tumekuwa tukichukua maeneo mbalimbali nchini kwa ajili ya miradi ya umma na tunapokuta kuna mali imewekezwa na mtanzania huwa tunalipa fidia.

Sasa suala la ucheleweshaji ni taratibu vigezo kama havijakidhi; moja, wakati tunafanya zoezi la tathmini ni lazima tufahamu nani hasa yuko hapo na amewekeza hiyo na lazima kuwe na viambata vinavyoeleza kwamba huyu ndio mwenye eneo hili na tunampiga na picha, thamani inatambulika hapo hapo na yeye anatambua thamani yake halafu maandalizi ya kulipa fidia yanafanywa.

Mheshimiwa Spika, ucheleweshwaji unakuja kama zoezi hilo halijakamilika au kuna migogoro ya wao kwa wao, wanagombania eneo hilo kwa umiliki, hapo inaweza kuchelewa, na wakati mwingine tathmini na idara inayolipa labda kama ilikuwa inategemea bajeti kunaweza kuwa na- delay, lakini niendelee kuwahakikishia Watanzania ambao wanafikiwa maeneo yao kwa ajili ya tathmini, kwa ajili ya kutumika kwa miradi na tunafanya tathmini kama kunachelewa. Hakuna Mtanzania, hakuna mwananchi ambaye anachukuliwa ardhi na huku akiwa amewekeza, tukafanya tathmini akakosa stahiki yake.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo Serikali itaendelea kusimamia maeneo hayo na kama yako maeneo labda pale Kigoma kuna eneo ambalo tathmini ilishafanyika na bado hatujalipa kutakuwa na moja kati ya haya niliyoyasema; au kuna migogoro, labda idara ilifanya tathmini hiyo na ilikuwa haijajiandaa na kama haijajiandaa tunarudi kwenye sheria yetu ile ya kwamba toka siku ya tathmini mpaka siku ya malipo ikiwa zaidi ya miezi sita lazima ifanyike tathmini tena ili kujua thamani halisi ya wakati huo ili sasa kuwezesha idara, lakini wananchi kujipanga kwa ajili ya kupata fidia yao.

Mheshimiwa Spika, hayo ndio maelezo sahihi ya Serikali ambayo yanatumika wakati wote tunaopohitaji kuchukua eneo na kufanya tathmini na kulipa wananchi. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister