Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 2 2021-02-04

Name

Shanif Mansoor Jamal

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Kwimba

Primary Question

MHE. SHANIF M. JAMAL: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana, umenipa nafasi nami niulize swali kwa Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa Serikali imetoa waraka kwamba mazao aina ya choroko, dengu na kadhalika kwa msimu huu yatanunuliwa na AMCOS kwa mkopo bila bei elekezi na watapeleka kwenye minada ya TMX na hatujui lini minada itatokea; na kwa kuwa wananchi wa Wilaya ya Kwimba ni wakulima wadogo wadogo ambao wamezoea kuuza sokoni kwa kilo tano, kilo kumi mpaka kilo 20 na wakishauza wanapata fedha cash wanakwenda kununua mahitaji yao kama chakula na kupeleka kwenye familia zao; hawa watu wanateseka kwa sasa hivi.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kwa kuwa wafanyabiashara wapo sasa hivi ambao kila mwaka walikuwa wananunua mazao hayo kwa cash, kwa bei ya soko na wakulima walikuwa wanapata fedha taslimu (cash), kwa nini wasiruhusiwe kuendelea kununua mazao hayo wakati AMCOS wanajiandaa kuwa na fedha taslimu ya kulipa kwa wakulima ili tupate ushindani? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Mansoor, Mbunge wa Kwimba kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, Mheshimiwa Mbunge ameeleza kwamba upo waraka unaoelekeza kununua mazao ya choroko kwa mkopo. Sina uhakika kama kweli Wizara iliagiza inunue kwa mkopo, ila ninachojua ambacho pia nimekipatia taarifa na tumeagiza pia Wizara ya Kilimo ifanyie kazi, ni pale ambapo Wizara ya Kilimo imeagiza Wakuu wa Mikoa na Wakuu wa Wilaya kusimamia kuwepo kwa ushirika kwa wakulima, iwe ni mahali ambapo wanaweza kuuza mazao yao kwa Mfumo wa Stakabadhi Ghalani ambao maeneo kadhaa ambayo wananchi wake hawajapata elimu kwa ule Mfumo wa Stakabadhi Ghalani inaonekana kama vile ni mkopo.

Mheshimiwa Spika, mfumo huu unawataka wakulima kukusana mazao, kuyaweka pamoja halafu kusubiri siku moja kutangaza soko. Kwa hiyo, kitendo kile cha wakulima kukusanya mazao na kuyaweka pamoja kusubiri soko, zile siku ndiyo inapotafsiriwa kwamba tayari wamekwenda kuuza na wamekopwa, kumbe mauzo bado, ndiyo mfumo wa Stakabadhi Ghalani. Sasa mgogo huu nimeusikia pia Mkoani Mwanza, Simiyu, Mara kwenye mazao haya na Shinyanga kwenye zao hili la choroko.

Mheshimiwa Spika, nataka niseme, kama waraka ulitoka kwenda kuwaagiza Wakuu wa Mikoa wasimamie hili, mfumo huu kabla haujatekelezwa ni lazima wakulima wapate elimu ili waweze kuelewa mfumo huu unakuwaje? Kama hakuna elimu, kunatokea malalamiko haya, kwa sababu uzoefu pia, hata kwenye mazao kama korosho, mfumo ulipoanza kulikuwa na migongano mingi ambayo ilipelekea kutoelewana na wananchi, wakaanza kuilalamikia Serikali kwa kauli hiyo hiyo kwamba wanakopwa.(Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, naagiza sasa mikoa yote ambayo inanunua mazao haya ya choroko na dengu, zao ambalo wazalishaji wengi wanazalisha kama alivyosema kilo tano, sita, saba; ili ukusanye dengu iweze kupata mzigo mkubwa na utangaze mnada, lazima itachukua siku nyingi. Kwa hiyo, kwa zao hili ni tatizo kidogo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nasema Wakuu wa Mikoa waridhie kwanza eneo hili la choroko na dengu ambalo uzalishaji wake ni mdogo mdogo, ni muhimu tukaufikiria upya kuanza kwake tofauti na mazao yanayopatikana kwa wingi kama vile korosho, chai, pamba, kahawa na mazao yale yanayozalishwa kwa wingi, yale inawezekana ukakusanya siku mbili ukapata mzigo mkubwa na kuuza kwenye mnada na kuwa na siku chache sana kufikia siku ya mauzo na mwananchi hawezi kulalamika. Ila fiwi, choroko na dengu ni zao ambalo linalimwa kwenye ekari moja, mtu anavuna kilo mbili. Sasa ukimpeleka kwenye mnada mpaka akae upate mzigo wa kutangaza mnada, lazima atalalamika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, kwenye eneo hili, naiagiza Wizara ya Kilimo ifanye mapitio tena ya waraka huo na ione mazingira ambako wananchi wanaona kama wanakopwa, lakini kumbe ni subira ya kusubiri siku ya mnada kwa uchache wa zao lenyewe ili Mfumo wa Stakabadhi Ghalani, tuanze na mazao yale ambayo yanapatikana kwa wingi. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kama kuna maeneo wameshaanza, wao waendelee kwa sababu mfumo huu umekuja kututhibitishia kwamba unaleta bei nzuri sana ya zao siku ya mnada kwa sababu mnada ule unashindanisha wanunuzi. Kila mmoja anakuja na bei yake na wakulima watakuwa na uhuru wa kumchagua mnunuzi aliyeweka bei ya juu.

Mheshimiwa Spika, kumbukumbu zetu zinaonesha, zao hilo hilo limewahi kuuzwa mpaka shilingi 600/= mpaka shilingi 700/=, lakini baada ya mnada lilienda mpaka shilingi 900/=, shilingi 1,200/= na zaidi, hasa pale Mkoani Shinyanga ambako walishaanza. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo, Wizara ya Kilimo ifanye mapitio tena kwenye eneo hili halafu tuwape mrejesho Waheshimiwa Wabunge na wananchi wajue ni nini kinatakiwa kifanyike kwenye mazao haya. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister