Jamhuri ya Muungano ya Tanzania

Question to Prime Minister

Term Session Sitting Sector Ministry Qn No Date
2015-2020 Session 18 Sitting 3 Questions to Prime Minister Maswali kwa Waziri Mkuu 3 2020-01-30

Name

Jaku Hashim Ayoub

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

House of Representatives

Primary Question

MHE. JAKU HASHIM AYOUB:Mheshimiwa Spika, kwanza nichukue fursa hii kumshukuru Mwenyezi Mungu, na vilevile nimshukuru Mheshimiwa Waziri Mkuu kwa ziara yake aliyoifanya Tanzania nzima bila kujali mvua, jua wala kula, nami ni shahidi upande wa kula; hasa kwa upande wa pili wa Muungano; Mheshimiwa nikupongeze kwa dhati kabisa, ni Waziri Mkuu wa Tanzania ikiwemo Zanzibar na kama kuna kitu kilichonivutia Mheshimiwa Waziri Mkuu ziara uliyoifanya katika …

SPIKA: Swali lako Mheshimiwa Jaku.

MHE. JAKU HASHIM AYOUB: Mheshimiwa Spika, ahsante ziara uliyoifanya katika Kiwanda cha Sukari cha Mahonda, umeiona hali ile na ukatoa maagizo. Yale maagizo uliyotoa Mheshimiwa Waziri Mkuu ni sawasawa na maagizo ya Serikali ya Mapinduzi ya Zanzibar, kuwa sukari ile inunuliwe pale, ikiisha ndipo waruhusiwe watu kuagiza nje yaani ni maagizo sawasawa uliyoyatoa wewe. Lakini kelele za mlango hazimkeri mwenye nyumba, wewe ndiyo mwenye nyumba zile kelele ulizozikuta pale zisikushughulishe soko kubwa la walaji liko Tanzania Bara.

Je, ni lini mtafikiria angalau ile bidhaa kama zinavyotoka hapa ni saruji ikiwemo Tanga cement, Twiga, Dangote, kiboko na mabati yanakwenda katika soko dogo la Zanzibar angalau nusu yake likaja katika soko lile…?

Name

Kassim Majaliwa Majaliwa

Gender

Male

Party

CCM

Constituent

Ruangwa

Answer

WAZIRI MKUU: Mheshimiwa Spika, naomba kujibu swali la Mheshimiwa Jaku, Mbunge kama ifuatavyo:-

Mheshimiwa Spika, kwanza nishukuru kwa kutambua jitihada kubwa tunazozifanya. Si mimi bali ni Serikali yetu; imeweka huo mpango na utaratibu wa kuwafikia wananchi popote walipo. Kwa hiyo ziara zangu ni utekelezaji wa mkakati wa Serikali wa kuwafikia wananchi kule waliko.

Mheshimiwa Spika,ni kweli nimefanya ziara kwenye Kiwanda cha Mahonda Mkoa wa Kaskazini Unguja; na nimepita ndani ya kiwanda nimeona, nimeenda mpaka Bohari tumekuta sukari nyingi bado imebaki. Kiwanda kile kinao uwezo wa kuzalisha tani 24,000 na sasa hivi kinazalisha tani 6,000. Mahitaji ya Unguja na Pemba ni tani 36,000. Hata hivyo nimeikuta sukari ghalani na bado mwekezaji wetu analalamika kwamba hana soko. Kwa kweli nililazimika kuwa mkali kidogo.

Mheshimiwa Spika, wakati Serikali inahamasisha wawekezaji kuja kuwekeza hapa na tumewahakikishia kuwa na masoko na kuwalinda, lakini bado hatumpi masoko; na hatumpi masoko kwa sababu tunakaribisha sukari nyingi ya nje kuingia halafu ya ndani inabaki. Kwa kufanya hilo tutakuwa hatumtendei haki yule mwekezaji.

Mheshimiwa Spika, ni vyema; umesema kwamba unahitaji soko pia na Bara, lakini palepale ilipo inapozalishwa sukari mahitaji ni tani 36,000, lakini hizo tani 6,000 hazijanunuliwa zimebaki bohari, mwekezaji anahangaika, anatafuta masoko, haiwezekani!

Mheshimiwa Spika, na mimi nilitumia lugha ile kwamba mpango huu si sahihi, mbovu kwa sababu kwanza tungehakikisha hizi tani 6,000 za ndani zinanunuliwa halafu uagize nyingine. Kama tani ni 36,000 ndiyo mahitaji ya eneo, kwanza tani 6,000 zingetoka; na wale waagizaji basi wangepewa masharti ya kwanza kuinunua sukari ya ndani halafu unawapa kibali cha kuweka top up.Sasa kuagiza sukari yote ya nje iwe inakuja ndani haiwezekani. (Makofi)

Mheshimiwa Spika, mimi kama Waziri Mkuu mwenye wajibu pia hata kwa chama changu kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi; mimi kwa pamoja na Makamu wa Pili wa Rais Zanzibar ndio wenye jukumu la kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi. Suala la viwanda liko kwenye Ilani ya Chama cha Mapinduzi na ninapaswa kwenda popote Tanzania kufuatilia utekelezaji wa Ilani ya Chama cha Mapinduzi, sina mipaka. Sasa leo ninapokuta mahali Ilani haitekelezeki lazima niwe mchungu na nitaendelea kuwa mchungu kwa kiasi hicho.(Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, lazima tuweke mpango wa kuwalinda wawekezaji wa ndani na kuwahakikishia masoko, na masoko tunayo. Pale naambiwa waagizaji wako watatu, kwa nini usiwape masharti angalau rahisi, ndio mpango mzuri. Waambie kwanza nunua tani 20,000 chukua tani 10,000 lete na mwingine, na mwingine, 6,000 tumezimaliza. Lakini unaagiza zote kutoka nje halafu huyu atauza wapi? Haiwezekani, haiwezekani. Halafu mtu anasema nimewachefua Wazanzibar; nimewachefua Wazanzibar au nimewachefua wanunuzi? (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, kwenye hili naomba nilieleze zaidi kile Kiwanda pale Mahonda kinawanufaisha wale wananchi wa Kaskazini Unguja kwa sababu wenyewe wanalima miwa, na soko lao ni kile kiwanda. Ukichukua sukari ya nje kama hainunuliwi wale wananchi miwa wanayolima haiwezi kupata soko unawaumiza Wazanzibar. Kile kiwanda kiko pale kinaajiri watumishi 400, wanufaika ni wale walioko Kaskazini Unguja; lakini leo usipouza huyu hawezi kuajiri, hawezi kulipa mishahara kwa sababu sukari iko bohari, haiwezekani! Leo kile kiwanda kiko pale kinalipa kodi, kodi ndiyo ile ambayo imeniwezesha kwenda kuona Kituo cha Afya kule Bambi, kituo cha afya kule Kizimkazi nimeona maabara nzuri imejengwa yenye viwango pale Bwejuu, nimeenda pia Unguja, Kaskazini Pemba nimekuta VETA inajengwa nzuri kwa sababu ya fedha ya kodi ya viwanda!Haiwezekani! (Makofi/Vigelegele)

Mheshimiwa Spika, mimi naamini Watanzania walinielewa na Watanzania hawa hata wenzangu wa Zanzibar nilichosema ni sahihi. Hao wanaotamka kwamba wamechefuliwa ni wanunuzi, na wala wasio wazanzibari. Sera yetu ni moja ya kuwalinda Watanzania, na tutaendelea kufanya hilo; tutakuwa wakali pale ambapo mambo hayaendi. Ahsante sana. (Makofi)

Additional Question(s) to Prime Minister