Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2022-02-10

Name

Sophia Hebron Mwakagenda

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. SOPHIA H. MWAKAGENDA: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa nafasi ya kumuuliza Waziri Mkuu swali. Mwaka 1994 aliyekuwa Waziri Mkuu, Ndugu yetu Samuel Malecela, alitoa tamko juu ya mabasi yanayosafiri usiku na kusema yasisafiri usiku. Tamko lile halikuwa na sheria wala sera. Ni nini Serikali sasa inasema kwa kuwa, nchi yetu sasa imekuwa ni nchi ya kati na uchumi unatakiwa uende mbele.

Mheshimiwa Waziri Mkuu unaonaje kwamba, mabasi hayo yaruhusiwe kutembea usiku na mchana ili tuweze kuongeza kipato, na hasa pato la Taifa kwa Watanzania wote kwa kuwa, mabasi yakifanya mchana peke yake tunalala usiku bila kuingiza fedha yoyote? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mwakagenda, Mbunge wa Mbeya, lakini sio Mbeya Mjini, Mbunge wa Mkoa wa Mbeya, kama ifuatavyo:- (Kicheko)

Mheshimiwa Spika, mara kadhaa tumekuwa tukitoa maelekezo, hasa kwenye eneo la usafiri, kulingana na hali ya usalama iliyoko nchini. Wakati huo agizo hili lilitolewa kwa sababu, mara nyingi mabasi yalikuwa yanatekwa yanaposafiri na tulikuwa tunalazimika pia kuweka jeshi la polisi kila basi linaposafiri ili kuhakikisha kwamba, wasafiri wanasafiri salama.

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba, sasa usalama umeimarika nchini na Serikali inaendelea kuimarisha zaidi usalama nchini. Umuhimu wa hilo jambo upo, lakini nitawasiliana na vyombo vya ulinzi na usalama kuona kama, je, wamejiridhisha kwa kiasi gani kwa usalama huo, ili tuanze kuruhusu mabasi kufanya kazi wakati wote, ili kuboresha uchumi, lakini kuwafanya abiria kuwa na mipango binafsi ya kibiashara ya kusafiri kutoka eneo moja mpaka eneo lingine katika kuendesha biashara zao kwa uhuru mkubwa.

Mheshimiwa Spika, katika hili lazima pia tutoe wito kwa Watanzania; kudumisha amani na usalama na utulivu nchini ni muhimu sana kwa sababu, malengo yetu ya kuboresha uchumi wa nchi, kama nchi haiko salama hatutayafikia. Wito uliotolewa na Mheshimiwa Mwakagenda unaendelea kusisitiza na kuonesha umuhimu wa Taifa hili kuendelea kuwa salama ili wale wanaoamua kufanya biashara zao wakati wowote wafanye biashara hizo.

Mheshimiwa Spika, pia tumeanza kutoa wito hata kwenye mamlaka ya Serikali za Mitaa kupitia masoko yao makuu kuhakikisha kwamba masoko haya yanafanya kazi masaa 24 ili kuwaruhusu hata wanaokuwa busy mchana kutwa kwenye ofisi zao waweze kufanya hivyo wanapopata muda wa mapumziko ambao pia ni usiku kama ambavyo tunaona kwenye nchi zilizoendelea za wenzetu, watu wanaenda shopping center, biashara zinafanywa masaa 24 na sasa tunataka Tanzania hiyo pia ijitokeze kuanzia kwenye masoko yetu, kwenye usafiri. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama ambavyo nimeagiza vyombo vya ulinzi hasa Jeshi la Polisi kupitia Kamati za Ulinzi na Usalama za Mikoa na Wilaya waendelee kufanya tathmini hiyo kwa haraka ili tupate taarifa hiyo tuweze kutoa vibali hivyo vya kusafiri nyakati hizo ili kazi ziendelee. Ahsante sana.

Additional Question(s) to Prime Minister