Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 38 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2021-05-27

Name

Hawa Mchafu Chakoma

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. HAWA M. CHAKOMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi ili nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, matumizi ya mbegu ya hybrid kwa mazao kama mahindi, maharage, mchele na mengine mengi yamefanya mazao hayo kupoteza ladha lakini pia yanahitaji matumizi makubwa ya mbolea na viuatilifu. Je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha inawekeza katika uzalishaji wa mbegu za asili kibiashara ili kuwawezesha wakulima kuzinunua lakini pia kufanya kilimo cha gharama nafuu na ku-maintain afya za Watanzania?

Mheshimiwa Spika, ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Hawa Mchafu, Mbunge kutoka Mkoa wa Pwani, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, ni kweli ameeleza kwamba yapo baadhi ya mazao ambayo tunatumia mbegu zile tunaita hybrid, zile mbegu ambazo zinakuzwa kwa kutumia madawa ambazo mazao yake yanaweza kuwa yanapoteza ladha kama ambavyo amesema. Hata hivyo, sisi ndani ya Serikali yetu kupitia Wizara ya Kilimo tumeweka Sera ya kuimarisha vitengo vyetu vinavyozalisha mbegu hizi ambazo ni za asili ambazo pia zinaweza zikazalisha kwa kiasi kikubwa. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunavyo vyuo vya utafiti vinaendelea na tafiti mbalimbali kwa mbegu hizi zinazozalishwa na kuona kuwa tunazalisha kwa kiasi kikubwa tuweze kukipeleka kwa wananchi. Pia tumehakikisha kwamba kila tunapolima zao hilo ambalo limetokana na mbegu hizi ambazo tumezitafiti na tumezilima kutokana na uasili wetu, tunatenga kiasi cha mbegu ambacho kitasaidia kulima pia msimu ujao. Tumefanya hivyo kwenye zao la pamba, korosho na mazao ya mahindi na mpunga. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tusingependa sana kuingiza mbegu hizi ambazo zimekuzwa kwa mfumo mwingine kwa sababu zina athari mbalimbali kama mahitaji ya mbolea na vitu vingine. Pia bado tunaendelea kufanya tafiti ya udongo tulio nao ili tuone udongo huo kama unaweza kuzalisha bila ya kutumia mbolea nyingi ili tuweze kuhakikisha kuwa uzalishaji wetu unapanda na unasaidia pia wakulima kupata tija kutokana na mazao wanayozalisha.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, hatua ambayo tunaichukua ni ile ya kuimarisha vyuo vya utafiti na kuongeza idadi ya wataalam, kuwapa fursa ya kufanya tafiti nyingi zaidi ili kupata mbegu. Tunayo taasisi ya mbegu ambayo pia nayo tunaitumia kuhakikisha kwamba inahakikisha tunapata mbegu za kutosha kwa kila zao linalolimwa hapa nchini na vituo hivi tumeviweka vingi kwa kanda ndani ya nchi ili kila kanda waweze kutafiti mbegu zinazolimwa kwenye maeneo hayo.

Mheshimiwa Spika, hizi ndiyo jitihada za Serikali ambazo tunazifanya na tutaendelea kufanya hilo ili Serikali na watu wake kwa maana ya Watanzania wapate manufaa kwa mbegu ambayo tunaizalisha sisi wenyewe na kusimamia kilimo kilicho bora kitakachovuna mazao mengi zaidi kama ambavyo mmejadili hapa kwenye Bajeti ya Wizara ya Kilimo. Kwa hiyo, huo ndiyo mkakati wetu wa Serikali.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister