Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 7 2021-02-04

Name

Tabasamu Hamisi Hussein Mwagao

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Sengerema

Primary Question

MHE. HAMIS H. T. MWAGAO: Mheshimiwa Spika, nakushukuru kwa kunipa nafasi na mimi nimuulize Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu akiwa ziarani Mwanza katika ziara yake ya kikazi alitoa tamko kwa nchi kuhakikisha wanafunzi wote wanakwenda darasani mwisho tarehe 28 mwezi wa pili. Tamko hilo liliungwa mkono na wananchi nchi nzima na wakuu wa mikoa wakalisimamia, wakuu wa wilaya wamelisimamia tunamshukuru Mwenyezi Mungu. Majengo yamejengwa, kuna maboma mengi katika nchi hii yamekamilika.

Mheshimiwa Waziri Mkuu nini tamko la Serikali kuhusiana na pesa za kumalizia haya majengo kwa nchi nzima ili watoto wote waingie kutokana na idadi ya siku uliyokuwa umetoa tarehe 28 Februari? Ahsante. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Tabasamu, Mbunge wa Sengerema kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, uko ukweli kwamba Halmashauri zetu zimekuwa zikifanya kazi za ukamilishaji wa maboma haya kama jambo la dharura kila mwaka, lakini sasa tumefika tumeziagiza Halmashauri hizi kuhakikisha kuwa wana mpango wa muda mrefu wa kudumu unaosimamia ujenzi wa miundombinu hii ikiwemo madarasa, matundu ya vyoo, nyumba za walimu kwenye shule zetu ili jambo hili lisiwe la zima moto kila mwaka. Kwa kutumia pia takwimu tulizonazo Halmashauri zote zinajua kila mwaka zina wanafunzi wangapi wa darasa la saba wanaotaka kumaliza mwaka huo na ambao wanaweza kufaulu.

Mheshimiwa Spika, upo utaratibu walimu wanautumia kujua wangapi wanaweza kufaulisha. Kutokana na takwimu hiyo inaweza kuifanya Halmashauri ikajiandaa kujenga vyumba vya madarasa na miundombinu nyingine. Lakini pia hata kwa sekondari wanapomaliza kidato cha nne wanaweza kutabiri tutakuwa na idadi ya wanafunzi wangapi ambao wanaenda kidato cha tano. Halmashauri ikamudu kujipanga vizuri kujenga miundombinu ya kuwapokea kidato cha tano. Jambo hili sasa limeenda sambamba na agizo ambalo nimelitoa.

Mheshimiwa Spika, lakini kama ulivyosema tumekuta maboma mengi yamejengwa na wananchi hajakamilishwa na umetaka kujua mpango wa Serikali wa kuhakikisha kwamba tunakamilisha majengo hayo. Bado kwanza tumetoa wito kwa Halmashauri zenyewe kupitia mapato yao ya ndani na kupitia mipango yao kukamilisha maboma yaliyojengwa na wananchi ili tuwe na miundombinu ya kutosha kila mwaka tuweze kupata nafasi ya kuingiza wanafunzi. Lakini kupitia pia bajeti inayoandaliwa na Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo haitoshi kumaliza maboma yote huwa tunaunga mkono juhudi za wananchi na Halmashauri kwa kukamilisha maboma yaliyopo kwa ajili ya kutoa nafasi ya wanafunzi wanaojiunga upya kwenye maeneo haya ili kila mwanafunzi ambaye anapata nafasi ya kuendelea na masomo aende kwa wakati bila ya kuwa na awamu ya kwanza na ya pili na kuendelea huko mwishoni.

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo niseme tu kwamba pale ambapo uwezo wa Serikali unaendelea, tutaendelea ku- support, kuunga mkono jitihada za Halmashauri na wananchi katika kukamilisha maboma, lakini awali kabisa Halmashauri zenyewe zijiwekee mpango endelevu wa kuhakikisha kwamba unapata miundombinu ya kutosha ili wanafunzi hawa waweze kuingia kwenye majengo haya ili kusiwe tena na maagizo, maagizo. Kwa sababu itakuwa kila mwaka Waziri Mkuu au Makamu wa Rais au Mheshimiwa Raisa toe maagizo ya kila mwaka, jambo hili halikubaliki na sasa tumewaambia wajipange vizuri ili tuwe na miundombinu endelevu. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana Mheshimiwa Tabasamu, Halmashauri zote zimesikia na kila Halmashauri imeagizwa iwe na mpango wa muda mrefu wa kuhakikisha kwamba miundombinu inajengwa kila mwaka na kila wanafunzi wanapofaulu wanaingia moja kwa moja bila ya maagizo. Ahsante sana kwa kunisikiliza. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister