Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2022-02-10

Name

Iddi Kassim Iddi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Msalala

Primary Question

MHE. IDDI K. IDDI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana. Kumekuwepo na ongezeko la bei za bidhaa mbalimbali nchini kote, lakini hasa Mkoa wa Shinyanga, Wilaya ya Kahama, Jimbo la Msalala na hususan bidhaa hizo ni mafuta ya kula, sabuni, lakini pia vifaa vya ujenzi kama nondo, simenti. Ni nini sasa kauli ya Serikali juu ya ongezeko au mfumuko wa bei katika bidhaa hizi mbalimbali? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Iddi Kassim, Mbunge wa Msalala, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, kumejitokeza siku za karibuni kupanda kwa bei kwa baadhi ya bidhaa zinazozalishwa hapa nchini. Upandaji wa bei hizi wakati mwingine ni wa makusudi unaofanywa na baadhi ya wafanyabiashara ambao sio waaminifu, lakini pia, upatikanaji wa malighafi. Viwanda vyote ambavyo vinazalisha hapa nchini vingi miongoni mwake vinategemea malighafi kutoka hapa nchini na malighafi zipo.

Mheshimiwa Spika, nakumbuka siku tatu, nne zilizopita, Mheshimiwa Dkt. Ashatu Kijaji, Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara, amezungumza na Taifa kwa kuwaambia kwamba, uko mkakati wa baadhi ya wafanyabiashara waovu wasiokuwa na nia njema wa kupandisha bidhaa kwa makusudi tu; moja, kwanza wanazalisha kidogo sana ili kutengeneza upungufu mtaani ili bei ziweze kupanda. Mbili, kumekuwa na utamaduni sasa wa baadhi ya wafanyabiashara waovu kukaa pamoja na kujadili tu bei ziweje na kusababisha mfumuko wa bei. Serikali tumeligundua hilo na ndio kwa sababu, Waziri Dkt. Kijaji, ametoka hadharani kutueleza mkakati wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, naunga mkono kauli yake, lakini pia, natoa agizo kwa wafanyabiashara kuacha tabia hiyo ovu inayosababisha jamii kushindwa kupata bidhaa kwa gharama nafuu kwa sababu, wakati tunawekeana mikataba na wakati tunajenga mazingira rahisi ya uwekezaji nchini, lengo la kwanza kubwa ilikuwa ni kupata bidhaa kwa wingi, kwa bei nafuu, lakini pia zipatikane wakati wote, sasa wengine wanaanza kukiuka masharti yetu.

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Waziri ametoa ultimatum kwao, nami narudia tena, hatutasita kuchukua hatua kwa wafanyabiashara ambao wanaweka mkakati tu wa kutaka kusumbua jamii kwa kununua bidhaa kwa bei ya juu bila sababu yoyote, kwa sababu, bidhaa tunazo, malighafi tunazo na viwanda vipo, uboreshaji ndani ya Serikali wa uwekezaji tumeufanya kwa kiasi kikubwa na kila siku tunakutana nao na wanaeleza namna ambavyo tungependa Serikali iwe na sisi Serikali tunafanya.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hili ambalo Mheshimiwa amelieleza, Serikali itaendelea kuchukua hatua kali na tutasimamia upandaji wa bidhaa hizi usiende kupanda mara zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niiagize taasisi yetu inaitwa FCC, ambayo inasimamia haki za wafanyabiashara katika kufanya biashara, ihakikishe inafanya ukaguzi wa kina kila bidhaa zinazozalishwa na mauzo yao, walinganishe na uzalishaji wao, uwezo wa kiwanda kwa mwaka, tuone kama je, wanazalisha kwa kiwango kilekile tulichokubaliana au wamepunguza uzalishaji kutengeneza upungufu? Pia tujue kwa nini wanapandisha bei, kati ya kiwanda na kiwanda bei zinatofautiana? Hili nalo tutalifanyia kazi.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niahidi kwamba, tutalifanyia kazi kupitia taasisi zetu za ndani ya Serikali, kama alivyoahidi Mheshimiwa Waziri wa Uwekezaji, Viwanda na Biashara. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister