Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 3 Sitting 38 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2021-05-27

Name

Festo Richard Sanga

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Makete

Primary Question

MHE. FESTO R. SANGA: Mheshimiwa Spika, ahsante kwa kunipa nafasi ya kuuliza swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Spika, naomba kuuliza swali ambalo limejikita kwenye usalama. Siku za karibuni hapa nchini kumekuwa na changamoto ya wimbi la ujambazi ambalo linaendelea hasahasa Mikoa ya Dar es Salaam, Dodoma, Mbeya, Mwanza na Arusha kitu ambacho kimekuwa kikihatarisha usalama wa wafanyabiashara wetu lakini mali pamoja na usalama wa wananchi wetu. Je, ipi ni kauli na maelekezo ya Serikali dhidi ya hivi vitendo viovu ambavyo vinaendelea kwenye Taifa letu?

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, nimshukuru Mheshimiwa Sanga kwa swali hili zuri na muhimu kwa usalama wa nchi yetu. Serikali inao wajibu wa kulinda raia wake kwa usalama wao, mali zao lakini pia kuhakikisha kwamba wanaendesha shughuli zao za kila siku kwa amani na utulivu. Kazi hii inafanywa vizuri na vyombo vyetu vya dola lakini pia kazi hii mara kadhaa tumewaomba Watanzania kushiriki kwenye ulinzi wa nchi yetu pale kila Mtanzania anapopaswa kujilinda yeye mwenyewe, jamii inayomzunguka na hatimaye jamii kubwa kwa ukubwa wake ili kujiridhisha kuwa usalama wa nchi unakuwa imara.

Mheshimiwa Spika, Jeshi letu la Polisi linafanya kazi nzuri sana na siku mbili/tatu hizi nimesikia kazi nzuri wameifanya Jijini Dar es Salaam na Watanzania wote wamesikia na wameona kazi ambayo wameifanya kudhibiti majambazi hawa. Nataka nikuhakikishie kwamba Serikali inaendelea na kazi hiyo ya kuhakikisha kwamba usalama wa raia na mali zao unaendelea. Watanzania wote wanajua kwamba hata Mheshimiwa Rais Mheshimiwa Samia Suluhu Hassan kupitia moja ya hotuba zake Kitaifa ameweza kuwaonya wale wote wanaofikiria kwamba huu ni wakati wa kufanya maovu nchini na amewataka wale ambao walikuwa wanafikiria kufanya hivyo waache mara moja. Anapoagiza haya maana yake anaagiza vyombo vya ulinzi na usalama kuchukua hatua kali dhidi ya wale wote ambao wanasababisha madhara ya usalama kwa Watanzania. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, ni jukumu letu sote kuhakikisha kuwa tunashiriki kikamilifu kwenye ulinzi wa nchi na kila Mtanzania pale anapohisi/anapoona kwamba kuna dalili za upotevu wa amani ni vyema kutoa taarifa kwenye vyombo vya sheria ili hatua kali ziweze kuchukuliwa. Kwa hiyo, bado tunaendelea na jukumu hilo la kulinda nchi, watu wake, mali zao na usalama wao ili nchi hii iendelee kuwa na tunu yake ya amani wakati wote. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, niwasihi Watanzania sasa kuhakikisha kuwa tunatoa taarifa pale ambapo tunaona kwamba kuna tatizo linaloweza kutokea mahali ili majeshi yetu yafanye kazi inayokusudiwa.

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister