Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 4 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2021-09-09

Name

Tarimba Gulam Abbas

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kinondoni

Primary Question

MHE. TARIMBA G. ABBAS: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana. Naomba na mimi nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa majibu mazuri ya swali lililopita lakini naomba nimuulize juu ya changamoto ambazo zipo katika matumizi ya Sheria ya Road Traffic (Road Traffic Act), ile Cap 168 pamoja na Kanuni zake.

Mheshimiwa Naibu Spika, kumekuwepo na matatizo ya matumizi ya barabara hasa kwa waendesha pikipiki/ bodaboda ambao wanakiuka sheria zilizopo katika mahitaji ya jinsi gani ya kuendesha vyombo vyao. Na sasa imezidi pale Dar es salaam hasa watumiaji wa barabara za mwendokasi, madereva wa mwendokasi wanapita kwenye taa nyekundu; hadi jana usiku saa moja na nusu wameua vijana wawili.

Ni nini kauli ya Serikali katika kuhakikisha watumiaji wote wa vyombo vya moto barabarani wanafuata sheria na kwamba polisi/trafiki wanasimamia sheria zile ipasavyo?

Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Abbas Tarimba, Mbunge wa Kinondoni kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, sheria hizi ambazo tumeziweka sisi hapa Bungeni tunatarajia kwamba kila Mtanzania atakuwa anatekeleza wajibu wake bila ya kushurutishwa. Matumizi ya barabara yameainishwa kikamilifu kupitia sheria zetu na usimamizi unaendelea pia kwa vyombo ambavyo tumevipa jukumu la kusimamia kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Naibu Spika, lakini usimamizi wa sheria hautakiwi usimamiwe na Jeshi la Polisi peke yake tu, kila Mtanzania anatakiwa kufuata sheria pale ambapo sheria imeshatungwa na inataka itekelezwe.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli kwamba watumiaji wa pikipiki walio wengi hawajali matumizi haya ya sheria zetu na kujali kwamba sheria hizi ni lazima zitekelezwe. Lakini pia Jeshi letu la Polisi linacho kitengo kinatoa elimu kila siku, na Waheshimiwa Wabunge na Watanzania wote mnajua kwenye televisheni zetu za TBC, ITV, Star TV lakini pia Azam tumetengewa muda na Jeshi la Polisi linafanya kazi hiyo vizuri sana, kuelimisha Watanzania kuhusu matumizi sahihi ya barabara. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, wakati tunasimamia sheria hizi nitoe wito kwa watumiaji wa barabara hasa watumiaji wa vyombo vya moto wote kwamba ni muhimu sana kuzingatia Sheria za Barabarani. Hii ni muhimu sana kwa sababu inalinda uhai wa Watanzania wote, kuanzia yeye mtumiaji wa chombo chenyewe cha moto, watumiaji wa njia hizo wanaotumia kwenda kwa miguu lakini pia pamoja na wale wanaotumia barabara hizi za mwendokasi.

Mheshimiwa Naibu Spika, kuhusu njia hii ya mwendokasi tumeshaieleza wazi, kwamba njia hii tumeitenga maalum kwa ajili ya magari ya mwendokasi, lakini pia tumetenga njia nyingine kwa ajili ya magari yetu ya kawaida. Tumejenga na njia ya pembezoni ya watembeaji wa miguu pamoja na vyombo vingine vya moto. Kwa hiyo, ni wajibu wetu Watanzania kutekeleza sheria, ikiwemo na kujali matumizi ya barabara zetu hizi. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, mkakati wa Serikali hapa ni kuendelea kutoa elimu na kusimamia sheria. Pale ambapo tunaona kuna mtu anavunja sheria, hatua za kisheria zinachukuliwa hapohapo; huo ndio mkakati ambao tunao kwa sasa. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister