Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 16 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 1 2019-09-12

Name

Rashid Abdallah Shangazi

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Mlalo

Primary Question

MHE. RASHID A. SHANGAZI: Mheshimiwa Spika, ahsante sana kwa nafasi hii.

Mheshimiwa Waziri Mkuu, Serikali ya Awamu ya Tano imehamasisha sana shughuli za kilimo na wananchi wamehamasika sana, lakini hivi karibuni limetokea tatizo kubwa sana la ufungaji wa mazao kwa mtindo wa lumbesa lakini pia kuwepo na vifungashio ambavyo havina viwango stahiki. Jambo la kusikitisha sana ni kwamba Mamlaka za Serikali, hasa Wakala wa Vipimo na Mizani, pia Serikali katika ngazi za Halmashauri, Wilaya na Mikoa zimeshindwa kabisa kudhibiti tatizo hili la ufungaji wa mazao kwa mtindo wa lumbesa. Je, Serikali ipo tayari kuanzisha operesheni maalum nchi nzima kudhibiti tatizo hili ambalo kwa kweli linawanyong’onyeza wakulima na kuwaletea lindi la umaskini? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Shangazi, Mbunge wa Mlalo kule Lushoto, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, ni kweli kwamba Serikali imeendelea kusisitiza wakulima wetu nchini wanapolima mazao yao waweze kunufaika kutokana na masoko yaliyo sahihi. Tunaanza kuona baadhi ya wanunuzi kutofuata sheria, kanuni na taratibu za manunuzi ya mazao hayo pindi wanapokwenda kwa wakulima.

Mheshimiwa Spika, nimefanya ziara Wilaya ya Karatu eneo maarufu linalozalisha mazao la Lake Eyasi, eneo la Eyasi kule chini. Moja kati ya malalamiko ambayo wakulima waliyatoa ni kama ambavyo Mheshimiwa Shangazi ameeleza, lakini Serikali imeweka utaratibu wa mazao yote yanayolimwa na kuingia kwenye masoko, lazima masoko hayo yatumie vipimo halisi ili liweze kulipa bei stahiki na mkulima aweze kunufaika. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, tunaposema vipimo stahiki maana yake kuna vipimo ambavyo tunavitumia, inaweza kuwa ni kipimo cha ndoo ambazo tunajua kuna ndoo za lita tano, kumi, ishirini, na ni rahisi pia kukadiria na bei ambayo inawekwa na wakulima inakuwa ndiyo bei sahihi. Pia kuna vifungashio kama vile magunia ya kilo hamsini, kilo mia, nayo pia ni sehemu ya vipimo halisi lakini muhimu zaidi ni kutumia mizani ambayo haina utata.

Mheshimiwa Spika, sasa imetokea wanunuzi kuwalazimisha wakulima baada ya kile kipimo halisi kuongeza tena nundu inayojulikana kwa jina la lumbesa kama ambavyo Mheshimiwa Mbunge ameeleza, hii haikubaliki. Tumetoa maelekezo sahihi kwa Wakuu wa Mikoa wote, Wakuu wa Wilaya wote, Wakurugenzi na Maafisa Kilimo na Maafisa Ushirika wanaosimamia masoko kwenye ngazi hizo za wakulima wawe wasimamizi wa biashara inayofanywa na wanunuzi kwa mkulima pindi anapouza mazao yake ili kujiridhisha kwamba vipimo vyote vinatumika na siyo kuongeza nundu zaidi ya kipimo ambacho kinatakiwa, kwa sababu kufanya hivyo tunamnyonya mkulima na mkulima anapata hasara kwenye mazao hayo. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, kwa hiyo utayari wa Serikali upo na tumeshatoa maelekezo kwa Wakuu wa Wilaya. Kwa hiyo nirudie tena kutoa wito kwa Maafisa Kilimo, Ushirika, Wakuu Wa Wilaya, Wakuu wa Mikoa kwenye maeneo yao wasimamie biashara hii na kuendesha operesheni kwenye maeneo yote ya masoko ili kujiridhisha kwamba mazao yetu yananunuliwa kwa vipimo kama ambavyo vimekubalika. Huo ndiyo msisitizo wa Serikali na tutaendelea kusisitiza wakati wote. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister