Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2021-02-04

Name

Joseph Kasheku Musukuma

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Geita

Primary Question

MHE. JOSEPH K. MUSUKUMA: Mheshimiwa Spika, nakushukuru sana kwa kunipa nafasi niweze kumuuliza swali Mheshimiwa Waziri Mkuu.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, tarehe 24 Oktoba, 2019 Mheshimiwa Rais alitoa agizo kwa Halmashauri za vijijini ambazo zilikuwa zinakaa mjini kwamba ndani ya siku 30 ziweze kurudi kwenye maeneo husika ili kutoa huduma karibu na wananchi. Baada ya siku 30 Halmashauri nyingi zilitekeleza agizo hilo.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, kumekuwa na shida, inaonekana kama kuna kukaidi agizo la Mheshimiwa Rais, kwani wamehamisha ofisi lakini makazi bado wanarudi kulala mjini, hata kama kule walikohamia kuna nyumba na inapelekea Halmashauri kuzipa mzigo wa kugharamia mafuta kila siku ya kurudisha watumishi kwenda kulala mjini.

Je, ni nini kauli ya Serikali kwenye Halmashauri hizo ambazo zimerudi vijijini na watumishi wanarudishwa kulala mjini? (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nakushukuru. (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, kwanza tumshukuru Mwenyezi Mungu kwa hatua tuliyofikia leo ambapo tuko kwenye Kikao cha Tatu.

Mheshimiwa Spika, naomba nijibu swali la Mheshimiwa King Musukuma, Mbunge wa Nzela, Geita Vijijini, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Mheshimiwa Rais alitoa maagizo kwa Halmashauri za Wilaya zote ambazo zilikuwa na Makao Makuu yake kwenye Makao Makuu ya Halmashauri za Miji kuhama mara moja na kwenda kwenye Makao Makuu huko ambako wananchi wa Halmashauri waliko, waweze kuwahudumia kwa karibu.

Mheshimiwa Spika, agizo hili Halmashauri nyingi zimetekeleza na mimi nimepata bahati ya kupita kwenye baadhi ya Halmashauri, kwa wafanyakazi wenyewe kwa kuhamisha ofisi zao na kuhamishia kwenye maeneo hayo mapya, lakini na wao wenyewe kuishi huko.

Mheshimiwa Spika, tunatambua yapo maeneo yenye changamoto; hatuna nyumba za kutosha kwa ajili ya makazi yao, lakini kuna Halmashauri ambazo zina nyumba za watumishi na wananchi wanazo nyumba ambazo zinaweza kupangishwa na hili lilikuwa agizo la Mheshimiwa Rais; na agizo la Mheshimiwa Rais ni agizo ambalo linatakiwa litekelezwe mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, pia kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge Musukuma alivyosema kwamba huko kuna makazi, kutokwenda ni kuvunja amri, kukataa amri ya Mheshimiwa Rais. Ni kosa kubwa sana kwenye utumishi wa umma. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, nataka niwaagize Wakuu wa Mikoa akiwemo na Mkuu wa Mkoa wa eneo ambako Halmashauri iliyotakiwa kuhama ilipo, Katibu Tawala wa Mkoa ambaye pia ni Mtendaji Mkuu kwenye Mkoa huo, ambapo kwenye Halmashauri zenye mazingira hayo ambayo watumishi wametakiwa waondoke kwenda kwenye makao mapya hawajaenda, waondoke mara moja. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa sababu kipindi cha kuondoka kilishatamkwa na Mheshimiwa Rais, kwa hiyo, hatuna sababu ya kuwapa muda tena. Ni kuondoka mara moja baada ya tamko hili. Endapo hawatafanya hivyo, Mkuu wa Mkoa wa Mkoa husika achukue hatua mara moja dhidi ya watumishi hao na hasa wale wote ambao hawataki kwenda kwenye maeneo mapya. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, baada ya kuwa tumeagiza haya, naagiza pia Ofisi ya Rais, TAMISEMI ambayo pia inasimamia Halmashauri hizi, kufuatilia kila Halmashauri iliyotakiwa kuhama kwenye maeneo ya zamani, kuhamia kwenye maeneo mapya ili watumishi wote waweze kuhamia na nitahitaji taarifa hizo keshokutwa Jumamosi, ofisini kwangu saa 4.00 asubihi ili nijue ni Halmashauri gani ambayo bado watumishi hawajahama, ili tuchukue hatua nyingine za kinidhamu kwa watumishi hao. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister