Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 8 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 4 2020-02-06

Name

Zaynab Matitu Vulu

Gender

Female

Party

CCM

Constituent

Special Seats

Primary Question

MHE. ZAYNABU M. VULU: Mheshimiwa Naibu Spika, ahsante sana kwea kunipa nafasi ya kuweza kumuuliza Mheshimiwa Waziri Mkuu swali; na nianze kwa kutoa pole kwa waathirika wote wa mafuriko.

Mheshimiwa Naibu Spika, swali langu ni kwamba; Mheshimiwa Waziri Mkuu, tumeshuhudia mvua zinazonyesha na zinazoendelea kunyesha. Tumeshuhudia maafa mbalimbali, vifo, watu kukosa maeneo ya kuishi, kupoteza mali zao, kuharibika kwa miundombinu, lakini pia watu wale hawana vyakula. Je, Serikali sasa ina mkakati gani wa kuweza kuwasaidia watu hao ambao wameathirika na mafuriko hayo na pia, kuboresha miundombinu nchini kwetu? (Makofi)

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Naibu Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Zaynabu Vulu, Mbunge Mkoa wa Pwani, kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Naibu Spika, kwanza nami niungane na Mheshimiwa Rais Dkt. John Pombe Magufuli kwa kutoa pole kwa waathirika wote a mafuriko nchini kwa maeneo yote ambayo yamekumbwa na tatizo hili la mafuriko. Pia Mheshimiwa Mbunge na yeye ametioa pole ni jambo zuri, jambo jema kwa sababu, wako Watanzania wamekumbwa na hali hiyo.

Mheshimiwa Naibu Spika, na kwa bahati nzuri jana nilikuwa Mkoani Lindi, Wilaya ya Kilwa ambako kulikuwa na mafuriko pia. Nimetembelea kwenye maeneo yote nimeona hali ilivyo, ingawa angalao sasa maji yamepungua kwenye maeneo yale yamebaki tu yanayotiririka kwenye mito.

Mheshimiwa Naibu Spika, ni kweli uharibifu mkubwa umejitokeza, kwanza wenzetu wametangulia mbele za haki na kwa kweli tuungane na Watanzania wote, Mungu aweke roho zao mahali pema peponi, amina. Mbili, tumeona watu wamepoteza nyumba, vyakula na miundombinu mbalimbali imeharibika ikiwemo na barabara na njia nyingi zimejifunga. Nataka niwaambie Watanzania, kwamba mwaka huu mvua ni nyingi sana, na Taasisi yetu ya Hali ya Hewa imeendelea kutuhabarisha kwamba, mvua ndio zinaanza. Sasa kama ndio zinaanza kwa hali hii tutarajie tutakuwa na matukio mengi makubwa zaidi ya haya ambayo tumeyapata.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, tunapopata taarifa za wingi wa kiasi cha mvua mwaka huu sisi wenyewe tunatakiwa tuchukue tahadhari. Wale wote waliokaa kwenye maeneo hatarishi, na kwa kiwango hiki cha mvua na hali ambayo tumeiona na wanasema mvua bado inakuja; uko umuhimu na kweli nitoe wito; watu waondoke kwenye maeneo yale ya mabondeni. Kule iwe ni kazi za kilimo na kulishia mifugo, tusifanye maeneo hayo kuwa ni maeneo ya makazi kwa sababu kuna hatari tena ya kupoteza maisha ya wenzetu, nyumba, vyakula na athari nyingine inaweza kujitokeza.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, hawa ambao tayari wamekumbwa kwenye maeneo yao kama vile huko Lindi, Kilwa, Liwale, Lindi Vijijini; pia Pawaga kule Iringa, Chikuyu Wilayani Manyoni, Magu Mwanza, Sengerema pamoja na Buchosa. Hayo maeneo yote ninayoyataja yana matatizo ya mafuriko. Kwa hiyo maeneo ni mengi na bado kuna mikoa sita ambayo mvua zitaanza kunyesha kwa wingi. Kamati za Maafa za Kata, Wilaya na Mikoa zipo zinafanya kazi yake na zinaendelea kutoa huduma kwa uwezo wao.

Mheshimiwa Naibu Spika, pale ambapo Kamati ya Maafa Mkoa inapokuwa na jambo kubwa sana wanatoa taarifa kwa Kamati ya Maafa ya Taifa ambayo iko Ofisi ya Waziri Mkuu nayo pia itasadia katika kuratibu.

Mheshimiwa Naibu Spika, pamoja na haya jambo hili ni la muda mfupi; muhimu zaidi tuanze kujiepusha kukaa kwenye maeneo hayo hatarishi ili kupunguza mzigo mkubwa ambao tutaupata. Haya yaliyotokea haya kamati za maafa zinafanya kazi nzuri, wakuu wa wilaya, viongozi wa kamati za wilaya, wakuu wa mikoa, kamati za mikoa, wameendelea kushirikiana na wale wote waathirika kuona mahitaji yao katika kipindi hiki kifupi na kazi inaendelea vizuri na taarifa tunaendelea kuzipokea.

Mheshimiwa Naibu Spika, kwa hiyo, Waheshimiwa Wabunge ambao pia mnatoka kwenye maeneo haya tunawapa pole na wananchi wetu tunawapa pole, lakini tuwahakikishie kwamba, kamati zetu za maafa zilizoko kwenye maeneo yale zinaendelea kushirikiana na wananchi huku tukiendelea kutoa wito wananchi wasirudi kwenye maeneo walikotoka ili kupunguza athari hii. Asante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister