Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 53 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 6 2021-06-17

Name

Jerry William Silaa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ukonga

Primary Question

MHE. JERRY W. SILAA: Mheshimiwa Naibu Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, tarehe Sita ya mwezi Aprili Mheshimiwa Rais katika shughuli ya kuapisha Makatibu Wakuu alitoa kauli ya kusikitishwa kwa jinsi wawekezaji wanavyokwamishwa kwenye vibali vya kazi. Katika kauli yake alitoa maelekezo ya Serikali kutengeneza utaratibu mzuri wa kuwasaidia wawekezaji kutopata mkwamo katika suala la vibali vya kazi ili kuweza kuboresha uwekezaji. Mheshimiwa Waziri Mkuu, kauli hii imepokelewa kwa furaha sana na wawekezaji wengi na imetoa sura mpya katika sekta ya uwekezaji nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kuna baadhi ya maeneo kauli hii imechukuliwa tofauti na baadhi ya wafanyabiashara wasiokuwa waadilifu wameanza kuleta wafanyakazi kwenye maeneo ambayo wazawa wanaweza kufanya kazi hizo. Mfano ni marubani kwenye baadhi ya kampuni binafsi za ndege. Naomba kujua kauli ya Serikali, ni nini mkakati wa kutekeleza maagizo ya Mheshimiwa Rais katika kuwaondolea vikwazo na urasimu wawekezaji kupata vibali vya kazi, wakati huohuo kuendelea kutimiza matakwa ya sheria The Non- citizens Employment Act, 2015 Kifungu cha 11(2) ambacho kinalinda ajira za Watanzania kwenye maeneo ambayo wana uwezo wa kufanyia kazi. Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jerry Silaa, Mbunge wa Ukonga kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge ameeleza utekelezaji wa maelekezo ya Mheshimiwa Rais aliyoyatoa alipokuwa anawaapisha Makatibu Waku una hasa katika kuboresha uwekezaji nchini. Uwekezaji nchini ni mkakati mpana kwa sababu kwanza tunahamasisha kujenga uchumi wetu na katika ujenzi wa uchumi moja ni kukaribisha wawekezaji wa nje na ndani ya nchi kwenye uwekezaji lakini wawekezaji hawa nao wanao watu ambao wanaamini wanawaamini kushiriki kwenye shughuli zao za uendeshaji wa uwekezaji wao. Sasa nasi Serikali tumeweka sheria kidogo kwa wawekezaji ambayo haipanui wigo mpana ukapoteza fursa ya Watanzania kushiriki kwenye uwekezaji huo ikiwemo na ajira. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Mheshimiwa Mbunge anapotaka kujua tunachukua hatua gani ya wale ambao wanatumia nafasi hii vibaya, Serikali kupitia Ofisi ya Waziri Mkuu kwa bahati nzuri hili jambo lipo ofisini kwangu na tunalisimamia vizuri. Kwanza tunahamasisha wawekezaji wote kuja nchini kuwekeza kwenye sekta mbalimbali kwa fursa tulizonazo lakini mbili tunawahamasisha Watanzania kushiriki kwenye uwekezaji huu ili na wao wawe sehemu ya ujenzi wa uchumi kupitia uwekezaji. Pia kwenye uwekezaji huu tumetangaza fursa zilizopo ajira lakini pia bidhaa tunazozalisha kuwa kama malighafi ya uwekezaji huo ikiwemo na kilimo na vinginevyo kwamba Watanzania washiriki huko ili waweze kunufaika na uwekezaji huu kwenye maeneo hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, sasa pale ambapo Mwekezaji anataka kuja kuwekeza na fedha yake lakini ana idadi ya watu anaotaka kufanya kazi, nalo pia tumeliangalia kwamba mwekezaji huyu asije akaleta idadi kubwa halafu akapoteza fursa za Watanzania kuingia pia kwenye ajira. Nini tunakifanya sasa tunatengeneza sheria na maboresho ya sheria zetu zinazoweza kuwafanya wawekezaji wasikwazwe kuwekeza nchini lakini na sisi Watanzania tusipoteze fursa ya kuweza kuajiriwa ili tuweze kwenda pamoja.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, matumizi ya fursa hiyo vibaya nataka nimhakikishie tu Mheshimiwa Mbunge kwamba tunasimamia vizuri na hasa maboresho ambayo tunayafanya kwenye uwekezaji. Maboresho haya yana nia njema sana hasa katika kutoa fursa kwa Watanzania kwenye maeneo mengi tu, kwamba maeneo haya yote ambayo tunayalenga yaweze kuwanufaisha Watanzania, ndiyo malengo yetu. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, hivyo Mheshimiwa Mbunge asiwe na mashaka maelekezo ya Mheshimiwa Rais tumeyapokea na tunayasimamia ili yasitumike vibaya na wale wenye nia mbaya kwenye maeneo haya. Haya ndiyo malengo ya Serikali kwa hiyo niendelee kutoa wito kwa wawekezaji waje nchini tuna ardhi ya kutosha, maji, umeme, malighafi ya kutosha lakini pia tuna labor inayojituma sasa ya Watanzania kwamba mwekezaji akija Tanzania hawezi kujuta kwa nini amekuja kuwekeza Tanzania. Tunaanza kuona idadi kubwa ya wawekezaji wanakuja na huduma wanaendelea na wanapata vibali kwa siku chache sana kutoka siku wanapoomba kuwekeza hapa nchini.

Mheshimiwa Naibu Spika, Wizara zetu za Uwekezaji na Viwanda na Biashara lakini pia Wizara yetu ya Ardhi zote hizi zinafanya kazi kwa pamoja ili kumwezesha mwekezaji kupata huduma yake kwa haraka sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister