Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2021-09-09

Name

Aida Joseph Khenani

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Nkasi Kaskazini

Primary Question

MHE. AIDA J. KHENANI: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa nafasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, mwaka 2017 Serikali ilikuja na utaratibu wa upigaji chapa kama eneo la kutambua mifugo nchini. Zoezi hilo lilikuwa na changamoto zake ikiwepo chapa hizo kupotea au kufutika pamoja na ngozi kukosa ubora. Kupitia Bunge lako Tukufu, Bunge liliitaka Serikali kuja na namna bora ya utambuzi wa mifugo. Mwaka huu Serikali imekuja na utaratibu mpya wa kuvalisha hereni mifugo; zoezi ambalo limeanza tarehe 17 mwezi wa Nane mwaka huu kwenye baadhi ya mikoa.

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hilo ni zuri kwa sababu lina barcode ya nchi, mkoa, wilaya na jina la mfugaji. Hata hivyo, changamoto kwenye zoezi hilo ni pamoja na gharama ya shilingi 1,750 kwa kila ng’ombe. Lakini ng’ombe huyo akipoteza hereni mfugaji analazimika tena kulipia.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa kuwa nia ya Serikali ni njema na itakwenda kuondoa wizi wa mifugo uliopo sasa hivi. Serikali haioni kuwa ni vyema iende ikafanye tathimini upya ione namna bora kwanza kupunguza gharama lakini kuona namna bora wataweka hiyo hereni na isiweze kuondoka kwenye mifugo? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Aida Khenani, Mbunge wa Nkasi kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba Serikali imetafuta njia nzuri sana ya kufanya maboresho ya utambuzi wa mifugo yetu, ng’ombe wakiwemo. Na mfumo huu ulitokana na tatizo kubwa sana la wizi wa mifugo hapa nchini pamoja na kukosa takwimu sahihi za mifugo yetu hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, tumetafuta njia kadhaa za kuweza kutambua na kupata takwimu za ng’ombe hawa. Awali tulikuwa tunatumia njia ya kupiga chapa, lakini tumegundua kwa kupiga chapa tunapoteza ubora wa ngozi ambapo ngozi zetu sasa nchini Tanzania haziuziki nje; na hata tulipoanza kutumia Kiwanda chetu cha Kilimanjaro Leather kwa kutengeneza viatu, ngozi zote zilizopigwa chapa hazitumiki vizuri kwa sababu zenyewe zimepoteza ubora. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa tumetafuta njia nzuri ya kuweza kutambua hawa ng’ombe, tukaamua kutumia njia ya kuvalisha hereni. Kwanza mwanzo tulikuwa tunatoboa lakini sasa hatutoboi bali tunaibandika. Inawezekana pia ng’ombe mmoja mmoja kutokana na kupita kwenye majani na miti hereni zinadondoka. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kupitia kikao cha juzi cha mifugo ambacho mimi mwenyewe nilikuwa mgeni rasmi na mjadala uliofanyika kwenye kikao kile juzi pale Jijini Dar es salaam, kwenye eneo hili Wizara ya Kilimo wameondoa hizo tozo; endapo ulinunua kwa mara ya kwanza na sasa ng’ombe amepoteza herein. Tunachofanya ni kurudi tena kwenye mtandao na kujaza zile data zote kwenye hereni mpya tunampa mfugaji ili ng’ombe aendelee kuwa na ile alama aendelee kutambulika. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo hatua nzuri ya kumuondolea gharama mfugaji ni hiyo ya kumrudishia tena ile hereni ili aweze kuivaa. Pili, hereni hii tumekuwa makini sana, hatutoboi tena bali tunatafuta namna ya kuigandisha vizuri pamoja na ile spring inabana vizuri kiasi kwamba hata akiwa na pilikapilika haiwezi ikadondoka kwa urahisi zaidi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunaendelea kutafuta njia nzuri zaidi ya hiyo. Niseme sasa kwamba tumepokea mawazo yako, na uzoefu ambao tumeuona kupitia wafugaji wetu kwamba hizi zinadondoka na kunakuwa na shida tena kurudi ofisini kupata hereni nyingine, kwa hiyo tunatafuta njia nzuri zaidi ya kutambua ng’ombe hawa kwa kuweka alama ambayo haitaharibu ubora wa masikio ya ng’ombe lakini pia haitasababisha gharama tena kwa mfugaji ili gharama ile ile aliyoitumia kwa mara ya kwanza iendelee kutumika kama alama ya kumtambulisha ng’ombe huyo. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister