Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 5 2021-02-04

Name

Kunti Yusuph Majala

Gender

Female

Party

CHADEMA

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. KUNTI Y. MAJALA: Mheshimiwa Spika, nikushukuru kwa kunipatia na mimi nafasi ya kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tangu nchi yetu imepata uhuru, Watanzania zaidi ya asilimia 75 ni wakulima kutokana na Serikali kutangaza kilimo ni uti wa mgongo lakini wakulima wetu hawa ambao ni Watanzania wameendelea kulima kilimo cha kutegemea mvua ya Mwenyezi Mungu ambacho kimekuwa hakina tija kwao wala tija kwa Taifa letu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, nini mkakati wa Serikali wa kuwatoa Watanzania wakulima kwenye kilimo hiki kisichokuwa na tija kwao na kwa Taifa letu kuwapeleka kwenye kilimo ambacho kitaweza kutuondoa Watanzania kwenye wimbi la umaskini na kwenda kufikia sasa kwenye uchumi wa kati ambao utakaokwenda kukidhi mahitaji ya muonekano kwa Watanzania wetu? Nakushukuru.

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Kunty Mbunge wa Viti Maalum kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, upo ukweli kwamba Serikali yetu sasa hivi inasisitiza kilimo ili kiweze kutoa manufaa au tija kwa wale wanaolima na wito huu wa kulima mazao haya ya biashara na chakula ni mkakati ule ule wa kuongeza tija kwa kilimo chetu. Ni kweli kwamba tukitegemea kilimo kinachotegemea hali ya hewa kama mvua pekee hatuwezi kupata tija. Nini tumekifanya Serikali.

Mheshimiwa Spika, Serikali ina taasisi au Kurugenzi ya Umwagiliaji ambayo yenyewe tumeipa bajeti ya kuhakikisha kwamba wanahakikisha tunafufua kilimo cha umwagiliaji nchini kitakachomwezesha mkulima kulima wakati wote masika, lakini wakati wa kiangazi ili uzalishaji uwe mkubwa na mkulima anapolima apate mazao ya kutosha, akiamua kuyauza kama atapata ziada, atapata uchumi lakini pia kumhakikishia usalama wa chakula pale anapozalisha, lakini kama ni zao tu la biashara kuendelea kumtafutia masoko. Kwa hiyo, mkakati wa Serikali katika hili ni kuhakikisha kwamba tunakuwa na kilimo cha aina zote mbili cha kutegemea hali ya hewa ya mvua lakini pia na umwagiliaji ambao pia tumeimarisha na tunaendelea pia kubaini maeneo yanayofaa kwa umwagiliaji na kuanzisha miradi hiyo.

Mheshimiwa Spika, nitoe mfano, Mheshimiwa Kunti yeye anatoka Chemba, Chemba ni eneo ambalo limepitiwa na mto mkubwa sana ambao unatiririsha maji mpaka maeneo ya Bahi. Mto ule unapitisha maji masika pamoja na kiangazi. Mkakati ambao tunao maeneo yote yanayopita maji yale kwenye mto pembezoni tunaona wakulima wapo ambao wanalima. Sasa tunawaanzishia miradi ya umwagiliaji ili wakulima hao waweze kulima kilimo ambacho kitawapatia fursa ya kutosha ili waweze kunufaika na kilimo hicho. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, malengo yetu kilimo chetu nchini kiwe na tija kwa wakulima, kituletee mazao ya chakula ya kutosha, pale ambapo wanalima mazao ya kibiashara basi wapate mazao ya kibiashara ya kutosha. Kwa ujumla wake tutaanza kuleta tija kwa wakulima, lakini pia kwa nchi na kuifanya nchi yetu kuwa na usalama wa chakula cha kutosha kwa kulima chakula cha kutosha na ziada. Huo ndiyo mpango wa Serikali kuhakikisha kwamba Serikali na wananchi wake wanalima kilimo hiki. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister