Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2021-02-11

Name

Dr. Charles Stephen Kimei

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Vunjo

Primary Question

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa kunipa fursa hii. Naomba nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu swali lifuatalo:-

Mheshimiwa Spika, kwa vile Serikali iliona umuhimu wa kuwafikishia wananchi kule vijijini umeme kwa gharama nafuu, kwa hivyo wakaweka utaratibu wa kuunganishia nyumba umeme kwa Sh.27,000 tu. Je, Serikali haioni umuhimu kwa kuzingatia kwamba maji ni uhai na ni hitaji kubwa sana kwa kila mtu hapa duniani, kuhakikisha kwamba wanaweka utaratibu kama huu wa kuweka gharama ya kumuunganishia mtu maji?

Mheshimiwa Spika, kwa sababu sasa hivi kule MUWASA na RUWASA natumaini na mamlaka nyingine za maji zitatoza 350,000 mpaka 600,000 kumuunganishia mtu maji. Sasa je, mtu ataweza kweli kuvuta maji kupeleka nyumbani? Kwa hiyo watu wameamua kuanza kunywa maji ya mfereji ambapo hiyo haisaidii…

SPIKA: Ahsante sana Mheshimiwa swali lako limeeleweka.

MHE. DKT. CHARLES S. KIMEI: Mheshimiwa Spika, ahsante.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Dkt. Kimei, Mbunge wa Vunjo, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Serikali imeweka utaratibu wa gharama za maji kupitia Sera yetu iliyoko pale Wizara ya Maji. Utaratibu huu tumeanzisha taasisi zitakazotoa huduma za maji sasa hivi tumezipeleka mpaka wilayani tunaita RUWASA, taasisi ambazo zinashughulikia maji vijijini.

Mheshimiwa Spika, kutokana na upatikanaji wa maji kupitia mahali ambako kuna vyanzo, naweza kukiri kwamba tunaweza kuwa tuna ugumu kidogo wa upatikanaji wa maji kwa ujumla wake, lakini pamoja na ugumu huo wa upatikanaji wa maji kwenye baadhi ya maeneo kwa kutokuwa na vyanzo, bado tumeweka viwango vya kawaida ili wananchi waweze kupata huduma. Malengo yetu ni kila mwananchi mpaka kwenye ngazi za vitongoji aweze kupata maji. Kwa sasa sera yetu inafika vijijini.

Mheshimiwa Spika, kazi kubwa inafanywa ya zile RUWASA kuainisha vyanzo na gharama ya kuanzisha miradi hiyo. lakini pia na Wizara ya Maji nayo kuwekeza kwenye mamlaka hizo ili kupata maji ya kutosha mpaka kwenye ngazi za vijiji.

Mheshimiwa Spika, natambua yako malalamiko ya bei ambayo pia hata wakati tulipokuwa kwenye ziara tumeona baadhi ya maeneo bei zinatofautiana kutoka eneo moja mpaka eneo lingine. Wizara ya Maji inaendelea na utaratibu wa kuona, je, tunaweza kuwa na kiwango kimoja nchi nzima kama vile ambavyo tumefanya kwenye REA kulipa Sh.27,000 ili mtu apate kuvutiwa maji?

Mheshimiwa Spika, kazi hiyo itakapokamilika, Wizara ya Maji itakuja hapa itatuambia sasa uvutaji wa maji kutoka kwenye chanzo au mahali ambapo unaweza kuunganisha kuleta nyumbani ni kiasi gani. Tutakapokuwa na maji mengi tutatamani sana kila mmoja avute bomba apeleke nyumbani kwake, lakini kwa sasa kwa kiwango hiki cha maji tunajenga vituo ili wananchi wote waweze kwenda hapo kwa ajili ya kupata maji.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo suala litakapokamilika na kiwango cha maji kikipatikana kwa wingi sasa tutakuja kuweka viwango vya kila mmoja kuvuta maji kupeleka nyumbani kwake. Huo ndiyo mkakati wa Serikali kwa sasa. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister