Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 38 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2021-05-27

Name

Nusrat Shaaban Hanje

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. NUSRAT S. HANJE: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi na mimi nimuulize Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Spika, kumekuwa kuna ugumu wa kupata ajira kwa vijana hasa waliomaliza darasa la saba kwenye taasisi za Serikali hata kama wamepata mafunzo katika fani mbalimbali kwenye vyuo vyetu vya ufundi hata vinavyotambuliwa na Serikali kwa kigezo cha cheti cha form four. Vyuo hivi vinatambuliwa na NACTE na Serikali kwa ujumla, je, Serikali ina mkakati gani kuhakikisha kwamba ina-recognize vijana wetu hawa wa standard seven ambao wanaulizwa kigezo cha form four wakati wamepatiwa mafunzo na wana uwezo wa kufanya kazi hizo? Serikali ina mkakati gani kuwatambua na kuhakikisha kwamba inawasaidia?

Mheshimiwa Spika, ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Nusrat, Mbunge kutoka Mkoa wa Singida, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, katika mazingira ya kawaida ni kweli upo ugumu wa upatikanaji ajira na changamoto ya ajira iko duniani kote ikiwemo na hapa kwetu Tanzania lakini kila Serikali inaweka utaratibu mzuri wa kukabiliana na changamoto hii. Kwetu nchini Tanzania kupitia Serikali yetu inayoongozwa na Mama yetu Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan imeendeleza mkakati wa Awamu ya Tano wa kupanua wigo ambao unaruhusu Watanzania kupata ajira bila ya kuangalia elimu yao; muhimu ni ujuzi na hasa anapozungumzia wale wamepata ujuzi kwenye vyetu vya ufundi vinavyotambulika na Serikali. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mkakati wa ujenzi wa viwanda ndiyo jibu sahihi la kupunguza changamoto hii ya ajira kwa ngazi zote; uwe umemaliza darasa la saba, kidato cha nne, una degree hata ukiwa Profesa unaweza kufanya kazi kwenye viwanda kwa sababu kazi za kufanya zipo nyingi. Kwa hiyo, mkakati wetu wa ujenzi wa viwanda ni miongoni mwa njia moja muhimu ya kuwezesha kupata ajira watu wa kada zote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mbili; tunaendelea pia kuimarisha vyuo vyetu vinavyotoa ufundi stadi kwa sababu unaposoma kwenye vyuo vya ufundi stadi unapata ujuzi, ukipata ujuzi unaweza kujiajiri, unaweza pia ukaanzisha taasisi ukawaajiri wenzako na kuajirika pia kwenye sekta nyingine. Nataka niwaongezee kuwajulisha kwamba hata Ofisi ya Waziri Mkuu tunao mkakati wa kutoa mafunzo ya watu wa ngazi zote ili waweze kupata ujuzi huo wapate nafasi ya kujiajiri, kuajiriwa lakini pia na wale wanaopata ujuzi wakaanzisha kampuni yao na kuweza kuwaajiri wengine; kwa utaratibu huu tumefanikiwa sana. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, katika miaka mitatu iliyopita tuliwahi kukusanya vijana wa taaluma mbalimbali zaidi ya 35,000 tukawapeleka kwenye sekta mbalimbali; kilimo, madini lakini pia utoaji huduma na maeneo mengine, tumewapeleka VETA na Chuo cha Don Bosco, tumewapeleka kwenye mahoteli na maeneo mbalimbali ya utoaji huduma. Wanapokuwa kule asilimia 40 ya muda ni nadharia, asilimia 60 ya muda wao unatumika kwa ajili ya vitendo. Wanapokamilisha mafunzo hayo ya miezi sita wanakuwa tayari wana ujuzi na wengi wamepata mafanikio wameajiriwa na wengine wamejiajiri. Kwa hiyo, huo ndiyo mkakati ambao Serikali inautumia ili kuwezesha kila mmoja kwa ngazi yake kuweza kupata ajira.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister