Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 6 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2022-02-10

Name

Leah Jeremiah Komanya

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Meatu

Primary Question

MHE. LEAH J. KOMANYA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipatia nafasi hii muhimu. Kumekuwa na changamoto ya ukame kujirudiarudia nchini kwetu na matokeo yake ukame huu umeleta athari nyingi, ikiwemo mifugo kufa kwa kukosa malisho.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, je, Serikali ina mkakati gani wa muda wa kati na wa muda mrefu wa kukabiliana na ukame huu hususan kwenye malisho ya mifugo? Nashukuru. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Komanya, Mbunge wa Meatu, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, amezungumzia ukame, anataka kujua mpango wa Serikali wa kukabiliana na ukame huu; ukame unaojitokeza mara nyingi nchini ni mabadiliko ya hali ya tabianchi ambayo yanaleta athari ya kukosekana kwa mvua na hasa pale ambapo athari hizo zinasababisha kutopata mvua kama ambavyo mwaka huu na mwaka uliopita hapa nchini kwetu, maeneo mengi yalikuwa makame kwa sababu hakuna mvua. Hii ni kutokana na mabadiliko ya tabianchi, lakini pia, ukame huu unatokana na uharibifu tu wa mazingira ambao wananchi wanaufanya kwenye maeneo yetu kwa kukata misitu na maeneo ambayo tunategemea sana kuwa na mvua.

Mheshimiwa Spika, Ofisi ya Makamu wa Rais, Mazingira, imeendelea kutoa elimu ya wananchi kuhifadhi mazingira kwenye maeneo yao ikiwemo misitu, ili isaidie kuleta mvua kwenye maeneo hayo kuachana na ukame. Hiyo ndio njia moja muhimu ambayo mimi naiona, lakini pia umehusisha maeneo ya malisho ya malisho ya mifugo. Kutokana na ukame huu ni kweli hatupati malisho na kwa hiyo, ni lazima pia tuhakikishe kwamba, tunaendelea kuhifadhi mazingira haya tupate mvua ili malisho mengi yaweze kupatikana.

Mheshimiwa Spika, ukiondoa ukame, lakini bado hata Wizara ya Mifugo na Uvuvi wanajitahidi sana kutoa elimu kwa wafugaji kuhakikisha kuwa wanafuga kitaalam kulingana na ukubwa wa malisho waliyonayo, ili kukabiliana na upungufu wa malisho ambayo kwa sasa yanakuwa hayapatikani kwa sababu ya kuwa na mifugo mingi zaidi. Jana tumelizungumza hapa ndani ya Bunge juu ya Ngorongoro kule, uharibifu unaoendelea kule Ngorongoro itakwisha, lakini hili ni sisi wenyewe ndio tutaweza kukabiliana nalo na kwa kuwa Serikali imeweka mkakati wa kuelimisha umma juu ya uhifadhi wa mazingira, lakini pia Wizara ya Mifugo inaendelea kuwaelimisha wafugaji, ili tuanze kuandaa malisho kwa kuhifadhi malisho, lakini pia tuweze kuchimba visima kupata maji ya chini na kuanza kumwagilia kwenye maeneo ambayo tumeyatenga kama maeneo ya malisho.

Mheshimiwa Spika, kwa ujumla wake kwenye mifugo tumefanya jitihada kubwa sana za maeneo yetu yale ya ranch. Tumegawa vipande, vinaitwa blocks na kuwagawia wafugaji ili kila mmoja aweze kutunza maeneo hayo na ikiwezekana pia na kupanda nyasi ikiwa ni njia ya kupata malisho mapya, ili mifugo iweze kuendelea.

Mheshimiwa Spika, nitoe wito sasa kwa Watanzania, ili kukabiliana na ukame ambao unaendelea ni lazima tuungane pamoja turekebishe, tuache tabia ya kukata miti na misitu kwenye maeneo tuliyonayo ili misitu hii iweze kutusaidia kupata mvua za kutosha. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nitoe wito pia kwa ndugu zangu wafugaji waendelee kufuga kitaalam, tuwe na mifugo michache unayoweza kuihudumia ikiwemo kupata na malisho, ikiwezekana pia hata kuboresha malisho kwa mifugo uliyonayo badala ya kuwa ng’ombe zaidi ya 2,000 ambao hauna uwezo wa kuwafuga na matokeo yake kukosa malisho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, huo ndio ujumbe wangu kwa swali ambalo Mheshimiwa Mbunge ameliuliza. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister