Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 53 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2021-06-17

Name

Jacquline Andrew Kainja

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. JACQUELINE K. ANDREA: Mheshimiwa Naibu Spika, asante kwa kunipatia nafasi ya kuuliza swali kwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, natambua kwamba tumekuwa na Benki ya Kilimo na Tanzania Investment Bank ambazo zimekuwa na riba kubwa vilevile mtaji wake ni kidogo. Lakini pia tumekuwa na mifuko ya kuchochea maendeleo mingi. Je, Serikali haioni kama tuna haja ya kuwa na mfuko wa kuchochea maendeleo ya kilimo na viwanda ili wananchi waweze kwenda kupata mikopo ya kujiwezesha kujiendeleza katika kilimo na viwanda kwa riba nafuu? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kainja, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, Mheshimiwa Mbunge anahitaji kujua mkakati wa Serikali wa kuanzisha mfuko ambao unaweza kutoa mikopo kwa urahisi na kwa gharama nafuu hasa kwenye riba baada ya kuwa ameringanisha uwepo wa benki TADB na TIB. Ni kweli kwamba Serikali inaendelea kuhamasisha taasisi za fedha zote pamoja na mifuko mbalimbali inayolenga kukuza kilimo, ili iweze kuwafikia wakulima wadogowadogo, wa kati na wakubwa ambao watawekeza kwenye viwanda na mashamba yenyewe iliwaweze kupata mikopo tena kwa riba nafuu.

Mheshimiwa Naibu Spika, ambacho kinafanyika sasa ni kwamba mazungumzo yetu kati ya Serikali na mabenki binafsi tumekubaliana mabenki haya kutoa mikopo tena wajitahidi kupunguza riba na hata Mheshimiwa Rais juzi amesisitiza benki zipunguze riba. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, mbili, tukasema tuanzishe benki yetu inayoshughuikia kilimo ili iweze kutoa mikopo kwa gharama na riba nafuu. Na tunayo tayari TADB ambayo inashughulikia kilimo lakini tuna benki ambayo pia Mheshimiwa Mbunge ameitaja TIB (Tanzania Investment Bank) ambayo pia na yenyewe ina eneo linashughulikia kilimo. Wakati huohuo tunayo mifuko mingi sana imejikita kwenye maeneo mbalimbali ambayo sasa tunaishughulikia ili kuipunguza idadi kubwa ya mifuko ili tuwe na mfuko angalu mmoja utakaokuwa unashughulikia kuratibu shughuli za kilimo kwa kukopesha na kuhakikisha kwamba inahudumia sekta nzima ya kilimo. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, zoezi hili litakapokamilika, sasa tutakuwa na mfuko unaoshughulikia kilimo ambao ni wetu wenyewe Serikali ambao pia utakuwa unaungana na Benki yetu ya Kilimo na mabenki mengine ili ihudumie wananchi wa kawaida wanaojishughulisha na kilimo kuanzia kule kwenye ngazi za vitongoji, vijiji na wale wakulima wakubwa ambao pia wanawekeza kwenye viwanda vinavyochakata malighafi za kilimo.

Mheshimiwa Naibu Spika, malengo yetu sasa ni kihakikisha kwamba Sekta ya Kilimo inakua kwa kasi na juzi nilikuwa Mkoani Singida kuzindua kampeni ya kilimo cha alizeti nchini. (Makofi)

Mheshimiwa Naibu Spika, moja kati ya mambo makubwa ambayo wadau walichangia ni kukosekana kwa mitaji ya kuanzisha kilimo lakini nimetoa maelekezo kwa mabenki yetu na tulikuwa na mabenki pale ikiwemo na hizi benki zetu ambazo tunazo mpaka vijijini kama vile CRDB, NMB lakini pia tuna NBC, Azania Bank na hiyo TIB na TADB yenyewe kuhakikisha kwamba inakuwa na matawi mpaka ngazi ya wilaya na inatangaza hiyo fursa ya wakulima kwenda kukopa lakini pia kila benki ihakikishe inawezekana pia inapunguza riba zao ili ziweze kuwawezesha wakulima kumudu kukopa na kurejesha kwa wakati. Wakati mwingine nao wasaidie pia namna ya kuzipata hizo fedha kwa sababu iko tabia ya kila mmoja anataka kukopa lazima awe na andiko, mwananchi wa kawaida hajui andiko.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tumesema lazima waanzishe dawati la kusaidia kutengeneza hilo andiko na halmashauri nazo tumeziagiza na zenyewe ziwe na maafisa wanaoshughulikia namna ya kumuwezesha mkulima kuwa na andiko linalomuwezesha kupata mikopo. Haya yote yatapelekea sasa kwenda kutoa huduma kwa wakulima ili waweze kulima lakini kutoa huduma kwa wawekezaji wa sekta ya kilimo wapate mikopo na wawekezaji kwa kiwango cha kati nao wapate mikopo ili mkakati wetu wa Serikali wa kuboresha kilimo nchini uweze kushamiri.

Mheshimiwa Naibu Spika, malengo yetu ya Serikali ambayo pia Mheshimiwa Rais Samia Suluhu Hassan amesisitiza ni kuhakikisha kwamba kilimo kinashamiri nchini ili sasa maazimio ya uchumi wa mtu mmoja mmoja yatatokana na kila mmoja kujishughulisha kwenye kilimo kwa kupatiwa mitaji na vinginevyo. Kwa hiyo, Serikali tunaendelea na utaratibu huo ili tuweze kutoa mikopo kwa wakulima wetu kwa riba nafuu, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister