Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 5 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2021-11-11

Name

Fatma Hassan Toufiq

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. FATMA H. TOUFIQ: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa nami niweze kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, sekta ya usafirishaji hasa bodaboda imekuwa ni ajira kubwa sana kwa vijana, lakini kumekuwa kukitokea ajali ambazo zimekuwa zikisababisha vifo na ulemavu kwa vijana wetu kutokana na kukosa elimu ya usalama barabarani. Nini mkakati wa Serikali katika kutoa mafunzo ya mara kwa mara ili kuwaepusha nguvukazi hii na ajali hizi? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa Toufiq, Mbunge wa Mkoa wa Dodoma, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, nami nikiri kwamba sekta ya bodaboda inayosimamiwa sana na vijana wetu imeweza kusaidia sana kupunguza tatizo la usafiri wa umbali mfupi mfupi na wakati mwingine hata umbali mrefu; na tunaona vijana wetu wa bodaboda wanafanya kazi nzuri. Pamoja na changamoto zilizopo, lakini huduma yao Serikali tunaitambua na tutaendelea kuisimamia ili iendelee kuboreshwa vijana hawa waweze kufanya kazi hiyo kusafirisha watu, lakini wapate pato la mtu mmoja mmoja, linasaidia sana kwenye familia zao.

Mheshimiwa Spika, tunatambua kwamba zipo ajali zinazoweza kutokea au kwa bahati mbaya, lakini wakati mwingine kwa uzembe. Tunachofanya ni kuimarisha elimu. Jeshi letu la Polisi limekuwa na mpango mzuri kabisa wa kuwafuata vijana hawa kwenye maeneo yao na kutoa elimu. Watanzania tunaona baadhi ya makamanda wa Jeshi la Polisi wakiwa wako mbele za vijana wa bodaboda wanawaelimisha baadhi ya mambo ambayo wanatakiwa kuyazingatia ili wafanye kazi yao vizuri pamoja na kupunguza ajali pia.

Mheshimiwa Spika, tunashukuru sana pia hata vyombo vya habari ambavyo vimekubali kutoa nafasi ya Jeshi la Polisi kwenda kutoa elimu kwa vijana wetu wa bodaboda. Tunaimarisha sasa kwa kila mwendesha pikipiki au bodaboda kwamba apate leseni na kuwahamasisha kuwa na angalau ile helmet. Yaani yale masharti yote yale ya usalama, kuendesha chombo cha moto waweze kuyakamilisha ili huduma hii iendelee kushamiri na iendelee kuwanufaisha wanaotumia.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Serikali katika hili, nafasi yetu ni kuendelea kuimarisha utoaji elimu kwa vijana wanaoshughulika na bodaboda ili wajue kwanza kazi na thamani ya kazi yao. Pili wasaidie sana kwa kuzingatia sheria kupunguza ajali. Hili jambo ni muhimu sana na tumeendelea kulisimamia hilo.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, nimhakikishie Mheshimiwa Mbunge kwamba eneo la bodaboda kwanza Serikali tumelitambua na tumeendelea kuliimarisha na tutaboresha zaidi kwenye eneo hili. Pili mkakati huo wa kielimu tutaimarisha zaidi na tutawafikia wananchi, hao vijana wanaoshughulikia bodaboda mpaka kwenye vituo vyao ili kurahisisha na wao kuwaondoa kwenye maeneo hayo kwa ajili ya kupata elimu. Kwa hiyo, tutaendelea kuimarisha eneo hili na hayo ndiyo malengo ya Serikali. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister