Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2020-2025 Session 2 Sitting 2 Energy and Minerals Wizara ya Madini 15 2021-02-02

Name

Tumaini Bryceson Magessa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Busanda

Primary Question

MHE. BRYCESON T. MAGESSA Aliuliza:-

STAMICO inamiliki maeneo yenye dhahabu lakini haiyatumii huku wachimbaji wadogo wakiwa hawana maeneo ya kuchimba.

Je, kwa nini Serikali isiwapatie wachimbaji wadogo maeneo hayo?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI Alijibu:-

Mheshimiwa Spika, napenda kujibu swali la Mheshimiwa Bryceson Tumaini Magessa, Mbunge wa Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, miongoni mwa majukumu ya Shirika la Madini la Taifa (STAMICO) ni kuwaendeleza wachimbaji wadogo nchini. Katika kufanya hivyo Shirika limekuwa likifanya kazi kwa karibu sana na wachimbaji hao katika kuhakikisha kwamba wanaongeza uzalishaji katika maeneo wanayochimba. Kupitia mkakati huo, Shirika pia limekuwa likitoa maeneo yake kuwapatia wachimbaji wadogo kwa lengo la kuwaendeleza.

Mheshimiwa Spika, mwaka 2018, Shirika lilitoa maeneo ya uchimbaji kwa vikundi 15 vya wachimbaji wadogo vilivyoundwa katika eneo la Lwamgasa (Geita) kwa usimamizi wa viongozi wa Kijiji na Afisa Ushirika yenye ukubwa wa kilomita za mraba 0.08. Vilevile, mwaka 2019, Shirika liligawa pia eneo la leseni ya Buhemba kwa vikundi vya wachimbaji wadogo waliopo Ilasaniro Mkoani Mara lenye ukubwa wa kilomita za mraba 1.2 na jumla ya leseni ndogo za uchimbaji 15 ziligawiwa. Aidha, kwa kushirikiana na mbia Shirika lilitoa leseni tatu katika eneo lake la mradi wa Buckreef (Geita) kwa wachimbaji wadogo wa maeneo hayo yenye jumla ya kilomita za mraba 7.2.

Mheshimiwa Spika, hata hivyo kwa sasa hakuna maeneo ambayo yanamilikiwa na STAMICO bila kuendelezwa. Shirika linaendelea kuendeleza maeneo yake kwa kufanya utafiti ili kujua kiwango cha mbale kilichopo kabla ya kuanza uchimbaji. Pia Shirika limeanza kuendeleza leseni yake ya dhahabu ya Buhemba kwa kushirikiana na mbia na uzalishaji unatarajiwa kuanza Septemba mwaka huu 2021. Ahsante.

Additional Question(s) to Prime Minister

Name

Tumaini Bryceson Magessa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Busanda

Question 1

MHE. BRYCESON T. MAGESSA: Mheshimiwa Spika, pamoja na majibu mazuri ya Mheshimiwa Waziri, je, ni lini atakuwa tayari yeye na STAMICO twende kupitia katika maeneo ambayo mimi najua bado kuna tatizo ili tuweze kumaliza matatizo yaliyopo kule?

Mheshimiwa Spika, swali la pili, kwa kuwa STAMICO kazi yake, pamoja na majukumu mengine, ni kuwaendeleza wachimbaji wadogo. Wachimbaji wadogo waliopo Busanda wengi wanabahatisha kujua dhahabu iko wapi. Je, ni lini STAMICO itakuwa tayari ama kuwakodisha vyombo au kujitolea ili waweze kutambua mahali wanapochimba kuna madini au hakuna badala ya kubahatisha?

Name

Prof. Shukrani Elisha Manya

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Nominated

Answer

NAIBU WAZIRI WA MADINI: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la nyongeza la Mbunge Tumaini Magessa kutoka Jimbo la Busanda, kama ifuatavyo: -

Mheshimiwa Spika, baada ya kikao hiki nimtaarifu tu Mheshimiwa Mbunge kwamba Wizara ipo tayari kutembelea Jimboni kwake na kuona maeneo wanayodhani kama yanahitaji kugawiwa kwa wachimbaji wadogo au la.

Mheshimiwa Spika, lakini pia Mheshimiwa Mbunge ajue kwamba Serikali imeendelea kuyatoa haya maeneo kila inapoona kuwa inafaa. Nadhani hata yeye mwenyewe katika jimbo lake ni shahidi kwamba maeneo mengi yameendelea kutengwa na kwamba Serikali ya Awamu ya Tano imewathamini sana wachimbaji wadogo na ndipo wakati ambapo wachimbaji wadogo nchini wamepewa maeneo mengi sana kwa ajili ya kuchimba.

Mheshimiwa Spika, swali la pili, sasa hivi Serikali inaendelea kuimarisha Shirika letu la STAMICO na siku za karibuni shirika limeweza kununua mitambo ya drilling ya kwake yenyewe. Kwa jinsi hiyo, tunaamini kwamba jitihada hizi zinazochukuliwa na Serikali za kuimarisha Shirika la STAMICO zitawezesha sasa kuweza kupata namna ya kuwasaidia wachimbaji wadogo kwa kufanyia utafiti ili sasa tunapoelekea maeneo yanayotengwa yawe ni yale ambayo yamefanyiwa tafiti na hatimaye kuwawezesha kuchimba kwa tija. Ahsante sana.