Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 9 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2022-11-03

Name

Jackson Gedion Kiswaga

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kalenga

Primary Question

MHE. JACKSON G. KISWAGA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi nami niweze kuuliza swali.

Mheshimiwa Spika, naomba kumwuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu kwamba, kwa kuwa suala la Mlima Kilimanjaro ni suala nyeti kwa uchumi wa nchi, na ni maeneo muhimu sana ambayo yanatuletea fedha nyingi pamoja na Ngorongoro na Serengeti; na Jeshi la Kujenga Taifa limeonesha uwezo mkubwa katika operesheni mbalimbali katika nchi hii: -

Je, kwa nini sasa Serikali isione umuhimu wa kuwa hata na kambi ndogo ndogo mbili hata za wanajeshi watano au sita, kuzunguka Mlima Kilimanjaro? Kwa sababu kwenda mbele inawezekana kuna wivu mkubwa unajitokeza kwa sababu ya matangazo makubwa ambayo tunayafanya ya kuleta watalii katika nchi hii.

Swali ni kwamba je, kwa nini Serikali isione umuhimu wa kuwa na kambi kambi ndogo ndogo mbili za Jeshi ili kulinda Mlima Kilimanjaro?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kiswaga, Mbunge wa Kalenga, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, tukio hili moto Mlima Kilimanjaro linajitokeza pia na maeneo mengine na linatokana na baadhi ya watu wasiopenda mema ambao pia hawataki hata uhifadhi, huchoma moto maeneo yote yanayotakiwa kuhifadhiwa kama ambavyo ingekuwa kupitia elimu mbalimbali zinazotolewa kwenye Mamlaka ya Serikali za Mitaa.

Mheshimiwa Spika, kwa kuwa sasa tumeona tatizo hilo na katika kipindi cha muda mrefu tulikuwa hatujapata moto kiwango hicho kwenye Mlima Kilimanjaro, lipo jambo tumejifunza. Ushiriki wa majeshi yetu yote; JWTZ, Jeshi la Mgambo, Jeshi la Polisi, na wananchi pamoja na Skauti na makundi mbalimbali yaliyojitokeza kwenda kuzima moto, tayari baada ya zoezi hilo litakapokamilika, tutakaa chini kufanya tathmini.

Swali lako ambalo limeingia pamoja na ushauri, tutauzingatia ili sasa tuwe na mkakati endelevu kwenye maeneo mengi muhimu ambayo yanaweza kujitokeza tatizo la moto, ikiwemo na kuimarisha Kitengo cha Maafa na hasa kwenye maeneo ya moto. Kuwa na vifaa, kuwa na wataalam ambao pia wanapata mafunzo ya mara kwa mara ili tuweze kukabiliana na majanga haya yanapotokea popote pale.

Mheshimiwa Spika, naomba kupokea pia na ushauri aliutoa Mheshimiwa Kiswaga. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister